Je Musa yupo anawashitaki watu..kulingana na Yohana 5:45?

by Admin | 3 May 2021 08:46 pm05

Tusome,

Yohana 5:45  “Msidhani kwamba mimi nitawashitaki kwa Baba; yuko anayewashitaki, ndiye Musa, mnayemtumaini ninyi.

46  Kwa maana kama mngalimwamini Musa, mngeniamini mimi; kwa sababu yeye aliandika habari zangu.

47  Lakini msipoyaamini maandiko yake, mtayaamini wapi maneno yangu?”

Mstari huo haumzungumzii Musa kama Musa, kwamba yupo mahali Fulani mbinguni, anawashitaki watu..hapana!! bali unazungumzia maneno ya Musa (yaani mahubiri yake). Hayo ndiyo yayowashitaki watu sasa, na yatakayowashitaki watu siku ya hukumu, ndio maana hapo katika mstari wa 47 unamalizia kwa kusema.. “Lakini msipoyaamini maandiko yake, mtayaamini wapi maneno yangu?”.

 Sasa Ni kwa namna gani maneno ya Musa yanawashitaki watu sasa?, tutakuja kuona mbele kidogo, lakini sasa tuangalie kwa ufupi ni jinsi gani yatawashitaki watu siku ya hukumu…

Bwana Yesu alisema mahali Fulani maneno haya..

Yohana 12:47  “Na mtu akiyasikia maneno yangu, asiyashike, mimi simhukumu; maana sikuja ili niuhukumu ulimwengu, ila niuokoe ulimwengu

48  Yeye anikataaye mimi, asiyeyakubali maneno yangu, ANAYE AMHUKUMUYE; NENO HILO NILILOLINENA NDILO LITAKALOMHUKUMU SIKU YA MWISHO.

49  Kwa sababu mimi sikunena kwa nafsi yangu tu; bali Baba aliyenipeleka, yeye mwenyewe ameniagiza nitakayonena na nitakayosema.”

Umeona? hapo Bwana Yesu anasema..”Neno analolihubiri ndilo litakalohumu siku ya mwisho”.

Hivyo hata Musa naye, hasimami kumhukumu mtu, bali injili yake ndiyo itakayohukumu watu siku ya mwisho..Kama Musa alitabiri kwamba “Atakuja Masihi”, na Masihi alipokuja kweli kulingana na huo unabii, watu wakamkataa Masihi huyo, basi siku ile ya hukumu, Unabii ule alioutoa kwa uwezo wa Roho utawahukumu wale watu, waliomkataa Masihi. Kwasababu Musa alisema kitu alichoonyeshwa na Mungu, na wala si kwa nafsi yake.

Na si maneno ya Musa tu peke yake, bali na ya Mitume wote wa Mungu na Manabii katika biblia takatifu.

 Kwamfano utaona mahali Fulani Mtume Paulo alisema maneno yafuatayo kwa uwezo wa Roho…

1Wakorintho 6:9  “Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? MSIDANGANYIKE; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti,  wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi”

Na mtu akausikia mstari huo aliouzungumza Paulo kwa ufunuo wa Roho, lakini akaudharau, na kuona kama kasema hayo kwa akili zake, siku ile ya hukumu, Maneno hayo ya Mtume Paulo yatamhukumu. Ndio maana Mtume Paulo mwenyewe alisema tena maneno yafuatayo..

Warumi 2: 16 “katika siku ile Mungu atakapozihukumu siri za wanadamu, SAWASAWA NA INJILI YANGU, kwa Kristo Yesu”.

Hapo anasema “sawasawa na Injili yangu”.. maana yake tutahukumiwa kulingana na Injili ya Paulo, na mitume wengine kwenye biblia, ndio maana nyaraka za Mitume, Roho Mtakatifu kazifanya leo kuwa ni Neno lake.  Chochote kilichozungumzwa na Mtume Paulo katika biblia, au Mtume Petro, au Yohana, au Mathayo kimekuwa ni NENO LA MUNGU KAMILI, na wala si la huyo mtume, na ndicho siku ile ya hukumu, kitakacho hukumu watu.

