SIKU ILE NA SAA ILE.

SIKU ILE NA SAA ILE.

Bwana Yesu alisema sehemu fulani maneno haya ” walakini siku ile na saa ile”..akiwa na maana kuwa Kuna siku inayokuja huko mbeleni, yenye Tarehe yake na mwezi wake, na mwaka wake. Siku hiyo itaitwa tarehe Fulani ya Mwezi Fulani na mwaka Fulani.

Siku hiyo upande mmoja wa dunia utakuwa ni mchana na mwingine usiku, siku hiyo watu watakuwa wanapika, wengine wanafanya biashara, wengine wanajenga, wengine wapo katikati ya harusi, wengine watakuwa safarini, wengine watakuwa misibani, wengine mashuleni, Wengine watakuwa wamelala, wengine wapo kanisani, wengine watakuwa mahospitalini, wengine mahakamani, wengine wanacheza mpira, wengine wapo disko. Wengine bungeni, wengine magerezani,wengine wanapanga mipango na mikakati ya namna ya kuimarisha vipato vyao na kazi zao n.k…Siku hiyo ndio itakuwa mwisho wa utendaji kazi wa Roho Mtakatifu duniani kwa watu wa mataifa…siku hiyo utapita kitu kinachoitwa UNYAKUO.

Wakati watu wengi watakuwa hawaelewi chochote, kufumba na kufumbua baadhi ya watu watatoweka, wachache sana…Tetesi tetesi chache zitasikika huko na huko kwamba kuna baadhi ya watu wamepotea katika mazingira ya kutatanisha, lakini kutokana na kwamba dunia imelewa na kulemewa na mambo mengi, wengi watasema ni habari za kuzusha, kwani imezoeleka kusikika unyakuo umepita na unakuta hakuna lolote lililotokea. Watasema mwaka 2000 ilikuwa hivyo hivyo, walitabiri na hakuna kilichotokea…mwaka 2002 ikawa hivyo hivyo, wakasema unyao umepita na hakuna lolote, kadhalika mwaka 2012…Na leo tena uzushi mpya umezuka.

Wakati mamia na maelfu ya watu wanapuuzia habari hizo na kuona ni habari za uzushi, upande wa pili kutakuwa na uchungu na vilio kwa wale waliowashuhudia wenzao wakinyakuliwa mbele ya macho yao, wale waliokuwa wanalima pamoja ghafla jirani anatoweka mbele yake, wale ambao walikuwa wamelala na wenzao katika chumba kimoja ambacho kilifungwa na makomeo kwa ndani, na walipoamka kwa ghafla wakakuta hawapo, huku milango bado imefungwa vile vile kwa ndani, wale ambao walikuwa wapo ibadani pamoja kanisani na ghafla wenzao wamepotea, wale ambao wamemwona mtu Fulani kaketi mahali Fulani na kufumba na kufumbua katoweka. Hao ndio watakaoelewa uchungu wa kuachwa. Watalia sana na kuomboleza lakini haitasaidia.

Siku hiyo utakapoona mwanao hayupo, dada yako aliyekuwa ameokoka hayupo, mchungaji wako hayupo, na wewe umeachwa! Itakuwa ni uchungu kiasi gani?. Ukitazama ni masaa machache tu nyuma umetoka kupokea rushwa, ukitazama ni masaa machache tu nyuma umesikia mahubiri ya kukuonya na ulimwengu ukakataa. Ukitazama ni wiki chache tu nyuma uliota ndoto inayokuonya kwamba hizi ni siku za mwisho ukapuuzia. Masaa machache tu ulisikia mahali panazungumziwa habari za unyakuo.

Ukitazama ni siku chache tu nyuma ndio ulianza kupoa, utajisikiaje? Ukitafakari sasa wenzako wanafutwa machozi mbinguni na wewe umebaki ukingojea dhiki kuu na chapa ya mnyama na ziwa la moto milele?, ukitafakari ni disko ndio iliyokuponza, mke au mume unayeishi naye ndio aliyekuponza, binti/kijana unayetembea naye ndiye aliyekuponza, utafutaji mali uliopindukia ndio iliyokuponza, miziki ya kidunia, na tamaa ndivyo vilivyokuponza kuikosa mbingu, utakuwa katika huzuni kubwa kiasi gani.

Ndugu hiyo siku inafika, labda ni leo, au kesho au kesho kutwa hakuna aijuaye! Lakini ipo karibuni sana biblia inasema hivyo…

Bwana Yesu alisema..

Mathayo 24:36 “Walakini habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba peke yake.

37 Kwa maana kama vile ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu.

38 Kwa kuwa kama vile siku zile zilizokuwa kabla ya Gharika watu walivyokuwa wakila, na kunywa, wakioa na kuolewa, hata siku ile aliyoingia Nuhu katika safina,

39 wasitambue, hata Gharika ikaja, ikawachukua wote, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu.

40 Wakati ule watu wawili watakuwako kondeni; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa;

41 wanawake wawili watakuwa wakisaga; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa.

42 Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu

43 Lakini fahamuni neno hili; kama mwenye nyumba angaliijua ile zamu mwivi atakayokuja, angalikesha, wala asingaliiacha nyumba yake kuvunjwa.

44 Kwa sababu hiyo ninyi nanyi jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana wa Adamu yuaja.”

Kukesha kunakozungumziwa hapo na Bwana Yesu, sio kujizuia kulala usingizi wa mwilini wakati wa usiku hapana!…Bali maana yake kujizuia kulala usingizi wa rohoni…kwasababu duniani sasahivi ni giza! Ni Giza Nene kutokana na matendo ya giza yanayotendeka, Na sikuzote tabia ya giza ni kusababisha usingizi, siku zote usiku ndio watu wanalala! Sio mchana wakati wa Nuru, Kwahiyo giza lililopo duniani leo linasababisha usingizi mkali wa kiroho, na hivyo tunapaswa tuushinde huo usingizi na kukesha! Kwasababu Bwana atakapokuja hatawachukua watu waliolala bali walio macho!

Waefeso 5:14 “Hivyo husema, Amka, wewe usinziaye, Ufufuke katika wafu, Na Kristo atakuangaza.

15 Basi angalieni sana jinsi mnavyoenenda; si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima;

16 mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu”.

Bado unaendelea na uasherati? Unaendelea na utoaji mimba? Unaendelea na uvaaji mbaya na ibada za sanamu? Tubu na kumgeukia mwokozi, kabla siku ile na saa ile haijafika. Kwasababu Bwana hapendi kumwona mtu yeyote aangamie, bali ni atubu, vilevile anataka watu wote waingie katika karamu ya mwana wake aliyowaandalia siku ile..Sasa Kwanini uikose?, tubu angali muda unao, na Bwana atakupokea na kukukaribisha katika ufalme wake.

Bwana akubariki!

Mada Nyinginezo:

TUUTAZAME PIA MWISHO WA UJENZI WETU.

SADAKA YA MALIMBUKO.

HATARI YA KUHUBIRI INJILI TOFAUTI NA ILIYOANDIKWA KWENYE BIBLIA.

JISHUSHE ILI MUNGU AKUHUDUMIE.

ROHO HUTUOMBEA KWA KUUGUA KUSIKOWEZA KUTAMKWA!

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
2 Comments
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
anna peter
anna peter
3 years ago

God bless you nimelia San kuyaon maandik hay inatakiw ifike wakat tuon mamb ya dunia hii ni ubatili mtupu.