Sharoni ni nini au ni wapi kibiblia?(1Nyakati 5:16)

by Admin | 27 November 2020 08:46 am11

Maana ya Neno Sharoni ni “uwanda” au “nchi tambarare”. Katika biblia, tunaona lipo eneo (wilaya) lililojulikana sana na waisraeli kama Sharoni, japokuwa biblia haijatolea maelezo yake mengi, Lakini ni eneo lililokuwa na rubuta nyingi, na lilikuwa lipo karibu na fukwe za ile bahari kubwa(yaani bahari ya Mediterenia), tazama ramani.

Utalisoma Neno hilo kwenye vifungu hivi vya biblia;

1Nyakati 5:16 “Nao wakakaa huko Gileadi, katika Bashani, na katika miji yake, na katika viunga vyote vya Sharoni, hata kufika mipakani mwake”.

1Nyakati 27:29 “na juu ya makundi ya ng’ombe waliolishwa katika Sharoni alikuwa Shitrai, Msharoni; na juu ya makundi waliokuwamo mabondeni alikuwa Shafati mwana wa Adlai”;

Isaya 33:9 “Nchi inaomboleza, na kulegea; Lebanoni imetahayarika na kunyauka; Sharoni imekuwa kama jangwa; Bashani na Karmeli zimepukutika majani”.

Isaya 65:10 “Na Sharoni itakuwa zizi la makundi ya kondoo, na bonde la Akori mahali pa kulala makundi ya ng’ombe, kwa ajili ya watu wangu walionitafuta”.

Na katika agano jipya utalisoma katika kifungu hichi;

Matendo 9:35 “Na watu wote waliokaa Lida na Sharoni wakamwona, wakamgeukia Bwana”.

UA LA UWANDANI

Lakini tukisoma kitabu cha wimbo ulio bora, tunaona, lipo Ua moja linatajwa kama Ua la Uwandani, au kwa jina lingine Ua la Sharoni (Rose of Sharon). Mwandishi wa kitabu hichi, anajifananisha yeye na Ua hilo ambalo limechipuka katika nchi hiyo ya Sharoni.

Wimbo 2:1 “Mimi ni ua la uwandani, Ni nyinyoro ya mabondeni.

2 Kama nyinyoro kati ya miiba, Kadhalika mpenzi wangu kati ya binti”.

Na bila shaka Ua hili ni Kristo, yeye ndiye aliyechipuka katika bonde la ulimwengu, na uzuri wake, na mwonekano wake ulikuwa ni tofauti na mwanadamu yoyote ulimwenguni. Yeye ndiye aliye Nuru ya ulimwengu, yeye ndiye aliyeiondoa harufu mbaya ya huu ulimwengu wa dhambi, hata tukapata kibali cha kumkaribia Mungu, yeye ndiye mwokozi wa ulimwengu.

Je! Na wewe umeliona Ua hilo?, Je umempata mwokozi moyoni mwako? Kumbuka hakuna njia nyingine yoyote utakayoweza kumfikia Mungu isipokuwa kwa njia yake yeye. Hakuna mwanadamu yoyote anayeweza kumpendeza Mungu kwa nguvu zake mwenyewe isipokuwa Yesu Kristo peke yake. Ukimkosa Kristo maishani mwako, haijalishi umepata ulimwengu mzima, hesabu kuwa umepoteza kila kitu. Lakini ukimpokea yeye, hata ukikosa vyote hesabu kuwa umevipata vyote.

Uamuzi ni wako,  kumbuka hizi ni siku za mwisho, Lakini ikiwa leo utapenda kuyakabidhi maisha yako kwake, Huo utakuwa ni uamuzi wa busara sana, Basi fungua hapa kwa ajili ya maelekezo ya Toba>>>  SALA YA TOBA

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

Uwanda wa dura ni nini?

Konde la Soani ni nini? (Zaburi 78:12,43)

Bisi ni nini? (Walawi 23:14, Ruthu 2:14)

Jaa ni nini katika biblia?

IKO NJIA IONEKANAYO KUWA SAWA MACHONI PA MTU.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/11/27/sharoni-ni-nini-au-ni-wapi-kibiblia1nyakati-516/