NITAFANYA YERUSALEMU KUWA JIWE LA KUWALEMEA .

by Admin | 14 December 2019 08:46 am12

Nitafanya Yerusalemu kuwa jiwe la kuwalemea watu wa kabila zote;


Kitakachochochea vita kuu mbili kuu ambazo tunazitazamia kuja huko mbeleni..ambayo ya kwanza ni ile vita ya Gogu na Magogu inayozungumziwa katika kitabu cha Ezekieli 38 & 39. Na ya pili ni ile ya Harmagedoni inayozungumziwa katika Ufunuo 16:15 na Ufunuo 19:11-21 ambayo hiyo itakuwa ni Mungu mwenyewe. Ipo nyingine ya Tatu ambayo itakuja kutokea baada ya ile miaka 1000 ya utawala wa Kristo kuisha, ambayo nayo itahusisha Magogu, lakini hiyo hatutaizungumzia leo hapa.

Hiyo ya kwanza inasema mfalme wa kaskazini atashuka akiyangoza baadhi ya mataifa ya kando kando, yatakusanyika  lengo lao likiwa ni kuindoa Israeli katika ramani ya dunia..Na kwasasa tunajua mfalme huyo wa Kaskazini atakuwa si mwingine Zaidi ya Taifa la URUSI, (ndio Gogu na Magogu), kwasababu hilo ndilo lipo upande wa kaskazini mwa Israeli, na ndio lenye nguvu kwa ukanda ule wote..Hivyo Siku za usoni, tendo hilo litafanyika, lakini hawatashinda, kwani watauawa kwa mauaji ya halaiki, biblia inasema kutakuwa na mizoga ya miili ya watu itafagiliwa kwa muda wa miezi saba pale Israeli.. na silaha zao watazitumia kama nishati kwa muda wa miaka 7 kwa jinsi zitakavyokuwa nyingi..

Ezekieli 39:12 “Na kwa muda wa miezi saba nyumba ya Israeli watakuwa wakiwazika, wapate kuisafisha nchi.

13 Naam, watu wote wa nchi hiyo watawazika; itakuwa ni sifa kwao katika siku ile nitakapotukuzwa, asema Bwana MUNGU.

14 Nao watawachagua watu wa kufanya kazi ya daima, watakaopita kati ya nchi, ili kuwazika waliosalia juu ya uso wa nchi, ili kuisafisha; miezi saba itakapokwisha kupita watatafuta”

Na wakati huo ndio utakaokuwa mwisho wa Taifa la Urusi halitakuwepo tena.

Na vita nyingine ni ile ya Harmagedoni, hii itaongozwa na mataifa yatokayo katika mawio ya jua, mataifa ya Mashariki ya mbali, nayo yatakuwa si mengine Zaidi ya korea, Japani, China, Tawani..haya ndio yatakayoingoza vita hiyo, na safari hii haitakuwa mataifa machache tu, hapana bali itakuwa ni mataifa yote duniani yaliyosalia yataungana na hawa viongozi wao kwa ajili ya kuipoteza tena Israeli.

Unaweza ukajiuliza ni kwanini jambo hili litokee tu kwa Israeli?.. Kwani Wana ugomvi gani hasaa mkubwa mpaka ifikie hatua mataifa yote ulimwenguni yanaungana kwenda kukishambulia ki-nchi kidogo kama kile chenye ukubwa usiozidi hata mji wa Daresalaam.

Kama ukifuatilia utagundua Israeli kwasasa hawaingilii siasa zozote…au mambo ya mataifa mengine, kama yanavyofanya sasahivi mataifa makubwa kama vile Marekani, au mataifa ya Ulaya, ambayo hayo kimsingi ndio yangepaswa yawe na sababu za kutosha za kuwa na maadui.

Lakini Israeli, haifanyi chochote lakini inachukiwa,..Watu hawajui kuwa jambo hilo linatoka kwa BWANA. Ikiwa leo hii hata bado neema haijawarudia wayahudi, tayari ni maadui wa mataifa mengi, Fikiria siku ambapo watarudiwa ni nini kitatokea?

Hili shinikizo lilipo sasa litazidi hata Zaidi ya mara mia kwa jinsi siku zinavyozidi kusogea, Mungu atanyanyua visa, mbalimbali ambavyo vitayafanya mataifa yote sasa yawe na kusudi moja la kuingamiza Israeli.. Ni Mungu mwenyewe atayachochea haya mataifa kwa namna isiyo ya kawaida, atayachochoe, kweli kweli mpaka hilo Neno litatimia linalosema…

Zekaria 12:2 “Angalia, mimi nitafanya Yerusalemu kuwa kikombe cha kuyumba-yumba kwa watu wa kabila zote, wazungukao pande zote; tena kitakuwa juu ya Yuda pia wakati wa kuhusuriwa Yerusalemu”.

3 Tena itakuwa siku hiyo, nitafanya Yerusalemu kuwa jiwe la kuwalemea watu wa kabila zote; wote watakaojitwika jiwe hilo watapata jeraha nyingi; na mataifa yote ya dunia watakusanyika pamoja juu yake.

