NINI TOFAUTI KATI YA KARAMA, UTENDAJI KAZI NA HUDUMA.

by Admin | 8 February 2020 08:46 pm02

Nini tofauti kati ya karama ya rohoni, utendaji kazi na huduma?. Vitu hivi vitatu ni ni ni hasa?

Shalom.Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe…Karibu tuongeze maarifa katika kujifunza Neno la Mungu..

Leo kwa Neema za Bwana tutajifunza  kidogo juu ya karama za Rohoni…Zinaitwa karama za rohoni kwasababu sio za mwilini..zipo karama za mwilini na za rohoni pia…Kila mwanadamu kaumbiwa na karama fulani ya mwilini…iwe anaijua au haijui..Na vile vile kila mtu anayo karama ya rohoni…

Karama ya rohoni lengo lake kuu ni kutumika kwaajili ya faida ya ufalme wa Mbinguni…Lakini mtu akiwa nje ya Kristo karama ile inakuwa inatumika na ajili ya ufalme wa giza aidha awe anajua au hajui. Sasa leo hatutaingia huko sana…bali tutajifunza maana ya KARAMA, HUDUMA na UTENDAJI KAZI.

Kama Umempa Yesu Kristo Maisha yako…na hujajua karama yako ni ipi..nakushauri ukatafute kujua maarifa hayo kwa bidii zote kwasababu ni muhimu sana kuyajua. Na kama hujui sehemu ya kuyapata tunalo somo juu ya hilo..kama ukilihitaji unaweza ukatutumia ujumbe ufupi inbox tukutumie.

Lakini leo hii tutaangazia tofauti kati ya KARAMA, HUDUMA na UTENDAJI KAZI.

Biblia inasema katika…

1Wakorintho 12:1 “Basi, ndugu zangu, kwa habari ya karama za roho, sitaki mkose kufahamu.

2  Mwajua ya kuwa mlipokuwa watu wa Mataifa, mlichukuliwa kufuata sanamu zisizonena, kama mlivyoongozwa.

3  Kwa hiyo nawaarifu, ya kwamba hakuna mtu anenaye katika Roho wa Mungu, kusema, Yesu amelaaniwa; wala hawezi mtu kusema, Yesu ni Bwana, isipokuwa katika Roho Mtakatifu.

4  Basi pana tofauti za KARAMA; bali Roho ni yeye yule.

5  Tena pana tofauti za HUDUMA, na Bwana ni yeye yule.

6  Kisha pana tofauti za KUTENDA KAZI, bali Mungu ni yeye yule azitendaye kazi zote katika wote.

7  Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana”

Kama tunavyoona hapo pana vitu vitatu…Karama, huduma…na utendaji kazi…Wengi imewawia ngumu kutofautisha vitu hivi..lakini leo kwa Neema za Bwana tutajifunza tofauti zake tukijifunza kupitia mifano ya kimaisha.

Mungu anapompa mtu karama… anaweza kumpa karama moja, au wakati mwingine mbili au tatu kwa mpigo…Lakini wengi Bwana anawapa karama moja tu ya rohoni… Na karama moja inaweza kuwa na utendaji kazi tofauti…Karama moja inaweza kuwa na utendaji kazi hata mara 100 tofauti tofauti..

Tuchukue mfano…Hospitalini kunaweza kuwa na madaktari 100, lakini wote hawatendi kazi inayofanana…wengine utakuta wamebobea katika mifupa, wengine vinywa, wengine Ngozi, wengine macho n.k Lakini wote hawa karama yao ni moja “udaktari/utabibu”…Na huduma yao wote ni moja “UAGUZI” wanaagua watu.  Hivyo tunaweza kurahisisha na kusema katika hospitali hiyo kuna watu 100 wenye karama moja na huduma moja lakini utendaji kazi tofauti.

Vivyo hivyo tukirudi kwenye SHULE.. shule inaweza kuwa na waalimu 50, kati ya hao kuna waalimu wa fizikia, kiingereza, biolojia n.k lakini wote hao karama yao ni moja “kufundisha” na huduma yao ni moja nayo ni UALIMU. Na vitengo vingine vyote vya kimaaisha ni hivyo hivyo…kwa wahandisi ni hivyo hivyo, kwa wanajeshi ni hivyo hivyo, utendaji kazi unatofautia n.k.

Tukirudi katika kanisa la Kristo ambalo ndio kitengo kikuu na cha juu na Taasisi iliyo kuu kuliko zote mbele za Mungu..Nalo pia lina watu wenye karama tofauti tofauti, huduma tofauti tofauti na utendaji kazi tofauti.

Kwamfano..Katika karama ya uimbaji wanaweza kuwepo waimbaji 100, kila mmoja akawa na namna yake ya kuimba, wengine wamejaliwa kuimba vyema katika nyimbo za kuabudu, wengine katika nyimbo za sifa, wengine katika nyimbo za tenzi za rohoni n.k hawa wote wanatenda kazi tofauti tofauti lakini karama yao ni moja “kuimba”, na huduma yao ni moja UINJILISTI kwa njia ya NYIMBO.

