Je! “majira na sheria” mpinga-kristo atakayokuja kubalisha ni kupindua siku ya sabato na kuwa jumapili?

by Admin | 2 September 2019 08:46 pm09

SWALI: Nina swali kuhusu alama ya mnyama, kulingana na baadhi ya injili zinazohubiriwa ni kuwa ..alama ya mnyama itapimwa kwa siku ya kuabudu, yani wale watakaokubali kusali jumapili wote watakuwa wamepokea 666, ikimaanisha kuwa Papa atatangaza siku moja tu ya kuabudu iwe jumapili dunia nzima, lengo likiwa kuvunja amri ya nne itunze siku ya saba, kwahyo amri ya papa itakapopita itapiga 666 kwa wote watakaokubaliana nayo, wana refer maandiko ya Danieli 7:25 KUWA ATABADILI MAJIRA NA SHERIA.


JIBU: Shalom ndugu, Ni kweli kabisa wapo wanaoamini kuwa Papa atageuza MAJIRA NA SHERIA kulingana na Danieli 7:25….Lakini ukijifunza biblia utagundua kuwa majira yanayozungumziwa hapo sio siku moja maalum itabadilika…hapana! Kwasababu majira ni Neno pana na la wingi ambalo linaweza kuwa kipindi Fulani cha muda…labda cha siku kadhaa, wiki, miezi au miaka kadhaa…kinachoambatana na tukio Fulani.   Ili tuelewe vizuri hebu tuchukue mifano kadhaa ya kwenye biblia..

Luka 21: 7 ‘’Wakamwuliza wakisema, Mwalimu, mambo hayo yatakuwa lini? Nayo ni nini ishara ya kuwa mambo hayo ya karibu kutukia? 8 Akasema, Angalieni, msije mkadanganyika, kwa sababu wengi watakuja kwa jina langu, wakisema, Mimi ndiye; tena, MAJIRA YAMEKARIBIA. Basi msiwafuate hao’’.  

Katika mstari huo unaona neno MAJIRA lilivyotumika hapo, sio kipindi cha SIKU MOJA MAALUM ambacho kitafika watu watakuja kwa jina lake na kusema wao ndio…Utaona sio tafsiri yake hiyo, bali majira ilivyotumika hapo ni kwamba ‘itafika kipindi Fulani cha muda’ ambacho hakijulikani kitadumu kwa muda gani ambapo watatokea manabii wa uongo wakija kwa jina la Yesu…Na hicho kipindi ndio hichi tunachoishi sasa,   Pia tunaweza kujifunza katika huu mfano mwingine Bwana alioutoa..  

Luka 12:54 ‘’Akawaambia makutano pia, Kila mwonapo wingu likizuka pande za magharibi mara husema, Mvua inakuja; ikawa hivyo. 55 Na kila ivumapo kaskazi, husema, Kutakuwa na joto; na ndivyo ilivyo.Enyi wanafiki, mwajua kuutambua uso wa nchi na mbingu; imekuwaje, basi, kuwa hamjui kutambua MAJIRA haya?’’  

Unaona hapo tena?…Majira yanayozungumziwa hapo ni kipindi Bwana Yesu alichokuwepo duniani akihubiri na kufundisha njia za haki…ni majira ambayo makutano walishindwa kufahamu kuwa Masihi yupo ulimwenguni…Na majira hayo ni kipindi cha miaka mitatu na nusu Bwana aliyokuwa anahubiri..na sio siku Fulani moja maalum.   Pia mfano mwingine ni huu..

Kutoka 21:18 ‘’Watu wakigombana, na mmoja akimpiga mwenziwe kwa jiwe, au kwa konde, asife, lakini yualazwa kitandani mwake;atakapoinuka tena na kuenenda nje kwa kutegemea fimbo, ndipo hapo yule aliyempiga ataachwa; ila atamlipa kwa ajili ya hayo majira yake yaliyompotea, naye atamwuguza hata apone kabisa..’’..

Hapo pia utaona ‘majira’ sio siku moja maalumu bali kipindi cha muda.   Kadhalika pia tunaweza kujifunza mfano huu wa mwisho maana ya majira..  

Luka 21: 29 ‘’Akawaambia mfano; Utazameni mtini na miti mingine yote. 30 Wakati iishapo kuchipuka, mwaona na kutambua wenyewe ya kwamba MAJIRA YA MAVUNO yamekwisha kuwa karibu. 31 Nanyi kadhalika, mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu.’’  

Unaona majira ya mavuno yanayozungumziwa katika maandiko sio siku moja MAALUMU, kama wasabato wanavyodhania, bali ni kipindi Fulani cha mavuno ambacho kinaweza kuwa ni siku kadhaa, au wiki kadhaa…Ipo mifano mingi unaweza ukapitia Pia (pitia Luka 21:54-55, Luka 21:23-25, Luka 19:41-44 utaelewa zaidi juu ya jambo hilo).  

Kwahiyo tukirudi pale kwenye Danieli 7:25…Kwamba Mpinga kristo atabadili ‘’majira na sheria’’ biblia haikumaanisha kuwa mpinga kristo atakuja kubadilisha siku moja ya kuabudu Jumamosi na kuwa jumapili…Hapana bali MAJIRA yatakayobadilika hapo ni MAJIRA YA mfumo mzima wa maisha, kutoka kuwa ya amani na kuwa ya dhiki, huwezi kununua wala kuuza bila ile chapa…wakati huo Majira ya Neema yatakuwa yameisha na sasa ni majira ya dhiki kuu….yatakuwa ni majira ya mavuno..na hayo hayatakuwa siku moja hapana ni kipindi fulani cha muda ambacho kitadumu miaka mitatu na nusu…Kwahiyo mfumo wake mpya wa umoja wa dini na madhehebu yote ndio utakaobadili majira ya ulimwengu mzima..  

Kama vile ujio wa Kristo ulivyobadili majira kutoka majira ya utumwa wa dhambi na sheria na kutuingiza katika majira ya Neema na uhuru wa roho, kadhalika baada ya unyakuo wa kanisa kupita Mpinga Kristo ataiingiza dunia katika majira mapya ya dhiki kuu na ghadhabu ya Mungu.   Kumbuka sasahivi tunaishi kipindi cha majira ya Neema ya Kristo, ambacho kinajulikana kama kipindi cha MAJIRA YA MATAIFA.(ukisoma Luka 21:24 utaona jambo hilo) Na kipindi hichi kitaishia na unyakuo.   Hivyo fundisho la wasabato linalosema kutotunza sabato, ndio kupokea alama ya mnyama, ni fundisho potofu na linapaswa liepukwe kwasababu halina msingi wowote wa kimaandiko.  

Bwana akubariki sana.


Mada Nyinginezo:

SABATO HALISI NI LINI, JE! NI JUMAPILI AU JUMAMOSI?, NI SIKU GANI ITUPASAYO KUABUDU?

LENGO LA SHETANI KWA WATOTO WA KIZAZI HIKI.

PENTEKOSTE NI NINI?

NJIA YA ‘UTAJIRI MKUU’ KWA KIJANA.

SAUTI AU NGURUMO?

MSTARI HUU UNA MAANA GANI? “TUPA CHAKULA CHAKO USONI PA MAJI; MAANA UTAKIONA BAADA YA SIKU NYINGI”. (MHUBIRI 11:1)

KWANINI MUNGU ANAMPA NABII HOSEA MAAGIZO YA KUMUOA MWANAMKE KAHABA?


Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/09/02/je-majira-na-sheria-mpinga-kristo-atakayokuja-kubalisha-ni-kupindua-siku-ya-sabato-na-kuwa-jumapili/