USIMLAANI KIZIWI, WALA USITIE KWAZO MBELE YA KIPOFU.

by Admin | 12 July 2021 08:46 am07

Walawi 19:14 “Usimlaani kiziwi, wala usitie kwazo mbele ya kipofu, bali umche Mungu wako; Mimi ndimi Bwana”.

Vifungu hivyo vinatuonyesha, tabia ya watu ambao wanatumia udhaifu wa watu wengine kuwaletea madhara au matatizo zaidi badala ya kuwasaidia.

Kibinadamu ukikutana na kipofu njiani, na anataka asaidiwe kuvuka barabara, bila shaka utamwonea huruma na kwenda kumshika mkono umvushe, huwezi kwenda kumvizia wakati gari linapita ndio umsogeze barabarani agongwe afe, afe huo sio utu.

Lakini cha ajabu ni kwamba hao watu wapo. Kwa mfano utakuta mtu anataka kununua bidhaa fulani, lakini kwa bahati mbaya mteja huyo hajui sana ubora wa bidhaa hizo, labda tuseme simu. Sasa muuzaji badala atumie busara kumwelekeza bidhaa bora, kinyume chake anatumia fursa ile, kwenda kumletea feki, na kumuuzia kwa bei ile ile ya orijino, kisa tu haijui orijino ipoje. Na mwisho wa siku mnunuzi anaitumie siku mbili tatu, imeharibika, anaitupa, anakuwa amepata hasara.  Sasa huo ndio ukwazo Bwana anaouzungumzia hapo mtu anaomwekea kipofu.

Hilo jambo linamkasirisha sana Mungu, Na kwa bahati mbaya wafanyabiashara wengi sana wanayo tabia hii. Ni tabia ya shetani, ambayo alikuwa nayo tangu zamani, Utakumbuka pale Edeni alipoona Hawa ni kipofu, hajui mema na mabaya, akatumia udhaifu huo kumdanganya, badala ya kumwelekeza kuyashika maagizo ya Mungu, na mwisho wake ukawa ni Hawa kutumbukia shimoni. Sasa wapo baadhi ya wanadamu waliokosa UTU namna hii, wanatumia udhaifu wa watu wengine kujitafutia faida zao.

Au utakuta ni mama ntilie, anaona akipika chakula bora hapati faida ya kutosha, anachowaza ni kwenda kutia  hamira kwenye ubwabwa wake, ili uvimbe awauzie wateja wengi zaidi, kwasababu anajua wateja wanapenda chakula kingi, Na amekuwa akifanya hivyo kwa muda mrefu, Hiyo yote ni kisa tu haonekani kwa wateja, wakati mwingine anapikia na mafuta ya trasfoma.. Hiyo ni dhambi inayomchukiza sana Mungu.

Walawi 19:14 “Usimlaani kiziwi, wala usitie kwazo mbele ya kipofu, bali umche Mungu wako; Mimi ndimi Bwana”.

Mwingine ni mtumishi wa Mungu, anakutana na mtu mwenye matatizo  fulani, pengine ya kiafya, au ya kifamilia, au ya kiroho sasa yeye badala amuhudumie kama mtumishi wa Bwana,anatumia nafasi  hiyo ya udhaifu wake, kumtisha, na kumpa  shuhuda za uongo, lengo tu ni atumie fursa hiyo kuchukua pesa zake. Watu kama hawa nimeshakutana nao sana. Huko ndio kutia kwazo mbele ya kipofu, na kumlaani kiziwi.

Tunapaswa tuwe kama Ayubu, ambaye alisema..

Ayubu 29:15 “Nalikuwa macho kwa kipofu, Nalikuwa miguu kwa aliyechechemea”.

Tuwasaidie wale ambao wanahitaji msaada, vilevile tuwaongoze mahali sahihi wale ambao wanahitaji kusaidiwa. Tumche Bwana wetu, Tupate  siku nyingi na za heri za kuishi katika dunia yake.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

Ni nani aliye kipofu, ila mtumishi wangu?

UFUNUO: Mlango wa 15

USIPOTEZWE NA MANENO YA MANABII WA UONGO.

SI KWA UWEZA WALA KWA NGUVU BALI KWA ROHO YANGU, ASEMA BWANA.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/07/12/usimlaani-kiziwi-wala-usitie-kwazo-mbele-ya-kipofu/