MASHAHIDI 40 WALIOUAWA MJINI SEBASTE, NI UJUMBE KWETU.

by Admin | 20 May 2020 08:46 pm05

Ilikuwa ni mwaka wa 320, wakati wa utawala wa mfalme Licinius wa Rumi, Kumbuka zamani hizo Rumi ndiyo iliyokuwa inatawala karibu dunia nzima wakati  huo na ndio iliyokuwa kichwa cha mbele kuwatesa na kuwaua wakristo ulimwenguni kote, Sasa huyu alikuwa ni mpagani, ambaye hakutaka kusikia Imani yoyote ya Kikristo.

Lakini upande wa pili kulikuwa na askari wa kirumi katika mji mmoja ulioitwa Sebaste (Kwasasa ni maeneo ya Uturuki) ambao  jumla yao 40, waliotoka katika nchi mbalimbali walimwamini Kristo, na kuikiri Imani bila uwoga wowote,.Sasa alipopata habari alitoa amri kali ya kuzuia mtu yeyote kuabudu miungu mingine tofauti na yake, hivyo mfalme alichokifanya ni kutoa agizo, kwa mtu yeyote atakayeonekana anafanya hivyo atateswa vikali na kuuawa.

Lakini hawa askari, historia inatuambia wote hawa mashahidi 40 walikataa kusalimu amri, hivyo wakachukuliwa na kupelekwa kando kando ya ziwa la maji ya baridi (wakati huo ulikuwa ni msimu wa kipindi cha baridi kali huko Asia), ili wapigwe na baridi mpaka kuganda na kufa.

Na wakati huo huo Mfalme alitoa amri  pembeni pawekwe bwawa la maji ya moto,  na chakula kizuri, kwa yeyote atayesalimu amri atolewe na kuingizwa kwenye hilo bwana la moto apate moto, kisha alishwe vizuri.

Lakini katikati ya mateso hayo makali ambayo yaliwafanya wakae siku tatu usiku na mchana, mmoja wa wale 40 kweli alisalimu amri na kutoka kwenye maji yale ya baridi, hivyo wakabakia 39, lakini mmoja tena kati ya wale askari waliokuwa wanawasimamia  akachomwa moyo sana, na usiku mmoja alipokuwa amelala kando kando ya moto kwenye barafu aliota ndoto, malaika ameshuka mbinguni, pale kwenye ziwa kisha akawavika wale askari mataji, anasema, aliyahesabu yalikuwa 39..

Alipoamka asubuhi akakata shauri, akavua silaha zake, akamkiri  Kristo na saa hiyo hiyo akavua nguo zake za ki-askari, akaingia majini kuungana na wale 39 ili  kutimiza idadi ya watu 40..

Na ilipofika siku ya nne asubuhi, wengi wao walikuwa wamekufa, lakini wale waliosalia hoi, waliuliwa, na miili yao ikachomwa moto, kisha, majivu yao yakaenda kutupwa kwenye mto.

Hivyo ndivyo walivyoishindania Imani mpaka kufa mashujaa hawa..

Biblia inatuambia..

Mathayo 16:25  “Kwa kuwa mtu atakaye kuiokoa nafsi yake, ataipoteza; na mtu atakayepoteza nafsi yake kwa ajili yangu, ataiona”.

Sisi tunaweza tusifikie huko kwenye kuchagua kifo au uzima kwa ajili ya Kristo, lakini kama tutashindwa kuchagua jambo jepesi la “kufa kwa Habari ya ulimwengu” kwa ajili ya Kristo , tusitazamie kamwe tutauona  ufalme wa mbinguni.. sehemu nyingi biblia imetuonya kwa kutumia neno hili “MSIDANGANYIKE”..Ikiwa na maana, tunaweza kudanganyika, tukadhani kuwa kwa kuendelea kuwa  walezi, siku moja tunaweza kuingia  mbinguni, kwa kuendelea kuzini mara moja moja, kwa kutoa mimba, kwa kusagana, kwa kuvaa  vimini na nguo za kikahaba, kwa kula rushwa, kwa kutazama picha za ngono mitandaoni, bado tukawa na nafasi ya kuingia mbinguni siku ya mwisho.

1Wakorintho 6:9  “Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti,

10  wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi”.

Biblia inatuambia tusidanganyike, njia ile imesonga sana, na wanaoyoiona ni wachache.  Kama hatutakubali kufa kwa Habari ya ulimwengu mpaka tukaonekana sisi si kama wao, tusahau kuiona mbingu..

Kama kuacha kuvaa vimini, kuvaa suruali(wanawake), kunyoa viduku na kusuka rasta(wanaume),kuacha kampani za watu waovu, kuacha kusikiliza nyimbo za kidunia, kuacha kwenda disko, kuacha kula rushwa, kuacha kutazama picha za ngono, ni Ngumu basi, ni uzima wa milele ni wa watu wengine si wako! ….ni sawa na huyo askari mmoja aliyejaribu kuingia kwenye hayo maji ya baridi lakini uzalendo ukamshinda na kutoka kurudi kwenye mambo ya kidunia.

Ikiwa Mambo ya kujikana nafsi tu, yatatushinda, utawezaje kuutoa uhai wako kwa ajili ya Kristo, siku ile Je! tutawezaje kufananishwa  na hili wingu kubwa la mashahidi wa Imani ambao walikuwa tayari kuyatoa Maisha yao (tena kwa kifo cha mateso) kwa ajili ya Kristo? (Waebrania 12:1)

Utasema mimi mazingira yanayonizunguka yananifanya nishindwe kuwa mkristo..Wenzako walikuwa ni wanajeshi wanatumika katika kazi ngumu za kidunia kushinda wewe lakini walikuwa tayari kumtanguliza Kristo kwanza.

Huu ni wakati wa kuvuta soksi zetu juu, na kuanza kuyatengeneza Maisha upya, nyakati hizi za mwisho si nyakati tena za kuvutwa vutwa tena katika wokovu, zama hizo zilishakwisha, kwasababu injili kila mahali anasikika sasa, huu ndio ule wakati Bwana Yesu alisema..

Mwenye kudhulumu na azidi kudhulumu; na mwenye uchafu na azidi kuwa mchafu; na mwenye haki na azidi kufanya haki; na mtakatifu na azidi kutakaswa (Ufunuo 22:11).

Hivyo kama wewe ni mtakatifu, pambana binafsi kuzidi kujitakasa, zidi kuogopa kuwa hapo katikati (vuguvugu), kwasababu biblia inasema walio hapo watatapikwa (Ufunuo 3:16 ). Hivyo ikiwa unajitahidi kufanya hivyo, kumbuka Bwana anakutia moyo na kukwambia, “Safari aliyoianzisha yeye moyoni mwako ataitimiza mpaka siku ile ya mwisho”.

Umeamua kuukataa ulimwengu, zidi kupiga hatua nyingine katika UTAKATIFU, haijalishi utaonekana umepotea kiasi gani, haijalishi utaonekana ni mjinga, endelea mbeleni.. lakini mwisho wako utakapofika utajikuta umetokea kwenye mji wa furaha…

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

CHUKUA MZIGO WA MWINGINE.

Chapa zake Yesu ni zipi hizo?

KUMBUKUMBU LA DHAMBI.

OLE WAO WANAOJITAHIDI KUMFICHA BWANA MASHAURI YAO.

KABLA YA MAANGAMIZI, KRISTO HUWA ANAONYESHA KWANZA NJIA YA KUTOROKEA.

USIMWOGOPE YEZEBELI.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/05/20/mashahidi-40-waliouawa-mjini-sebaste-ni-ujumbe-kwetu/