SAUTI NI SAUTI YA YAKOBO, LAKINI MIKONO NI YA ESAU.

by Admin | 30 November 2019 08:46 am11

Sauti ni sauti ya Yakobo, lakini mikono ni ya Esau maana yake ni nini?

Shalom! Kama vile Zaburi 68:19 inavyosema… “Na ahimidiwe Bwana, ambaye Siku kwa siku hutuchukulia mzigo wetu;”

..Hivyo kila inapoitwa leo hatuachi kumshukuru Mungu kwa msaada wake anaotupa maishani.

Esau.

Tukisoma kitabu cha Mwanzo, tunaona maisha ya Isaka na wanawe wawili (Esau na Yakobo) jinsi yalivyokuwa,.. wengi wetu tunaifamu habari Esau kuwa alikuwa ni mtu aliyependwa sana na baba yake, na Yakobo alipendwa na mama yake, ..Isaka alimpenda Esau kwasababu alikuwa anamjali sana, ni mtu ambaye alikuwa radhi kupoteza muda wake mwingi ili tu kuhakikisha kuwa baba yake yupo katika hali nzuri, na nafsi yake inafurahi,.. alikuwa anamjali baba yake kiasi kwamba hakuruhusu hata mtu yeyote wa kawaida tu awe anamlisha baba yake, bali yeye mwenyewe alikuwa anatoka na kwenda kumtafutia mnyama mzuri,.. kisha anakuja kumwandaa mwenyewe, na kumtengea baba yake mezani, huo upendo sio wa kawaida..

Hivyo baba yake akampenda sana kwasababu alikuwa anatoa kilicho bora kwa ajili yake,..Esau hakuwa mtu wa kuingia tu zizini na kuchukua mbuzi au kondoo, na kuandaa kwa ajili ya baba yake..Kwake hicho aliona kama sio kitendo cha heshima, badala yake alijiota na kuingia porini mwenyewe kwenda kumtafutia baba yake chakula chenye ladha tofuati na vile ambavyo vinaliwa sikuzote nyumbani..Hata kama ingekuwa wewe ni mzazi ungeachaje kumpenda mtoto kama huyo….hakununulii tu suti zinazotoka labda Kariakoo, bali anafunga safari yeye mwenyewe kwenda kukutafutia suti nzuri nje ya nchi labda Ujerumani au Canada, ili tu nafsi yako ifurahi..

Hiyo ikamfanya baba yake amthamini sana Esau kuliko Yakobo, na ilipokaribia sasa wakati wa kufa kwake, akamwita Esau kisirisiri ili ambariki..hakumwambia hata Yakobo siri hiyo, lakini alimwita akamwambia amwandalie mawindo mazuri kama ilivyo desturi yake ya siku zote na mwisho aje kumbariki.. Esau akaondoka haraka pasipo kujua kuwa mama yake yupo karibu sana na Isaka kuliko yeye anavyodhani.. Ndipo mama yake akafanya haraka haraka kwenda kumweleza Yakobo mambo yote, na akampa siri ya kumfanya auchukue ule mbaraka wa Esau ..

Lakini Yakobo akamwambia mama yake, maneno haya:

Mwanzo 27:11 “Yakobo akamwambia Rebeka mamaye, Esau ndugu yangu ni mtu mwenye malaika, na mimi ni mtu laini.

12 Labda baba yangu atanipapasa, nami nitakuwa machoni pake kama mdanganyifu; nami nitaleta juu yangu laana wala si mbaraka.

13 Mamaye akamwambia, Laana yako na iwe juu yangu, mwanangu, usikie sauti yangu tu, enenda ukaniletee wana-mbuzi”.

 

Ukiendelea kusoma utaona, Rebeka alimwandalia Yakobo, mambo mawili makuu, moja ni vazi la mnyama, ili kuvaa shingoni na mikononi mwake, na pili ni vazi la Esau lenye harufu ya mawindo ili Isaka akimkaribia asikie harufu nzuri aliyozoea kumsikia nayo Esau kila alipokuwa akimletea mawindo mezani..

Mwanzo 27:21 “Isaka akamwambia Yakobo, Karibu, tafadhali, ili nikupapase, mwanangu, nione kwamba wewe ndiwe mwanangu Esau, ama siyo.

22 Basi Yakobo akamkaribia Isaka, babaye, naye akampapasa, akasema, Sauti ni sauti ya Yakobo, lakini mikono ni mikono ya Esau”.

