Kwanini Herode aliwakasirikia watu wa Tiro na Sidoni? (Matendo 12:20)

by Admin | 21 October 2021 08:46 pm10

Jibu: Tusome,

Matendo 12:20 “Naye Herode ALIKUWA AMEWAKASIRIKIA SANA WATU WA TIRO NA SIDONI; wakamwendea kwa nia moja, na wakiisha kufanya urafiki na Blasto, mwenye kukitunza chumba cha mfalme cha kulalia, wakataka amani; kwa maana nchi yao ilipata riziki kwa nchi ya mfalme.

21 Basi siku moja iliyoazimiwa, Herode akajivika mavazi ya kifalme, akaketi katika kiti cha enzi, akatoa hotuba mbele yao.

22 Watu wakapiga kelele, wakisema, Ni sauti ya Mungu, si sauti ya mwanadamu.

23 Mara malaika wa Bwana akampiga, kwa sababu hakumpa Mungu utukufu; akaliwa na chango, akatokwa na roho”.

Tiro na Sidoni ni miji iliyokuwepo kaskazini mwa mji wa Galilaya, miji hiyo kwasasa ni sehemu za Lebanoni.

Zamani za biblia Herodi ndiye alikuwa anatawala Yudea, na watu wa miji ya Tiro na Sidoni, walikuwa wanaitegemea Yudea kwa chakula. Lakini ulifika wakati Herode alichukizwa nao (biblia haijataja sababu ni nini), lakini alichukizwa nao, na akakatisha kuwauzia chakula hao watu wa Sidoni na Tiro.

Watu wa Tiro na Sidoni, walipokaa muda mrefu bila chakula, ikawabidi wakatafute amani na Herode huko Yudea, lakini njia waliyoitumia ni kumtafuta mtu aliyeitwa Blasto, ili amshawishi Herode waweze kuwa na mdahalo wa wazi na Hao watu wa Sidoni, kwasababu haikuwa rahisi Herode, kumfikia.

Huyu Blasto ambaye alikuwa anafanya kazi katika nyumba ya Mfalme Herode, na ambaye ndiye aliyekuwa mtu wake karibu kuliko wengine wote, alifanikiwa kumshawishi Herode azungumze na watu wa Tiro na Sidoni kwa wazi.

Hivyo siku ilipofika Herode alijitokeza kuzungumza na watu hao. Lakini kama inavyojulikana Herode alikuwa ni mtu wa kupenda utukufu, alikuwa anajitukuza yeye kama Mungu hapo Yudea. Alikuwa anapenda  kuabudiwa kama Mungu. Alimuua Yakobo ndugu yake Yohana kwa upanga, na mwisho alimfunga Petro ili amuue kama alivyomuua Yakobo,  lakini Malaika wa Bwana alimwokoa na mauti yake. Na hapa anasimama ili ajitukuze, awaonyeshe watu wa Sidoni na Tiro kwamba yeye ndiye anayetoa chakula!, pasipo yeye wao hawawezi kuishi.

Na watu wa Sidoni kwasababu ni watu wa kipagani waliozoea kuabudu miungu, na kumtukuza mtu yeyote ambaye wanamwona ni wa tofauti, kama wale watu wa Athene waliotaka kumtukuza Paulo na Barnaba..

Matendo 14:11 “Na makutano walipoona aliyoyafanya Paulo wakapaza sauti zao, wakisema kwa Kilikaonia, Miungu wametushukia kwa mifano ya wanadamu.

12 Wakamwita Barnaba, Zeu, na Paulo, Herme, kwa sababu ndiye aliyekuwa mnenaji”.

 Kadhalika na hawa watu wa Tiro na Sidoni walipomwona tu Herode kasimama anahutubia kimajivuno na kimajigambo kiasi kile, wote kwa pamoja wakaanza kupaza sauti zao na kusema “Hii ni sauti ya Mungu na si mtu..hii ni sauti ya Mungu na si mtu”

Tofauti na akina Paulo na Barnaba ambao wao walipoona watu wanawageuza miungu-watu walizirarua nguo zao na kuwaeleza kuwa wao ni watu tu kama wao, na sio Mungu. Kinyume chake Herode yeye hakufanya hivyo, bali moja kwa moja alizidi kujitukuza na kutaka kuchukua utukufu zaidi.

Na kwasababu Mungu hashiriki utukufu wake na wanadamu, pale pale Malaika wa Bwana alishuka akampiga Herode kwa change, Chango ni ugonjwa mbaya wa kuliwa na minyoo.. kwa maelezo marefu juu ya ugonjwa huu fungua hapa >>>>>> CHANGO KIBIBLIA

Lakini ni nini tunajifunza katika habari hiyo?

Tunachoweza kujifunza kikubwa ni kuwa Mungu hashirikiani utukufu na mwanadamu yeyote…Na ni jambo la hatari sana kutafuta ufukufu, jambo lililombadilisha shetani kutoka kuwa Kerubi na kuwa Ibilisi ni hilo hilo, la kutafuta kuabudiwa.

Na jambo lingine pia linalomhuzunisha Mungu sio sisi tu kutafuta kuabudiwa bali hata sisi tunapotafuta kuabudu watu au kitu kingine chochote.

Tunapoabudu sanamu, au watu, au fedha au kingine chotechote kile kuna hatari kubwa sana ya kuadhibiwa na Mungu.

Bwana atusaidie na kutubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

TUJIFUNZE JAMBO KWA WANAWAKE HAWA WAWILI:

HERODE NA PILATO, MAADUI WAWILI WAPATANA.

TABIA ZA WATAKAOMKARIBIA SANA MUNGU SIKU ILE.

CHACHU YA MAFARISAYO NA CHACHU YA HERODE.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/10/21/kwanini-herode-aliwakasirikia-watu-wa-tiro-na-sidoni-matendo-1220/