USIHUZUNIKE.

by Admin | 13 April 2020 08:46 am04

Katika maisha kila mwanadamu ambaye ameumbwa na Mungu mkuu, ni lazima ameumbiwa kitu kinachoitwa huzuni ndani yake. Maana yake ni kwamba ni lazima atapitia vipindi vya huzuni na vile vile atapitia vipindi vya furaha. Kila mwanadamu hata kama ni mtumishi wa Mungu ni lazima atapitia hivyo vipindi..Bwana wetu Yesu Kristo ambaye alikuwa ni mkamilifu asilimia zote alivipitia si zaidi sisi tusiokuwa wakamilifu?..Ni lazima tuvipitie. Na huzuni ni kama ugonjwa ukiwekwa katika mazingira Fulani inazidi na pia ikiwekwa katika mazingira Fulani unapungua.

Na huzuni inaweza kuja aidha kutokana na kupata taarifa mbaya, au umepatwa na jambo baya..au unakwenda kupatwa na jambo baya…au wakati mwingine inakuja pale linapotokea jambo ambalo hukulitegemea au hukulipanga, au hukutamani liwe hivyo lilivyo.

Mtu anapofikia hali kama hiyo anajikuta anazama katika dimbwi kubwa la mawazo, na kukosa hamu ya kufanya jambo lolote lile..hata hamu ya kula inatoweka, wakati mwingine hata hamu ya kuishi.

Siku ile ambayo Bwana ndio alikuwa anakwenda kusulibiwa, Huzuni kubwa iliwaingia wanafunzi wake, baada ya kuwaambia kwamba muda si mrefu atakwenda kusulibiwa, na ataondoka atakwenda zake kwa Baba..

Yohana 16:5 “Lakini sasa mimi naenda zangu kwake yeye aliyenipeleka, wala hakuna mmoja wenu aniulizaye, Unakwendapi?

6 Ila kwa sababu nimewaambia HAYO HUZUNI IMEJAA MIOYONI MWENU.

7 Lakini mimi nawaambia iliyo kweli; yawafaa ninyi mimi niondoke, kwa maana mimi nisipoondoka, huyo Msaidizi hatakuja kwenu; bali mimi nikienda zangu, nitampeleka kwenu”.

Na zaidi ya yote walipoambiwa kwamba mmoja wao atamsaliti..Ndio kabisa moto wote ukakata ndani yao..Wakati wanadhani kwamba Kristo atazidi kuendelea kuwepo, yeye anawapa taarifa za msiba, kwamba anakwenda kusulibiwa..wakawa wanawaza kwanini hayo yote yampate Bwana wao, sasa maisha yatakuwaje baada ya yeye kuondoka.

Na hata Bwana alipowachukua usiku ule kwenda kusali naye hata nguvu zilikuwa zimewaisha kabisa, hawakusali sana wakalala kwasababu ya huzuni nyingi..Tusome..

Luka 22:45 “Alipoondoka katika kuomba kwake, akawajia wanafunzi wake, AKAWAKUTA WAMELALA USINGIZI KWA HUZUNI.

46 Akawaambia, Mbona mmelala usingizi? Ondokeni, mkaombe, msije mkaingia majaribuni”.

Lakini katika hali kama hiyo, Bwana aliuona udhaifu wa mioyo yao kwamba wamechoka na wanahuzuni nyingi. Lakini aliwaambia waamke waombe..kwasababu roho i radhi lakini mwili ni dhaifu…Hivyo wanapaswa waishinde hali hiyo ya huzuni..kwasababu wana huzuni, lakini siku chache baadaye watakuwa na furaha. Hivyo alijaribu kuwaasa kwamba wajaribu kuishinda huzuni ambayo ilipelekea udhaifu wa mwili wasimame waombe kwasababu majaribu hayo ni ya siku chache tu..siku mbili baadaye watakuwa na furaha isiyo na kifani. Kwasababu aliwaambia bado kitambo kifupi hawamwoni (yaani atakufa na kuzikwa)..na tena bado kitambo kidogo watamwona tena (yaani siku atakapofufuka)..wataendelea kumwona mpaka Pentekoste na watakuwa na furaha kuu.(Soma Yohana 20:20).

Katika wakati huu unaoitwa wa pasaka miongoni mwa mambo mengi tunayojifunza basi ni muhimu kulijua hili pia…USIHUZUNIKE..Pengine umepitia shida Fulani, au umepata usumbufu Fulani, au huzuni Fulani, au tabu Fulani, au taarifa Fulani, au jambo lolote lile ambalo limekuletea huzuni kubwa moyoni hata umekata tamaa ya kila kitu na ya kuendelea mbele katika imani…Huo sio wakati wa kuzidi kuipalilia huzuni kwa kukata tamaa na kuiacha Imani, sio wakati wa kulala usingizi kwa huzuni..Bali ni wakati wa kusimama na KUOMBA kwa nguvu…ni wakati wa kuzidi kuendelea mbele kwasababu huzuni hiyo ni ya kitambo tu!. Baada ya siku chache itaondoka na furaha itakurudia kama mwanzo na utajuta kwanini siku chache nyuma ulikuwa unahuzunika…utajuta kwanini ule muda ambao ulikuwa na huzuni usingeutumia hata kuomba au kumsifu Mungu.

Hivyo simama sasa mtu wa Mungu, huu sio wakati wa kupalilia huzuni bali ni wakati wa kuomba..Mitume wa Yesu huzuni yao iligeuka furaha pale walipomwona Bwana kafufuka…nawe pale utakapoona kile kilichokuwa kimekufa kimefufuka, siku sio nyingi furaha yako itarudi. Hivyo usihuzunike..simama uombe, simama uendelee mbele kwasababu hatua zilizobakia mbele yako ni chache kuliko ulizoziacha nyuma. Hivyo sio wakati wa kunyongonyea ni wakati wa kuomba.

Bwana akubariki

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

MTINI, WENYE MAJANI.

Je kupiga miayo ni ishara ya mapepo?

USIKIMBILIE TARSHISHI.

USHAURI KWA MWANAMKE WA KIKRISTO.

JE SALA YA ROZARI TAKATIFU NI YA KIMAANDIKO?

JINSI EDENI ILIVYOKUWA.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/04/13/usihuzunike/