Bwana alimaanisha nini kusema “waache wafu wazike wafu wao.(Mathayo 8:21)?

by Admin | 2 September 2019 08:46 pm09

JIBU: Ili kufahamu vizuri hii habari turudi kidogo kwenye historia ya Wayahudi katika shughuli zao za mazishi, Kumbuka Waisraeli walivyozika zamani sio kama wanavyozika leo, leo hii mtu akifa wanamvisha sanda,(katika baadhi ya tamaduni) kisha wanamfukia chini bila jeneza, na shughuli inakuwa imeisha, lakini zamani, haikuwa hivyo katika tamaduni zao, kwanza makaburi yalikuwa sio ya kuchimbwa chini futi 6 kama yanayotumika sasa hivi hapana, bali yalikuwa yanachongwa kwenye mwamba, au pango lililotokea lenyewe asilia, na yalikuwa sio ya kuzikia mtu mmoja mmoja hapana bali yalikuwa ni ya familia, na kulikuwa kuna kuzikwa “kwa kwanza” na “kuzikwa kwa pili”, tofauti na tamaduni karibu zote tulizonazo sasahivi.

 Kwa mfano imetokea mshirika wa familia amekufa, mwili wake ukishaoshwa na kuvishwa sanda, ulikuwa unapelekwa kwenye kaburi hilo la familia, wakifika huko wanamweka sehemu yake maalumu peke yake,kwenye shelfu ambalo litakuwa limechongwa ndani ya kaburi hilo na huko wanaoruhusiwa kuingia ni wanafamilia tu, Hivyo wakishamlaza jambo linalofuata wanalifunga kaburi kwa jiwe kubwa kisha wanalisakafia, kisha wanarudi nyumbani kuendelea na maombolezo ambayo hayo yanadumu kwa muda wa siku kadhaa ikiwa aliyefariki ni mtoto katika familia, lakini kama ni mzazi iwe ni baba au mama siku za kuomboleza zinaendelea kwa muda wa mwaka mzima..Kisha baadaye mwaka ukishaisha wanafamilia wote na ndugu wanakusanyika tena kwa ajili ya maziko ya pili. 

Hapa ndipo mifupa ya Yule marehemu inatolewa, pale alipolazwa mara ya kwanza na kupelekwa kwenye shelfu lingine lenye mifupa ya wanafamilia wote waliokufa kabla yake, na mifupa yake inalazwa pamoja na ya kwao, kisha habari ya mazishi inakuwa imeisha rasmi, na ndio maana kama ulishawahi kusikia, pale biblia “inaposema akafa akakusanywa pamoja na watu wake”, hilo lilikuwa ni tendo la mwilini ambalo lilifunua tendo la rohoni, (Soma Mwanzo 49:29-33, Hesabu 20:24, Waamuzi 2:10 n.k.)…Kuna kukusanywa katika mwili na katika roho pia. Lakini hatutaenda huko sana. Sasa turudi kwenye swali, kwanini Bwana alimwambia Yule mtu vile..tusome:

Mathayo 8:21 ‘Mwingine katika wanafunzi wake akamwambia, Bwana, nipe ruhusa kwanza, niende nikamzike baba yangu.

22 Lakini Yesu akamwambia, Nifuate; waache wafu wazike wafu wao’.

Tumekwisha kuona jambo la kumzika Baba, halikuwa jambo jepesi la kwenda na kurudi kuchukua siku mbili au tatu, ni jambo linalochukua mwaka..Lisingekuwa jambo kubwa kwa Bwana kumwambia nenda urudi, Kama ni hivyo hata Bwana Yesu asingekaa kuhudhuria msiba wowote lakini tuona aliposikia habari za msiba wa Lazaro pamoja na umbali wote ule na hatari zote zile za kutaka kuuliwa.(Yohana 11),lakini alifunga safari kwenda kumponya. Lakini utaona huyu mtu alikuwa anajaribu kutafuta njia za kuikwepa kazi ya Kristo. 

Ndugu fahamu kuwa ili uwe mwanafunzi wa Yesu, ipo gharama ya kuingia, yeye mwenyewe alisema apendaye Baba au Mama kuliko mimi hanistahili. Pale Mungu anapokuambia sasa ni wakati wa wewe kunitumikia, usiwe ni wakati wa wewe kusema ngoja kwanza nikamalizie kufanya biashara zangu msimu huu ukiisha nitakutumikia, Mungu hataki udhuru. Na ndio maana akamwambia Yule mtu waache wafu wawazike wafu wao, ikimaanisha kuwa mtu yeyote aliye mbali na Kristo, ni mfu tayari katika roho japo atakuwa anatembea, lakini mauti ipo ndani yake na siku akifa wafu wenzake ambao bado hawajafa ndio watakaokwenda kumzika, Mauti inaanzia tukiwa tunapumua kadhalika wokovu unaanzia tukiwa bado tunapumua hapa hapa duniani..ndio maana hatuokoki tukishafika kule, wokovu unaanzia hapa hapa duniani, tunaokoka hapa, kule ni hitimisho la wokovu wetu. hivyo sisi tunaonywa pia tusitoe udhuru kwa vitu tuvipendavyo pale Yesu anapotuchagua tumfuate. 

Bwana akikuita umtumikie, na amekuambia acha kitu Fulani, usianze kutazama ni jinsi gani utawaachia wengine hiyo fursa wewe waachie wanaokifanya hicho kitu waendelee kukifanya wewe nenda kamtumikie Mungu, ikiwa leo hii amekuambie acha biashara haramu nifuate, usianze kumwambia Mungu ngoja kwanza nimalizie kuuza hizi zilizopo kisha nitaanza kufanya biashara halali. Mungu hapendi kuwekwa wa mwisho. 

Na ndio maana YESU akawaambia wanafunzi wake. ‘’Mtu aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa Mungu’’.(Luka 9:62). Ukristo unayo gharama. Ni kujikana na kupiga gharama kweli kweli.

Ubarikiwe.


Mada Nyinginezo:

JE! NI KWELI UMEMFUATA YESU?

JIKANE NAFSI MTEULE WA MUNGU.

MKUMBUKE MKE WA LUTU.

UKOMA NA UJANE ULIO NDANI YAKO, UMEUPATIA TIBA?

LENGO LA SHETANI KWA WATOTO WA KIZAZI HIKI.

JINSI ITAKAVYOKUWA KATIKA SIKU ILE


Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/09/02/bwana-alimaanisha-nini-kusema-waache-wafu-wazike-wafu-wao-mathayo-821/