JE! KUNA JAMBO LOLOTE TUNAWEZA KUJIFUNZA HAPO KATIKA AGANO JIPYA?

Pamoja na mengi yasiyofaa juu ya Esau ambayo tusingepaswa kuyaiga lakini pia upo ufunuo mwingine wa kipekee juu ya maisha ya Esau na Yakobo. Kama vile yasivyokuwa mengi ya kujifunza juu ya maisha ya yona (kwa tabia yake ya kutokutii), lakini pia kutokutii kwake kulibeba ufunuo wa Yesu kukaa kaburini siku tatu.(Soma Luka 11:30-31). Kadhalika na Esau ni hivyo hivyo, maisha yake yamebeba ufunuo juu ya Yesu.

Kumbuka Yakobo kama Yakobo ambaye tunamwona leo hii anayeitwa Israeli asingekuwa vile, wala asingekuwa na Baraka zile kama Sio Esau aliyemwandalia..Hivyo Esau ni mfano kamili wa Bwana wetu YESU KRISTO…Sisi tunaoitwa wakristo, tusingekuwa hivi tulivyo leo hii kama kusingekuwa na mtu ambaye tumemwibia Baraka zake..Na huyo si mwingine zaidi ya Bwana wetu YESU KRISTO…Yeye ndiye aliyempendeza Baba yetu (Mungu) kuliko mwanadamu yoyote hapa duniani, mpaka siku moja sauti ikasikika kutoka mbinguni ikisema huyu ni mwanangu mpendwa wangu niliyependezwa naye…Yeye ndiye mwana peke yake alistahili kupokea Baraka zote peke yake ndiye aliyestahili kubarikiwa na Mungu…Amefanyika kuwa laana kwa ajili yetu sisi, ili sisi tuzishiriki Baraka zake,..kama asingejitwika fedheha zetu, na dhambi zetu sisi leo hii sijui tungekuwa wapi..

LAKINI VIPO VIGEZO VYA SISI KUBARIKIWA.

Kumbuka halikuwa jambo la Yakobo kwenda tu kichwa kichwa kunyakuwa Baraka zile, kulikuwa na taratibu za kufuata. Kwanza ilimbidi avae mavazi ya Esau pili avae ngozi ya mnyama inayofanana na Esau vinginevyo angekumbana na laana ya baba yake badala ya baraka…Hata leo hii wapo watu wanamwendea Mungu bila kufuata kanuni Mungu aliyoiweka..na mwisho wa siku wanaangukia laana badala ya Baraka..Yaani kwa ufupi kama wewe upo nje ya Kristo, ni heri uendelee katika hali yako ya dhambi kuliko kumkaribia Mungu na kumfanyia ibada ukidhani kuwa ndio utampendeza….

Mungu hakuwahi kupendezwa na mwanadamu yoyote ni Yesu Kristo tu peke yake..Na hivyo ili na wewe uonekane unampendeza yeye ni sharti uvae vazi la YESU KRISTO..Kama sio Yesu Kristo sisi ni kama mbolea tu, hatustahili hata kulitaja jina la Mungu.

Tulishapotea siku nyingi kwenye dira za kiungu.

Hilo tu ndilo litakalo tufanya sisi tubarikiwe na Mungu..Na tunaweza kufanya hivyo kwa kutubu dhambi zetu zote kwa kudhamiria kuziacha kabisa kisha kwenda kubatizwa katika ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi (Yohana 3:23) na kwa jina la YESU KRISTO (Matendo 2:38), na baada ya hapo Roho Mtakatifu kuja juu yetu…Tukikamiliza hatua zote hizo tutakuwa na uhakika wote kuwa dhambi zetu zimeondolewa na sisi nasi tutazishiriki Baraka zile zile za Bwana wetu Yesu Kristo.

UTUKUFU UNA KRISTO YESU, BWANA WETU..MKUU WA WAFALME WA DUNIA (Ufunuo 1:5), Aliyetuosha dhambi zetu kwa Damu yake. Ubarikiwe sana.WHATSAPP

Mada Nyinginezo:

YONA: Mlango 1

TUMAINI NI NINI?

UWE MWAMINIFU HATA KUFA.

BUSTANI YA NEEMA.

MAPIGO YA VITASA SABA, NA SIKU YA BWANA.

DOWNLOAD PDF

WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/11/30/sauti-ni-sauti-ya-yakobo-lakini-mikono-ni-ya-esau/