Hali kadhalika kwenye huduma ya kiualimu,watakuwepo waalimu wa Watoto kanisani, watakuwepo waalimu wa vijana kanisani, watakuwepo waalimu wa kila namna kulingana na Neema kila mtu aliyopewa, wengine waalimu kwa njia ya vitabu, wengine waalimu kwa njia ya mitandao, nk. mwalimu mmoja hawezi kufanana na mwingine kwa kila kitu…sasa hawa wote karama yao ni moja “kufundisha” lakini huduma yao ni moja tu “WAALIMU”..Haijalishi watakuwa wamejigawanya gawanya katika vitengo vingapi..lakini huduma yao ni hiyo hiyo moja tu.

Warumi 12:6  “Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbalimbali, kwa kadiri ya neema mliyopewa; ikiwa unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya imani;

7  ikiwa huduma, tuwemo katika huduma yetu; mwenye kufundisha, katika kufundisha kwake;

8  mwenye kuonya, katika kuonya kwake; mwenye kukirimu, kwa moyo mweupe; mwenye kusimamia kwa bidii mwenye kurehemu, kwa furaha”.

Hali kadhalika wapo katika kanisa ambao wamepewa karama ya ndoto kama Danieli, wengine maono, wengine unabii, n.k hawa huduma yao ni “UNABII”.

Na karama nyingine zote zilizosalia, kama miujiza, Imani, Neno la Hekima, unabii n.k.. zina utendaji kazi tofauti na huduma tofauti tofauti.

Hivyo kwa hitimisho ni kwamba…kila karama inayo huduma..Na karama moja inaweza kuwa na utendaji kazi tofauti tofauti kulingana na mtu. Hivyo usitafute kujilinganisha na mtu mwingine, wala usitafute kufanana na mwingine..wala usimdharau mwingine..

Kama wewe unaweza kuona maono ya nini kitatokea kesho..mwingine anaweza kupewa kuliona jambo hilo hilo kwa njia ya ndoto, mwingine si kwa ndoto wala maono bali kwa ufunuo…Hivyo usijisifu kwa kuona maono wala kwa ndoto, wala kwa ufunuo..wote karama yenu ni moja “unabii”  lakini zinatenda kazi tofauti tofauti..

Wewe una karama ya Matendo ya miujiza, ukimwekea mtu mkono anapokea uponyaji..usijisifu kwa mwingine, kwasababu mwingine anaweza kumtamkia tu mtu na akapokea uponyaji, ule ule ambao wewe ungeufanya kwa kumwekea mikono..Mna karama moja isipokuwa utendaji kazi tofauti.nk. nk NK

Hivyo ni muhimu kuwa wanyenyekevu na pia kukaa kila mtu katika nafasi yake pasipo kunia mkuu..

Warumi 12:3  “Kwa maana kwa neema niliyopewa namwambia kila mtu aliyeko kwenu asinie makuu kupita ilivyompasa kunia; bali awe na nia ya kiasi, kama Mungu alivyomgawia kila mtu kiasi cha imani.

4  Kwa kuwa kama vile katika mwili mmoja tuna viungo vingi, wala viungo vyote havitendi kazi moja;

5  Vivyo hivyo na sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika Kristo, na viungo, kila mmoja kwa mwenzake”

SASA JAMBO KUU LA MWISHO LA KUKUMBUKA ni  kuwa  karama yoyote au huduma yoyote uliyopewa..lengo la kupewa karama hiyo ni kuujenga mwili wa Kristo, sio kujionyesha wewe ni mtaalamu..au mjuzi, au una uwezo Fulani wa kipekee Zaidi ya wengine.. Mtu mmoja aliniuliza mtumishi nifanye nini ili niwe  na upako, wa kufufua wafu, na kuwekea watu mikono wapone saa hiyo hiyo, nifanye miujiza mikubwa, nikamuuliza unataka hayo yote kwa lengo gani,..hana jibu..Ndugu karama za rohoni sio za kujitafutia umaarufu au kuwa nazo tu basi..

Hizo Mungu kaziweka ili kuokoa Roho za watu wake.. hivyo unapaswa uitumie katika kuwaleta watu katika ufalme, watubu wamgeukie Mungu na kuucha ulimwengu kama wewe ulivyouacha Hilo ndio lengo kuu…Usipoitumia inavyopaswa siku ile utatoa hesabu..Ikiitimia kujipatia pesa utatoa hesabu, ukiitumia kulaania watu utatoa hesabu, ukiitumia kupotosha watu utatoa hesabu, ukiitumia kujitengenezea umaarufu wako na watu badala ya kumwogopa Mungu na kumtumikia Mungu wanakuogopa wewe siku ile utatoa hesabu..ukiitumia karama uliyopewa kujichukulia utukufu wewe badala ya kumpa Mungu utukufu..siku ile utatoa hesabu ndugu yangu…Siku ile utapoangaliwa na kuonekana karama uliyopewa hajaleta watu wowote katika ufalme wa mbinguni, utawajibishwa katika hilo..

Leo tumejua tofauti kati ya karama, utendaji kazi na Huduma, Bwana azidi kutusaidia sana..tuwe waaminifu hata siku ile ya kuja kwake.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

NITAIFAHAMU VIPI KARAMA YANGU?.

ROHO YA MPINGA KRISTO IKITENDA KAZI SIKU HIZI ZA MWISHO

TOA SADAKA ISIYO NA KASORO KWA BWANA.

KWANINI MUNGU ALIMTUMIA MUSA KWA VIWANGO VILE?

FIMBO YA HARUNI!

KARAMA ILIYO KUU.

ITAMBUE KARAMA YA MUNGU.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/02/08/nini-tofauti-kati-ya-karama-utendaji-kazi-na-huduma/