VAZI KUU AMBALO MUNGU AMETUANDALIA KILA MMOJA WETU.

by Admin | 18 March 2021 08:46 pm03

Ukisoma kitabu cha Mwanzo, utaona mara baada ya Adamu na Hawa kuasi, kwa kula yale matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya,ambayo Mungu aliwakataza wasiyale, utaona pale kwa tendo lile hawakuona kwanza dhambi ndani yao, bali waliliona tatizo kwenye miili yao. Hawakujiona wamemkosea Mungu, bali walijiona wapo uchi, na ndio maana muda ule ule wakaanza harakati zao za kutafuta namna ya kwenda kujisitiri na sio kwenda kutubu,

Wakaenda  kujishonea matawi ya mtini, ili wajirudishe katika hali yao ya mwanzo, wajaribu kuisitiri ile aibu iliyowaingia, sasa unaweza kudhani walikuwa ni wajinga, hapana hawakuwa wajinga, walijua kabisa, nyenzo iliyowafanya wao waweze kumkaribia Mungu na kuzungumza naye ilikuwa ipo katika miili yao. Ndio maana wakakimbilia kwanza kwenda kushona majani,wajisiriti na sio kutubu dhambi zao.

Lakini tunaona hata baada ya kufanya vile, bado haikusaidia waliendelea kujiona wapo uchi, kuonyesha kuwa aibu ile ilipenya mpaka ndani kabisa ya mioyo yao. waligundua hata wakijisitiri kwa nguo za namna gani, bado miili yao imeshaingiwa na aibu kubwa isiyoneneka.

Mwanzo 3:7 “Wakafumbuliwa macho wote wawili wakajijua kuwa wa uchi, wakashona majani ya mtini, wakajifanyia nguo.

8 Kisha wakasikia sauti ya Bwana Mungu, akitembea bustanini wakati wa jua kupunga; Adamu na mkewe wakajificha kati ya miti ya bustani, Bwana Mungu asiwaone.

9 Bwana Mungu akamwita Adamu, akamwambia, Uko wapi?

10 Akasema, Nalisikia sauti yako bustanini, nikaogopa kwa kuwa mimi ni uchi; nikajificha”.

Ni kama tu wakati wa Samsoni, yeye alijua kabisa asili ya nguvu zake ipo katika nywele zake, lakini siku alipokatwa nywele na Delila, muda ule ule alikuwa dhaifu hata wafilisti walipokuja hakuweza tena kushindana nao,. Ndivyo ilivyokuwa kwa Adamu na Hawa, ujasiri wao wa kuongea na Mungu ulikuwa upo katika miili yao. Lakini walipoasi maagizo ya Mungu, waliona kasoro kubwa sana, ambayo hata majani na ngozi ambazo Mungu alikuja kuwafanyia baadaye ziwasiriti bado hazikufanikiwa kuiondoa ile aibu ya miili yao.

Sasa, aibu hii ya miili ipo hadi sasa, na ndio maana kwa miili yetu hii hatuwezi kumwona Mungu, au kuzungumza na Mungu. Haiwezekani, tatizo sio Mungu, tatizo ni aibu iliyo kwenye miili yetu, haiwezi kustahili utakatifu wa Mungu, sikuzote tutaukimbia tu.

Na ndio maana baada ya Mungu kulijua hilo, akamtuma mwanawe Yesu Kristo duniani, ili afe, kisha afufuke, kisha aende mbinguni kutuandalia VAZI  lake mwenyewe ambalo Kila mmoja wetu atakapolivaa hilo, basi aibu hiyo ya mwili ife, na kuanzia hapo amwone Mungu, na azungumze naye Uso kwa Uso kwa ujasiri wote, katika utakatifu hata Zaidi ya kile alichokuwa anakifanya Adamu kwa Mungu pale Edeni.

Na vazi hilo ni MIILI MIPYA itakayoshuka kutoka mbinguni. Hapo ndipo utajua ni kwanini siku tukienda katika unyakuo, hatutaacha miili yetu hapa chini ardhini, bali tutafufuliwa nayo kwanza, kisha tutavikwa hii miili mipya kama vile VAZI,. Na saa hiyo hiyo  aibu ya mwili itaondoka..hatutajiona tena tupo uchi, tutapata ujasiri mkubwa sana wa kumwona Mungu wetu, na kuzungumza naye, na kumfurahia milele. Biblia inasema..

2Wakorintho 5:1 “Kwa maana twajua ya kuwa nyumba ya maskani yetu iliyo ya dunia hii ikiharibiwa, tunalo jengo litokalo kwa Mungu, nyumba isiyofanywa kwa mikono, iliyo ya milele mbinguni.

2 Maana katika nyumba hii twaugua, tukitamani sana kuvikwa kao letu litokalo mbinguni;

3 IKIWA TUKIISHA KUVIKWAHATU TAONEKANA TU UCHI.

4 Kwa sababu sisi tulio katika maskani hii twaugua, tukilemewa; si kwamba twataka kuvuliwa, bali kuvikwa, ili kitu kile kipatikanacho na mauti kimezwe na uzima”.

Unaona? Biblia inasema. Tukishavikwa hiyo miili mipya hatutaonekana tena tu Uchi.

Tutamani sana tuifikie hiyo siku, kwasababu itakuwa ni siku ya furaha isiyokuwa na kifani, miili yetu itafanana na ya malaika, haitakuwa na kuumwa, au kufa, au kusinzia, au kuchoka, au kushikwa na udhaifu wowote. Kwasababu itakuwa ni miili ya kimbinguni, vazi la utukufu.

Swali sasa lipo kwako, je wakati huo ukifika utakuwa wapi? Ikiwa leo usiku parapanda italia utakuwa wapi ndugu yangu, kwasababu dalili zote za mwisho wa dunia Bwana Yesu alizozizungumza katika maandiko zimeshatia karibia zote, tunachongoja sasahivi ni UNYAKUO muda wowote. Embu jiulize utakuwa katika majuto makubwa kiasi gani utakaposikia wenzako baadhi wameondoka, wapo mbinguni wakimfurahia Mungu, halafu  wewe umebaki hapa duniani, ukijiandaa na dhiki kuu ya mpinga-Kristo na mapigo ya Mungu.

Ndugu yangu, usisubiri, mhubiri Fulani siku moja aje kukubembeleza umgeukie Muumba wako, hizi ni nyakati za wewe mwenyewe kutafakari ulipotoka, ulipo na unapoelekea, na kufanya uamuzi sahihi, kwa hali inavyoendelea sasa hivi duniani, hakuna anayejua kama kesho atakuwa hai. Hivyo tukilijua hilo ni wakati wetu wa kumkaribisha Kristo mioyoni mwetu kwa kumaanisha kabisa.Ili atupe wokovu na uzima wa milele.

Maran Atha.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

Kutahayari ni nini katika biblia?(2Timotheo 2:15)

PINDO LA VAZI LAKE SASA LIMEREFUSHWA.

Nini maana ya Mungu amemfanya mwanadamu mnyofu?

MARINDA KATIKA BIBLIA NI KITU GANI?

KITABU CHA YUDA: SEHEMU YA 3

Nini maana ya Mungu amemfanya mwanadamu mnyofu?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/03/18/vazi-kuu-ambalo-mungu-ametuandalia-kila-mmoja-wetu/