MSIJISUMBUE KWA NENO LOLOTE.

by Admin | 4 December 2019 08:46 am12

“Msijisumbue kwa neno lolote;….(Wafilipi 4:6)

Vita nyingine kubwa ambayo inapiganwa katika akili ya mkristo, ni vita ya hofu ya maisha,.. kwamba kesho yangu itakuwaje, nitakula nini, nitavaa nini, nitakuwa wapi miaka 5 mbeleni,.. nikiendelea katika hali hii hii uzee wangu utakuwaje, kodi ya nyumba mwezi ujao ikiisha nitapata wapi nyingine, watoto wangu wakiugua kwa ghafla fedha ya matibabu makubwa nitaitolea wapi? n.k.n.k… hayo ni mawazo ambayo yanapenya katikati ya mawazo yetu, wakati mwingine aidha tunataka au hatutaki,, na madhara yake ni kuwa jambo hii likishakita mizizi ndani yetu, sasa Neno KUSUMBUKIA ndipo linapozaliwa..

Tunaanza Kujisumbua kwa mawazo mengi usiku na mchana, kwa nguvu nyingi, kwa gharama zozote ili tu ufikie malengo hayo..Sasa sio vibaya kufikiria mambo yajayo na kuyawekea mipango..lakini kupo kufikira kuliko sahihi na kupo kufikiria kusiko sahihi… Kufikiri kusiko sahihi kunaleta HOFU!!

Bwana alilifahamu hilo, na anajua kabisa kwa jinsi tulivyo hapa duniani tumezungukwa na mambo mengi ya kidunia, hofu ya maisha ni lazima ituvamie,…. lakini yeye alitupa suluhisho sahihi la sisi kuweza kuishinda hali hiyo akasema..

Wafilipi 4:6 “Msijisumbue kwa neno lolote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu”.

Unaona, anasema, msijisumbue kwa Neno lolote, sio moja, au mawili, au matatu, bali lolote.., anajua yapo mengi hayawezi kuisha, makubwa kwa madogo,hivyo lolote lile tusijisumbue nalo, yatatufanya tutoke katika mstari wa wokovu na fikra zetu za kutazama mambo ya mbinguni,.. bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu,”…

Hizo ni nguzo muhimu sana..

Tunapokutana na changamoto za ki-maisha, au shida Fulani, tusianze kupaniki kwa haraka na kuanza kuzichosha fahamu zetu,… kuwaza sana hadi kukosa usingizi, hapana bali tunapaswa tuchukue haja zetu hizo katika maombi, tumpelekee yeye haja zetu hizo, kwasababu anasema pia..

1Petro 5:6 “Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake;

7 huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu”.

Unaona Mungu anajishughulisha sana na mambo yetu, pale tunapojinyenyekeza mbele zako na kumtwika yeye kila shida yetu.. ukitaka kufahamu hilo kama Mungu anajishughulisha kweli na mambo yetu, angalia huo moyo wako unaodunda miaka na miaka hatujawahi kuununulia betri ili uendelee kudunda kila saa,.. wala hujawahi kuuhudumia au kuufanyia service yoyote ili ufanye kazi vizuri, lakini fahamu yeye ndiye Mungu anayeudundisha kila wakati..hata chakula tunachokila tumboni baada ya hapo hatushughulikii mmengenyo wake..mwili ndio unaofanya hiyo kazi wenyewe…wewe huhusiki hata kidogo…Sasa ikiwa hatujajisumbukia kwa hilo kwanini kuumiza vichwa kwa hayo yaliyosalia..?

