Tofauti kati ya Hekima, ufahamu na maarifa, ni ipi?

by Admin | 15 March 2021 08:46 pm03

SWALI: a) Naomba kujua tofauti Kati ya Hekima , Ufahamu na Maarifa kwenye biblia

b) jinsi gani vitu hivyo vinavyohusiana?

Mithali 2:6 “Kwa kuwa BWANA huwapa watu hekima; Kinywani mwake hutoka maarifa na ufahamu”;

2 Mambo ya Nyakati 1:10 “Basi sasa nipe hekima na maarifa, nijue kutoka na kuingia mbele ya watu hawa; kwa kuwa ni nani awezaye kuwahukumu watu wako hawa walio wengi”?


JIBU:

i) MAARIFA:

Maarifa ni uwezo wa kujua mambo mengi, na hiyo inakuja kwa kusoma sana, au kujifunza Neno la Mungu kwa bidii, au kusikiliza, au kupitia mazingira Fulani ambayo yatakupa uzoefu husika.

Mungu anatutaka sana watu wake tuwe na maarifa ya kutosha kuhusu yeye ili tusiangamie. Kwani biblia inasema,

Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maarifa; (Hosea 4 :6)

Na ndio maana moja ya zile ngazi 7 zinazozumngumziwa katika kitabu cha 2Petro ambazo kila mkristo anapaswa azipitie, ni maarifa.

2Petro 1:5 “Naam, na kwa sababu iyo hiyo mkijitahidi sana kwa upande wenu, katika imani yenu tieni na wema, na katika wema wenu maarifa”

Tukikosa maarifa hata kama sisi tutasema ni wakristo tutashindwa kuwa na ujasiri na Mungu kwasababu hatujui tabia zake, tutashindwa hata kumwamini Mungu ipasavyo kwasababu hatuujui uweza wake, vilevile tutaishi maisha ya uvuguvugu kwasababu tu,hatuna maarifa ya kutosha ya kujua nyakati na majira tunayoishi. Hivyo maarifa ni nyenzo muhimu sana kwa mkristo yeyote.

Na hayo yanakuja kwanza kwa kuonyesha bidii kusoma Neno lake ‘kwa kujifunza’ na sio kama gazeti. Pia kwa kuonyesha kiu ya kutafuta kuijua kweli yake kwa kusikiliza mafundisho sahihi yatakayokusaidia kumjua yeye kupitia watumishi wake.

ii) HEKIMA:

Hekima. Ni uwezo wa kupambanua, kuhukumu, na kufanya maamuzi sahihi. Sulemani alimwomba Mungu hekima na Mungu akampa, na ndio maana utaona mwanzoni kabisa,mwa hekima yake kujidhihirisha ilikuwa ni siku ile wale wanawake wawili walipomfuata, awamue kwa habari ya watoto wao, sasa kwa tukio lile kama asingekuwa na hekima ya ki-Mungu ndani yake asingeweza kupambanua lolote..(Soma 1Wafalme 3:16-18 )

Utaona tena wakati ule yule malkia wa Sheba alipokuja kumjaribu kwa mafumbo yake ya ndani, aliweza kuyafichua yote, kwa usahihi, mpaka yule malkia akashangaa sana (1Wafalme 10)

Vivyo hivyo katika siku hizi za mwisho, Mungu anasema walio na hekima, ndio watakaoelewa siri za Mungu na mafumbo ya yule mnyama(mpinga-Kristo) na kazi zake, inahitaji hekima ya Mungu ya kutosha iwepo ndani yetu ili tuelewe, vinginevyo, zipo habari katika haya maandiko kamwe hatutakaa tuzielewe, hususani zile zinazozuhusu nyakati za mwisho. Soma

Danieli 12:10 “Wengi watajitakasa, na kujifanya weupe, na kusafika; bali wabaya watatenda mabaya; wala hataelewa mtu mbaya awaye yote; BALI WAO WALIO NA HEKIMA NDIO WATAKAOELEWA.

Ufunuo 3:17 “tena kwamba mtu awaye yote asiweze kununua wala kuuza, isipokuwa ana chapa ile, yaani, jina la mnyama yule, au hesabu ya jina lake.

18 HAPA NDIPO PENYE HEKIMA. Yeye aliye na akili, na aihesabu hesabu ya mnyama huyo; maana ni hesabu ya kibinadamu. Na hesabu yake ni mia sita, sitini na sita”.

iii) UFAHAMU:

Ufahamu ni uelewa. Ukikosa uelewa huwezi kutafuta maarifa, wala kuomba hekima. Wanyama hawana ufahamu, na ndio maana hawajui kumtafuta Mungu, halikadhalika, wanadamu pia tumepishana viwango vya ufahamu, na ndio maana wengine hawamtafuti Mungu kwasababu wamekosa ufahamu wa kujua umuhimu wa Mungu maishani mwao ni upi.

Kwa mfano mtu anayepata ufahamu wa kujua madhara ya zinaa, kamwe hawezi kwenda kuzini ovyo, kwasababu anajua mwisho wake utakuwa ni ukimwi, au mimba zisizotarajiwa. Au kijana anayepata ufahamu wa kujua elimu ina umuhimu gani kwake ,kamwe hawezi kuchezea shule.

Vivyo hivyo kibiblia mtu anayeikimbia dhambi huyo amepata ufahamu.

Ayubu 28:27 “Ndipo alipoiona na kuitangaza; Aliithibitisha, naam, na kuichunguza.

28 Kisha akamwambia mwanadamu, Tazama, kumcha Bwana ndiyo hekima, NA KUJITENGA NA UOVU NDIO UFAHAMU”.

b) Hivyo vyote hivi vitatu ni nguzo kwa mtu yeyote kuwa navyo katika maisha yake, Ufahamu, maarifa na Hekima. Na vyote hivi Mungu anataka kuviona ndani yetu.

Hivyo tumche Bwana, pia tuonyeshe kumpenda na kumtafuta ndipo atakapotugawia.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Jiunge na kundi letu la mafundisho ya Biblia whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp

Mada Nyinginezo:

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/03/15/tofauti-kati-ya-hekima-ufahamu-na-maarifa-ni-ipi/