HERI WAPATANISHI, MAANA HAO WATAITWA WANA WA MUNGU

by Admin | 9 May 2022 08:46 am05

Unajua ni kwasababu gani Bwana Yesu aliitwa Mwana wa Mungu? ..Mungu kukuona wewe kama  mwana wake kweli kweli sio tu uwe umezaliwa na yeye kwa kumkiri na kubatizwa, hapana bali pia kuwa na huduma ya upatanisho ndani yako….

Biblia inasema..

Mathayo 5:9

[9]Heri wapatanishi;

Maana hao wataitwa wana wa Mungu.

Jiulize Kwanini isiseme wataitwa watakatifu, au wataitwa wafalme, au wataitwa makuhani wa Mungu..bali wana wa Mungu.

Hilo jambo ambalo Yesu Kristo alilijua ndio maana kusudi lake kubwa la yeye kuja duniani, lilikuwa ni kutupatanisha sisi na Mungu..Yaani sisi tuliokuwa tumefarakana na Mungu kwasababi ya dhambi, sasa tunawasiliana naye kwa kupitia Yesu Kristo mwana wake..

Tunalithibitisha hilo katika mistari hii..

2 Wakorintho 5:18-19

[18]Lakini vyote pia vyatokana na Mungu, aliyetupatanisha sisi na nafsi yake kwa Kristo, naye alitupa huduma ya upatanisho;

[19]yaani, Mungu alikuwa ndani ya Kristo, akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake, asiwahesabie makosa yao; naye ametia ndani yetu neno la upatanisho.

Umeona? Tendo la Yesu kuacha enzi na mamlaka, na kuja duniani ili kutupatanisha tu sisi hilo ndio lililomfanya Mungu amwone kuwa ni mwana  bora kuliko wana wake wote aliokuwa nao.

Ndio maana akamshuhudia  mwenyewe..Huyu ni mwana wangu, mpendwa wangu, niliyependezwa naye. (Mathayo 3:17)

Akampa kibali cha kipekee kuliko wanadamu wote walioko ulimwenguni.

Hata sisi ili  Mungu atuone ni wana wake kwelikweli hatuna budi kuwa na huduma hii ya upatanisho ndani yetu.

Tuulete ulimwengu kwa Kristo. Lakini jambo ambalo hatujui ni kuwa kuwapatanisha watu waliogombana si jambo rahisi..la kwenda kuwashikanisha mikono tu halafu basi.. Hapana..lina gharama kubwa sana..kama ulishawahi kujaribu utalithibitisha hilo.

Ilimlazimu Yesu aache enzi na mamlaka, aje duniani, na kama hiyo haitoshi akataliwe kwanza na wale anaowapatanisha, (yaani sisi), na bado autoe uhai wake pia kwa ajili wao.

Kwa ufupi ni kwamba alikuwa anafosi upatanisho ambao ulikuwa hauwezekani kwa namna yoyote ile, ni uadui uliokuwa umekomaa..lakini hakukata tamaa, hadi mwisho wa siku ukatokea tu wenyewe.

Na sisi vivyo hivyo anasema ametupa huduma ya upatanisho. Yaani na sisi tukaupatanishe ulimwengu na Mungu kwa kupitia yeye.

Hivyo tufahamu kuwa tunapowahubiria watu, hadi kuokoka halitakuwa jambo rahisi kama sisi tunavyodhani..Watu wengi wamekatishwa tamaa  kuhubiri habari njema..kisa watu wanaowahubiria hawana geuko au badiliko, lolote..wengine ndio wanawatukana na kuwapiga

Hatuna budi kuendelea..kwasababu hakuna upatanisho ulio mwepesi. Ni unajitoa sadaka kwa vita ambayo si yako. Leo atakupuuzia, kesho atakutukana, lakini kesho kutwa ataokoka.

Ukifanikiwa kwa jambo hilo moja. Utajiongezea daraja la juu zaidi mbinguni..La kuwa mwana mpendwa wa Mungu. Na kwa jinsi unavyoendelea kufanya ndivyo kubali chako kinavyoongozeka kwa Mungu, hatimaye..kufikia kilele cha kufanana na Yesu Kristo..Ukimwomba Mungu lolote atakupa, na kazi zake zote utazifanya..Kama yeye alivyosema maneno haya..

Yohana 5:20-21

[20]Kwa kuwa Baba ampenda Mwana, naye humwonyesha yote ayatendayo mwenyewe; hata na kazi kubwa zaidi kuliko hizo atamwonyesha, ili ninyi mpate kustaajabu.

[21]Maana kama Baba awafufuavyo wafu na kuwahuisha, vivyo hivyo na Mwana awahuisha wale awatakao.

Umeona hiyo ndio faida za kuwa mwana wa Mungu kwelikweli.

Nasi pia tuanze kwa kuthamini wengine, kwa kuwahubiri habari njema, hapo tutakuwa tunaukiri UWANA wetu kwa Mungu..Ukimwona jirani yako amepotea basi pambana naye kwa hali na mali mpaka amgeukie Kristo kama wewe…wakati mwingine ugumu utakuwepo japo si kwa wote..

Ukifahamu kuwa hakuna upatanisho usiokuwa na gharama, basi utakuwa na uvumilivu na amani kwa yote utakayokutana nayo.

Bwana akubariki.

Uwe na utumishi mwema wa upatanisho.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

MJUE SANA YESU KRISTO.

UVUVI BORA HAUCHAGUI, CHA KUVUA.

Heri maskini wa roho maana ufalme wa mbinguni ni wao.

Kwanini, tuimbe, je! kuna ulazima wowote wa kufanya hivyo?

Injili iliyopo kwa Samaki aina ya Eeli.

Kiyama ni nini?

DHIKI KUU INAKUJA NA UNYAKUO UPO KARIBU.

MAUTI NA KUZIMU ZIKAWATOA WAFU WALIOKUWAMO NDANI YAKE.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/05/09/heri-wapatanishi-maana-hao-wataitwa-wana-wa-mungu/