Jaribu kutafakari tena  vizuri:

Angalia, kucha zako, zinavyokuwa, na nywele zako ambazo kila siku unazikata.., haijawahi kutokea hata sikumoja ukawa na hofu kwamba ahaa, pengine hizi nywele zinaweza zisiote tena, embu ngoja nikazitafutie mbolea nzuri za kuziwekea ili ziote vilevile kwa rangi ile ile,.. sasa ikiwa hayo hatuwezi kuyasumbukia ambayo yanayo umuhimu mkubwa zaidi kuliko kazi zetu, na nyumba zetu, na nguo zetu kwanini tuiruhusu hofu?…Huwezi kumtumikia Mungu ukiwa na hofu, huwezi kusonga mbele ukiwa na hofu, kazi ya Mungu huwezi kuifaya ukiwa na stress..Ukishaona unahofu kali kuhusu kesho fahamu kuwa Mungu hayupo hapo..kwasababu Roho wa Mungu kamwe hamletei Mtu hofu bali Amani na kabla ya kuanza kuzungumza na wewe na kukupa ufunuo fulani,..ataanza kushughulika kwanza na hofu iliyopo ndani yako..hiyo ikishaondoka ndipo azungumze na wewe..

Hivyo tukiwa waombaji, kudumu katika sala itatusaidia kuuvuta uwepo wa Mungu karibu zaidi na sisi Mungu muweza wa yote asiyeshindwa na lolote,.. Mungu aliyeumba milima, na bahari, nyangumi wa kubwa, na mabara, Mungu aliyeumba dhahabu zote na almasi zote za ulimwengu mzima,… aliyeumba matajiri na maskini, aliyeumbwa wafalme na viongozi wote, huyo ndiye anayekuambia Usijisumbue kwa Neno lolote, bali nitwike mimi fadhaa zako,niachie mimi wewe endelea kuwaza mambo ya ufalme wa mbinguni..

JE! TUKIJIFUNZA KUWA WATU WANA NAMNA HIYO, FAIDA YAKE NI IPI?

Ukiendelea sasa kusoma mstari ule ule mbele kidogo utaona unasema hivi..

Wafilipi 4:6 “Msijisumbue kwa neno lolote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu.

7 Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu”.

Umeona hapo chini? Anasema “NA AMANI YA MUNGU, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu”… Ukishamtwika yeye fadhaa zako zote, na shida zako zote, ukaondoa ufahamu wako wote katika matatizo yanayokuzunguka… ukijua kabisa yeye mwenyewe atayashughulikia..Basi ile AMANI yake itashuka juu yako wakati huo huo…hiyo ni amani ipitayo fahamu zote, amani ya ki-Mungu si ya kibinadamu, ambayo hiyo huwa ikishushwa juu ya mwanadamu, anakuwa mtu mwingine kabisa,

Watu wanaweza kumshangaa inakuwaje mtu huyu yupo katika hali hii au hali ile, amefiwa na ndugu zake wote, hana hiki au hana kile, kodi inakaribia kuisha.. lakini anayofuraha na amani kuliko hata sisi wenye kila kitu, yeye ndiye anayekuja kutufariji sisi? ..Hawajui kuwa hiyo ndiyo Amani ipitayo fahamu zote…Sio kwamba matatizo hayapo! Yapo lakini…Amani ya Kristo imeyafunika na hivyo huna hofu.

Zaburi 127:2b……. Yeye humpa mpenzi wake usingizi’.

Amani hiyo ikimwingia mtu vizuri, hofu yote inaondoka, anaishi kama ndege ambaye anaamka asubuhi akimwimbia Mungu nyimbo za furaha, na kabla ya kwenda kulala anamwimbia Mungu nyimbo za furaha, hajali kesho yake itakuwaje, kwamba kitakuwepo au hakitakuwepo..Lakini hata siku moja Mungu hutasikia kuwa Mungu amemnyima rizki..

Lakini amani hiyo ni ngumu kuifikia kwa namna ya kawaida kama hatutakuwa watu wa kuomba, na watu wa kushukuru, pamoja na kujijengea utaratibu wa kulitafakari Neno lake kwa wakati mwingi kwa kadri tuwezavyo mpaka. Ipo Mifano mingi ya kujifunza ndani ya Neno la Mungu..Tusiposoma Neno hatutaijua na hivyo kupungukiwa nguvu za rohoni.

Bwana akubariki. Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mada Nyinginezo:

FAIDA ZA MAOMBI.

MAJARIBU MATATU YA YESU KRISTO

KISIMA CHA MAJI YA UZIMA NI KILE KILE CHA ZAMANI.

SIKU ILE NA SAA ILE.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/12/04/msijisumbue-kwa-neno-lolote/