Mtume Paulo alisema  kwa ufunuo wa Roho…“  Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika kama sina upendo mimi si kitu”. Maana yake kama hatutatafuta upendo kwa bidii, na kujitumainisha kwa karama tulizo nazo, kama lugha au unabii,  siku ile hatutaurithi uzima wa milele, kwasababu Neno hili litasimama kutuhukumu, kwamba tulipaswa tuwe na upendo na si karama tu peke yake.

Lakini pamoja na hayo, Maneno yote ya Watumishi wa Mungu waliopo katika Biblia, yanasimama pia kutuhukumu leo, Maana yake ni kwamba Injili ya Musa, Paulo, Petro, Yohana, na wengine wengi katika biblia, yapo yanatuhukumu wakati huu.

Sasa yanatuhukumu kwa namna gani?

Jibu ni rahisi, kwa njia ya MASHITAKA!.

Mtu anayejiita ameokoka, na huku anajua kabisa katika biblia Mtume Paulo aliandika kwa uwezo wa Roho katika..

1Wakorintho 6:16  “Au hamjui ya kuwa yeye aliyeungwa na kahaba ni mwili mmoja naye? Maana asema, Wale wawili watakuwa mwili mmoja”

Na kwa kulijua hili neno, akakaidi na kwenda kufanya uasherati makusudi, moja kwa moja Shetani analichukua hili andiko na kwenda nalo mbele za Mungu, kumshitaki mtu huyo, atakachosema ni hichi>> “Bwana Mungu Yule mtu, anayesema amekupokea wewe, tazama anafanya uzinzi na kahaba makusudi na ilihali anajua kabisa katika maandiko yako umesema, yeye ajiunganishaye na kahaba ni mwili mmoja naye,”.

Kwa mashitaka kama hayo, shetani anashinda hoja juu yako, na hivyo unahesabika kuwa na hatia juu ya hilo andiko… Ni heri ungekuwa hujaokoka halafu unafanya hayo, shetani asingekuwa na hoja nyingi juu yako, lakini unasema umempokea Yesu lakini unafanya uasherati, hapo ndipo unakabidhiwa shetani na Adui yako shetani anaweza kukufanya lolote kuhakikisha kuwa unakuwa mwili mmoja na Yule unayezini naye… Maana yake matatizo yake yote na laana anazobeba huyo unayezini naye, zinakuja kwako (kwasababu mmeshakuwa mwili mmoja), hata kama anamapepo basi na wewe ni rahisi kuyashiriki. Ndio maana kuna hatari kubwa sana ya kulipuuzia Neno la Mungu, hata tukiwa hapa duniani, kabla hata ya kufika siku ya hukumu.

Hivyo ni muhimu sana kulifuata na kulishika Neno la Mungu, na wala si la kulidharau, kwasababu  ndilo tutakalohukumiwa nalo siku za Mwisho na ndilo linalotushitaki sasa kupitia adui yetu shetani. Na neno la Mungu linapatikana katika kitabu kimoja tu! Kinachoitwa Biblia yenye vitabu 66, na si kwenye kitabu kingine chochote.

Kama hujampokea Yesu leo, huu ndio wakati wako, shetani hakupendi kama unavyodhani, anachokitaka kwako ni ufe katika dhambi zako, siku ile ukahukumiwe na kutupwa katika lile ziwa la Moto. Huko tumwache aende peke yake, lakini sisi tujiokoe roho zetu kwa kumwamini Bwana wetu Yesu Kristo, na kutubu dhambi zetu, na kubatizwa katika ubatizo sahihi wa maji tele na kwa jina la Yesu, na kupokea Roho Mtakatifu, ili tujiweka salama na tuwe na uhakika wa uzima wa milele.

Bwana atubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

JE NI HALALI KUOA WAKE WENGI, AU KUTOA TALAKA?

MMESIKIA KWAMBA IMENENWA?

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 1

NJIA YA KUPATA WOKOVU.

Tofauti ya kazi ya Damu ya Yesu na Jina la Yesu ni ipi?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/05/03/je-musa-yupo-anawashitaki-watu-kulingana-na-yohana-545/