NYAKATI HIZI NI ZA MWISHO, HII DUNIA INAKWENDA KUISHA.

by Admin | 3 June 2020 08:46 pm06

Isaya 24:19 “Dunia kuvunjika, inavunjika sana; dunia kupasuka, imepasuka sana; dunia kutikisika, imetikisika sana.

20 Dunia inalewa-lewa kama mlevi, nayo inawaya-waya kama machela; na mzigo wa dhambi zake utailemea; nayo itaanguka, wala haitainuka tena”.

Shalom,

Hii dunia yetu imefananishwa na mlevi wa kupindukia.. Mlevi ni mtu ambaye ameshapoteza uwezo wake wa kuji-control, yaani akili yake na mwili wake havina uhuwiano tena, akisimama anajiona kama kaning’inizwa, na akianza tu kutembea anajiona kama anazungushwa kama tairi, hivyo mwendo wake unaishia kuwa ni kuyumba yumba tu safari nzima na mwisho wake unakuwa ni kuangukia mtaroni wakati huo akiwa hata tayari ameshajisaidia..

Na kibaya Zaidi akishaanguka pale, ndio haamki tena  mpaka asubuhi..

Na hii dunia yetu ndio imekuwa hivyo, tumeinywesha pombe na maovu, na hivyo imelewa haiwezi kuji-control tena.. Leo hii utaona matetemeko makubwa na madogo  ya ardhi kila mahali, utajiuliza ni kwanini hayo mambo yamekithiri sana wakati huu.. Ujue ni dhambi zetu zimeilewesha dunia na moja ya hizi siku itakwenda kuanguka.

Utaona, magonjwa makubwa ya mlipuko duniani kote (kama corona)..Utajiuliza tena ni kwanini?.. Ni kwasababu haiwezi kujidhibiti yenyewe, inawaya waya.

Utajiuliza ni kwanini vitendo viovu na mauaji ya kinyama yanaendelea duniani kote kila kukicha.. Ni kwasababu imeshalewa vya kutosha na hivyo itakwenda kupumzika tu muda sio mwingi.

Utajiuliza tena ni kwanini mafundisho mengi ya mashetani , na manabii wengi wa uongo wamezuka duniani kuliko vipindi vingine vyote vya nyuma..Jibu ni lile lile, haiwezi kustahimili tena, mzigo wa dhambi umekuwa mzito sana hivyo wakati wake wa kwenda kujipumzisha umekaribia sana.

Kwanini vitisho vya vita, vinavuma kila mahali, mabomu ya Atomic yanatengenezwa na mataifa kila pembe ya dunia..Utajiuliza ya nini yote hayo wakati kwa kizazi chetu, mbona tunaishi katika dunia inayosimamia masuala ya haki za kibinadamu.? Ni uthibitisho kwamba silaha hizo ni lazima zije kutumika tu wakati si mrefu.

Tumekuwa tukisikia habari za mwisho wa dunia, tunapuuzia, tunadhani, ni mambo ambayo yanahitaji maandalizi mengi sana, au yataanza taratibu taratibu, lakini biblia haituambii hivyo, inasema siku ambazo watu wanadhani kuna amani na salama ndipo uharibifu utakavyokuja kwa ghafla..

1Wathesalonike 5:1  “Lakini, ndugu, kwa habari ya nyakati na majira, hamna haja niwaandikie.

2 Maana ninyi wenyewe mnajua yakini ya kuwa siku ya Bwana yaja kama vile mwivi ajavyo usiku.

3 Wakati wasemapo, Kuna amani na salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa”.

Unaona? Wakati wasemapo amani na salama..Lakini mtume  Paulo anaendelea kwasisitiza watakatifu wote na kusema…

4  Bali ninyi, ndugu, hammo gizani, hata siku ile iwapate kama mwivi.

 5  Kwa kuwa ninyi nyote mmekuwa wana wa nuru, na wana wa mchana; sisi si wa usiku, wala wa giza.

 6  Basi tusilale usingizi kama wengine, bali tukeshe, na kuwa na kiasi.

7  Maana walalao usingizi hulala usiku, pia na walewao hulewa usiku.

 8  Lakini sisi tulio wa mchana, tuwe na kiasi, hali tukijivika kifuani imani na upendo, na chapeo yetu iwe tumaini la wokovu”.

Je! Wewe bado upo usingizini?.. Bado upo gizani?..Je unatamani kuishuhudia hiyo siku ya kuanguka kwa dunia moja kwa moja jinsi itakavyokuwa?..Wakati huo ambao wenzako watakuwa wameshanyakuliwa wewe utakuwepo hapa chini kuyashuhudia yote..Na siku yenyewe biblia inasema itakuwa ya namna hii:

2Petro 3:10  “Lakini siku ya Bwana itakuja kama mwivi; katika siku hiyo mbingu zitatoweka kwa mshindo mkuu, na viumbe vya asili vitaunguzwa, na kufumuliwa, na nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea.

11  Basi, kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa,

12  mkitazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuihimiza; ambayo katika hiyo mbingu zitafumuliwa zikiungua, na viumbe vya asili vitateketea na kuyeyuka?

Kama tunavyosoma hiyo siku ya moto na Volkano duniani, sio ya kuitamani kabisa..Mimi siitamani, natumai na wewe pia..Hivyo Mgeukie Kristo sasa, kwa kutubu dhambi zako na kwa kumaanisha kumfuata Bwana, kama bado hujampokea.

Bwana akubariki sana.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

NEHUSHTANI (NYOKA WA SHABA).

JIEPUSHE NA MASHINDANO YA DINI.

UTAWALA WA MIAKA 1000.

JE! WATOTO WACHANGA WANAWEZA KUHUKUMIWA NA KUTUPWA MOTONI.

JE! KUNA UMUHIMU WOWOTE WA KULIPA ZAKA?

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/06/03/nyakati-hizi-ni-za-mwisho-hii-dunia-inakwenda-kuisha/