Nini maana ya kumlingana Mungu?

by Admin | 4 December 2020 08:46 pm12

Kumlingana Mungu ni Kiswahili cha zamani chenye maana ya  “kumwita Mungu”.  Pale mtu anapopitia jaribu, au tatizo, anapomwita au kumlilia Mungu wake kwaajili ya kupata msaada, maana yake mtu huyo “amemlingana” Mungu.

Tunaweza kuona mifano michache katika biblia ya watu waliomlingana Mungu.

Wana wa Israeli:

Hawa walimwacha Bwana, na Bwana akawatia chini ya utumwa mkali kwa maadui zao.

Waamuzi 3: 8 “Kwa hiyo hasira za Bwana ziliwaka juu ya Israeli, naye akawauza na kuwatia mikononi mwa Kushanrishathaimu mfalme wa Mesopotamia; na wana wa Israeli wakamtumikia huyo Kushan-rishathaimu muda wa miaka minane.

9 Kisha wana wa Israeli walipomlingana Bwana, Bwana akawainulia wana wa Israeli mwokozi, aliyewaokoa, yaani, Othnieli mwana wa Kenazi, ndugu mdogo wa Kalebu”.

Yabesi:

1 Nyakati 4: 10 “Huyo Yabesi akamlingana Mungu wa Israeli, akisema, Lau kwamba ungenibarikia kweli kweli, na kunizidishia hozi yangu, na mkono wako ungekuwa pamoja nami, nawe ungenilinda na uovu, ili usiwe kwa huzuni yangu! Naye Mungu akamjalia hayo aliyoyaomba”.

Kwa Habari ndefu kuhusu huyu Yabesi na maisha yake unaweza kufungua hapa >> MAISHA YA YABESI.

Pia Neno hilo limetumika katika mistari mingine michache ifuatayo..1Nyakati 5:20, na 1Nyakati 21:26.

Jambo tunalojifunza ni kwamba hata sisi tunapoadhibiwa na Mungu, kutokana na makosa yetu tunapomgeukia Bwana na kumlilia (kumlingana), yeye ni mwenye rehema na huruma, anaghairi mabaya.

Na kama tupo kwenye dhambi, yaani hatumkabidhi Yesu Maisha yetu, basi ghadhabu ya Mungu ipo juu yetu, na kila tunapoisikia injili inayohubiriwa na watumishi wa Mungu, na kuidharau, Mabaya yanatuandama…

Yeremia 26:2 “Bwana asema hivi, Simama katika uwanja wa nyumba ya Bwana, useme na miji yote ya Yuda, wajao ili kuabudu katika nyumba ya Bwana; sema nao maneno yote ninayokuamuru kuwaambia, usizuie hata neno moja.

3 Labda watasikia, na kughairi na kuacha kila mtu njia yake mbaya; ili niyaghairi mabaya niliyokusudia kuwatenda, kwa sababu ya uovu wa matendo yao”.

Bwana yupo tayari kughairi mabaya aliyokuwa ameyapanga kuyaleta juu yako kwasababu ya uzinzi wako, au kwasababa ya utoaji wako mimba, au ulevi wako, au yoyote yale mabaya unayoyafanya. Endapo ukiamua kutubu na kumgeukia yeye.

Kama upo tayari leo kutubu na kumwita yeye (kumlingana), kama alighairi mabaya kwa wana wa Israeli, na kwa watu wengine wengi, ikiwemo mimi hatashindwa na wewe basi kama upo tayari leo kuanza maisha mapya fungua hapa kwa msaada Zaidi >> SALA YA TOBA.

Na kama tayari umeshaokoka, basi usiache  kumwita (kumlingana) Mungu wako kila wakati, kwasababu yeye anajishughulisha sana na mambo yako.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

WAENDEE WANA WA ISAKARI, UWE SALAMA.

WAPE WATU WANGU RUHUSA ILI WAPATE KUNITUMIKIA.

Je! Wana wenu huwatoa kwa nani? maana yake ni nini?

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/12/04/nini-maana-ya-kumlingana-mungu/