Nyama zilizosongolewa ni zipi?Je kunywa damu ni dhambi?

by Admin | 5 September 2020 08:46 am09

 Naomba kufahamu Nyama zilizosongolewa ni zipi?Je kunywa damu ni dhambi kwa Mkristo?


Nyama zilizosongolewa ni nyama za wanyama ambao hawajachinjwa, na damu yao kumwagika chini.

Kipindi kabla hata ya agano la kwanza(Kale) , Mungu tayari alikuwa ameshampa Nuhu maagizo kuwa asile nyama ya mnyama yoyote pamoja na damu yake ndani yake.

Mwanzo 9:4 “Bali nyama pamoja na uhai, yaani, damu yake, msile”.

Tunaona miaka mingi baadaye Mungu anakuja kumwambia tena Musa jangwani maneno hayo hayo:

Kumbukumbu 12:23 “Ila ujihadhari kwamba usile damu, kwani ile damu ndiyo uhai; na uhai usile pamoja na nyama. 24 Usiile; imwage juu ya nchi kama maji”.

 

Walawi 17:10 “Kisha mtu awaye yote wa nyumba ya Israeli, au miongoni mwa hao wageni wakaao kati yao, atakayekula damu, ya aina yo yote, nitakunja uso wangu juu ya mtu huyo alaye damu, nami nitamkatilia mbali na watu wake.

11 Kwa kuwa uhai wa mwili u katika hiyo damu; nami nimewapa ninyi hiyo damu juu ya madhabahu, ili kufanya upatanisho kwa ajili ya nafsi zenu; kwani ni hiyo damu ifanyayo upatanisho kwa sababu ya nafsi.

12 Kwa hiyo naliwaambia wana wa Israeli, Hapana mtu miongoni mwenu aliye na ruhusa kula damu, wala mgeni aketiye kati yenu asile damu”.

Lakini tukirudi tena katika agano letu jipya, tunaona moja ya maagizo ambayo mitume wanalipa kanisa la mataifa(yaani sisi) Ni kutokula nyama zilizongolewa( yaani nyama ambazo hazijachinjwa na damu kumwagika)..

Matendo 15:19 “Kwa sababu hiyo mimi naamua hivi; Tusiwataabishe wale waliomgeukia Mungu katika Mataifa;

20 bali tuwaandikie kwamba wajiepushe na unajisi wa sanamu, na uasherati, na nyama zilizosongolewa, na damu.

21 Kwa maana tangu zamani za kale Musa anao watu wahubirio mambo yake; katika kila mji husomwa kila sabato katika masinagogi”.

Sasa swali linakuja Je kwa mantiki hiyo  wakristo haturuhusiwi  kabisa kula nyama zilizongolewa au kunywa damu?

Ukweli ni kwamba kulingana na mazingira ya wakati ule  kwa watu wa mataifa, na ya sasa, ni ngumu kuishi bila kukutana na nyama za namna hiyo.. Kwasababu nyama nyingi siku hizi, hazichinjiwi nyumbani, unazikuta mabuchani, au supermarket, na kule hujui zimechinjwaje chinjwaje.. Hivyo huwezi kuuliza hii nyama iliandiliwaje, vinginevyo hutakaa ule nyama kabisa…Sasa Bwana Yesu kwa kulijua hilo akawaagiza mitume wake, kuwa watakachokutana nacho mbele yao kila mahali mnapokaribishwa  wale (Luka 10:8),

Mtume Paulo naye aliliweka wazi hilo kwa wakorintho  na kuwaambia..

1Wakorintho 10:25 “Kila kitu kiuzwacho sokoni kuleni, bila kuuliza-uliza, kwa ajili ya dhamiri;

26 maana, Dunia ni mali ya Bwana na vyote viijazavyo”.

Kwamfano Soseji nyingine zinatengenezwa na damu ndani yake, na  nyingine hazitengenezwi na damu, Hivyo ukipewa kula bila kuuliza uliza, ukikuta zinauzwa dukani nunua ule bila kuuliza uliza.

Kwasababu sisi agano letu halipo katika vyakula, bali lipo rohoni..vyakula havitubadilishi kitu. Lakini pale inapotokea unachinja mbuzi wako, au kuku wako, au ng’ombe wako nyumbani ni vema ukaimwaga damu ya mnyama huyo chini, usinywe kisusio..Si vema kufanya hivyo, kwasababu tumeshapewa maagizo hayo.

Zaidi ya yote amani ya Kristo iamue ndani yako.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

DAMU YA YESU INANENAJE MEMA KULIKO YA HABILI?

MUNGU AKIKUPITA LEO, HAIMAANISHI KUWA HAJAKUCHAGUA.

USITAFUTE FAIDA YAKO MWENYEWE BALI YA WENGINE.

MAJONZI YA MTUME PAULO KWA NDUGU ZAKE.

HUDUMA YA WALE MASHAHIDI WAWILI.

UNYAKUO.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/09/05/nyama-zilizosongolewa-ni-zipije-kunywa-damu-ni-dhambi/