INGIENI KWA KUPITIA MLANGO ULIO MWEMBAMBA.

by Admin | 19 November 2019 08:46 pm11

Tuingie kwa kupitia mlango ulio mwembamba. Shalom. Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe. Karibu tuyatafakari pamoja maandiko…Bwana Yesu alisema maneno yafuatayo katika kitabu cha Luka..

Luka 13:22 “Naye alikuwa akipita katika miji na vijiji, akifundisha, katika safari yake kwenda Yerusalemu.

23 Mtu mmoja akamwuliza, Je! Bwana, watu wanaookolewa ni wachache? Akawaambia,

24 Jitahidini kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia, wasiweze.

25 Wakati mwenye nyumba atakaposimama na kuufunga mlango, nanyi mkaanza kusimama nje na kuubisha mlango, mkisema, Ee Bwana, tufungulie; yeye atajibu na kuwaambia, Siwajui mtokako;

26 ndipo mtakapoanza kusema, Tulikula na kunywa mbele yako, nawe ulifundisha katika njia zetu.

27 Naye atasema, Nawaambia, Siwajui mtokako; ondokeni kwangu ninyi nyote mlio wafanyaji wa udhalimu”

Moja ya sentensi zinazoogopesha ambazo Bwana Yesu alizizungumza ni hii..Nyingine ni ile ya Mathayo 12:31 anayosema…“ Kwa sababu hiyo nawaambia, Kila dhambi na kila neno la kufuru watasamehewa wanadamu, ila kwa kumkufuru Roho hawatasamehewa.”

Na nyingine ya Tatu ni hii…

Mathayo 7:22 “Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi?

23 Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu.

Sentensi hizi tatu alizozizungumza Bwana Yesu kama ukizitafakari kwa makini zinaogopesha sana..Sio za kuzichukulia kiwepesi wepesi kabisa.. Ni sentensi nzito sana. Na kama tunavyojua Bwana Yesu anachokisema siku zote ni lazima kije kutimia. Alimwambia Petro kabla Jogoo kuwika utanikana mara tatu…Na tunaona masaa machache tu mbeleni unabii huo ulitimia kama ulivyo. Kadhalika aliposema siku ile wengi watakuja na kumwambia Bwana Bwana hatukutoa pepo, hatukufanya unabii. Hatukufanya miujiza mingi kwa jina lako Ni kweli siku hiyo itafika na watakapokuja maelfu ya watu mbele zake na kusema hayo maneno hivyo hivyo.

Watakuwepo wahubiri wengi siku hiyo watakaosema maneno hayo mbele zake na Bwana atawakataa. Hivyo ni kujitahidi kuwa makini sana na kumwomba Bwana atusaidie siku zote hao watu wasiwe sisi. Kwasababu hakuna wa kusalimika hapo kama Neema yake haitahusika.

Lakini leo tutaitafakari sentensi hiyo ya kwanza ambayo alisema “Tujitahidi kuingia katika mlango ulio mwembamba”.

Tusome tena mahali pengine alipozungumza maneno hayo ili tupate picha Zaidi..

Luka 7:13 “Ingieni kwa kupitia mlango ulio mwembamba; maana mlango ni mpana, na njia ni pana iendayo upotevuni, nao ni wengi waingiao kwa mlango huo.

14 Bali mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani, nao waionao ni wachache.

Hapo kuna vitu viwili NJIA na MLANGO..Na anasema njia ni nyembamba, maana yake hiyo huwezi kupita kwa kifaa chochote kama gari au pikipiki. Wala hamwezi kupita ukiwa na mizigo, wala hawezi kupita mkiwa makundi. Ni mtu mmoja mmoja, kwasababu . Ulishawahi kupita kichochoroni na gari? Au na pikipiki?. Au ulishawahi kupita kichochoroni mkiwa mmeshikana mikono watu sita au 7 kwa pamoja?. Ni wazi kuwa hicho kitu hakiwezekani. Kwasababu njia ni nyembamba. Inahitajika apite mmoja mmoja. Na tena akiwa hana mizigo mizigo.

Kadhalika njia ya wokovu, ni habari ya mtu mmoja mmoja. Sio mtu na mke wake. Au mtu na baba yake. Inahitajika mtu kujikana nafsi peke yake na kuamua kumfuata Yesu. Na pia tunapomfuata Yesu yeye ni njia nyembamba hauendi na dini yako. Wala dhehebu lako litakalokusaidia kupita katika huo uchochoro. Unaweka dhehebu lako pembeni, dini yako pembeni. Unachukua msalaba wako unamfuata kama ulivyo.

Na pia anasema “MLANGO NI MWEMBAMBA”.

Maana yake mwisho wa hiyo NJIA nyembamba ya uchochoro ulio mwembamba utakutana na mlango. Na huo mlango pia ni mwembamba vile vile kama hiyo NJIA. Hapo ndipo Bwana anatuambia tujitahidi. Uchochoro utapita bila gari, bila baiskeli, bila pikipiki lakini mlangoni je?.

Hapo Itakubidi upunguze hata mwili. Kwasababu pengine mwili wako ukiwa mkubwa sana unaweza ukakwama mlangoni. Hivyo ili uingie itahitajika hata upunguze baadhi ya viungo..Ndio maana Bwana Yesu alisema.

Kiungo chako kimoja kikikukosesha kikate, Ni heri uingie katika ufalme wa mbinguni ukiwa kilema kuliko kuwa mzima na kuishia jehanamu.

Mathayo 5:30 “Na mkono wako wa kuume ukikukosesha, ukate uutupe mbali nawe; kwa maana yakufaa kiungo chako kimoja kipotee wala mwili wako mzima usitupwe katika jehanum”.

Hizo ndizo gharama! Na sio rahisi zina ugumu wake ndio maana Bwana hapo juu kasema TUJITAHIDI! Maana yake tufanye bidii kwa hali na mali tupite mlangoni. Tukitia Nia yeye katuahidi kutusaidia katika (Mathayo 19:26).

Je ni mali zako ndio zinazokukosesha na kukuzuia wewe kumtafuta Mungu? Ziweke pembeni kwa muda. Mtafute Kwanza Mungu na hizo zitakutafuata zenyewe baadaye. Je ni ndugu ndio wanaokuzuia kumgeukia Mungu na kufanya mapenzi yake?. Ikumbuke njia ile ni Nyembamba haiwezekani kupita makundi. Bwana Yesu alisema “apendaye Baba au mama kuliko mimi hanifai (Mathayo 10:37)”. Waambie ndugu zako kwa upendo, sasa umeokoka umeamua kumfuata Yesu kwa gharama zote.

Chochote kile kinachotuzuia kuingia katika ufalme wa Mbinguni sasa tunapaswa tujiepushe nacho, ili tukidhi vigezo vya kuingia katika huo mlango ulio mwembamba. Na hatupaswi kukawia kwasababu pale juu amesema. Utafika wakati mlango huo mwembamba utafungwa..Na watu watatamani kuingia watashindwa. Maisha ya ukristo ni Maisha ya mapambano, lakini Bwana akiwa upande wetu hakuna linaloshindikana. Tutashinda na Zaidi ya kushinda. Tukimfanya yeye kuwa tegemeo letu.

Bwana akubariki sana.

Tafadhali share na wengine.


Mada Nyinginezo:

Naomba kujua watakaoenda mbinguni je! ni wengi au wachache?

NAFASI YA MWANAMKE KATIKA KANISA

Je! Kuna dhambi kubwa na ndogo, na kama hakuna je! Mtu aliyeua na aliyetukana je watapata adhabu sawa?

Biblia inamaana gani kusema;aliyezaliwa na Mungu hatendi dhambi?

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/11/19/ingieni-kwa-kupitia-mlango-ulio-mwembamba/