Unaona, hiyo ndio itakayopelekea sasa mataifa yote duniani kufikia Kiama chao..

Watakusanyika pale Harmagedoni..Sasa kumbuka wakati huo Taifa la Israeli litakuwa litakuwa limeshamwamini Masihi wao Yesu Kristo, hivyo watapaza sauti zao na kumlilia, aje kuwapigania kama alivyowapigania enzi za kale. Wakati huo ambapo mataifa yote sasa yameshaizunguka nchi hiyo ndogo,.. ndipo watakapomwona mwa Adamu akishuka na mawingu kutoka mbinguni kwa nguvu na utukufu mwingi akiwa na majeshi wa watakatifu wake ambao alishawanyakua.

Na hapo ndipo mataifa yote yatakapoomboleza, lakini utakuwa ndio mwisho wao, Bwana atawauwa wote kwa upanga utokao katika kinywa chake..

Ufunuo 19:11 “Kisha nikaziona mbingu zimefunuka, na tazama, farasi mweupe, na yeye aliyempanda, aitwaye Mwaminifu na Wa-kweli, naye kwa haki ahukumu na kufanya vita.

12 Na macho yake yalikuwa kama mwali wa moto, na juu ya kichwa chake vilemba vingi; naye ana jina lililoandikwa, asilolijua mtu ila yeye mwenyewe.

13 Naye amevikwa vazi lililochovywa katika damu, na jina lake aitwa, Neno la Mungu.

14 Na majeshi yaliyo mbinguni wakamfuata, wamepanda farasi weupe na kuvikwa kitani nzuri, nyeupe, safi.

15 Na upanga mkali hutoka kinywani mwake ili awapige mataifa kwa huo. Naye atawachunga kwa fimbo ya chuma, naye anakanyaga shinikizo la mvinyo ya ghadhabu ya hasira ya Mungu Mwenyezi.

16 Naye ana jina limeandikwa katika vazi lake na paja lake, MFALME WA WAFALME, NA Bwana WA MABwana.

17 Kisha nikaona malaika mmoja amesimama katika jua; akalia kwa sauti kuu, akiwaambia ndege wote warukao katikati ya mbingu, Njoni mkutane kwa karamu ya Mungu iliyo kuu;

18 mpate kula nyama ya wafalme, na nyama ya majemadari, na nyama ya watu hodari, na nyama ya farasi na ya watu wawapandao, na nyama ya watu wote, waungwana kwa watumwa, wadogo kwa wakubwa.

19 Kisha nikamwona huyo mnyama, na wafalme wa nchi, na majeshi yao, wamekutana kufanya vita na yeye aketiye juu ya farasi yule, tena na majeshi yake”.

Wakati huo upo karibu sana, leo hii kila mmoja wetu anashuhudia kinachoendelea mashariki ya kati, kama wewe si mfuatiliaje wa taarifa za habari..anza kufuatilia habari hususani za mashariki ya kati… jifunze, au ulizia ufahamu mambo yanayoendelea ulimwenguni.. Idadi ya mataifa yanayoipinga nchi ya Israeli inazidi kuongozeka, dini zinazolichukia taifa la Israeli nazo zinaongezeka.

Hilo lote ni shinikizo kutoka kwa Bwana mwenyewe..Kutuonyesha kuwa mwisho upo karibuni sana..

Nitafanya Yerusalemu kuwa jiwe la kuwalemea watu wa kabila zote;

Na kabla hayo yote hayajatokea Utatangulia unyakuo wa kanisa kwanza..Ambao dalili zote zinaonyesha wakati wowote kuanzia sasa parapanda italia..na wafu wote waliokufa katika Kristo watafufuka na kwenda katika karamu ya mwanakondoo mbinguni..

Ila wale waliobakia mlango wa neema hautakuwa kwao tena, bali kwa wateule wa Mungu wayahudi..Leo hii unasubiri nini usimruhusu Kristo aingie maishani mwako akubalishe, usidanganywe na uvumi kama uvumi wa amani unaouna sasa hivi, huo ni kuwapumbaza watu waone kama tuna mamilioni ya miaka hapa duniani.. biblia inasema…

1Wathesalonike 5:1 “Lakini, ndugu, kwa habari ya nyakati na majira, hamna haja niwaandikie.

2 Maana ninyi wenyewe mnajua yakini ya kuwa siku ya Bwana yaja kama vile mwivi ajavyo usiku.

3 Wakati wasemapo, Kuna amani na salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa”.

Unaona? Tubu dhambi zote, umgeukie Kristo ndani ya wakati huu mfupi tuliobakiwa nao kabla ya parapanda kulia, tengeneza mambo yako kwasababu injili tuliyonayo sasa si ile tena ya zamani ya kuvutwa kwa maneno laini, tuliyonayo sasa ni ile ya mtakatifu na aendelee kujitakasa na mwenye dhambi aendelee kufanya dhambi..Kwani wakati wa mavuno upo karibu sana…Hivyo maombi yangu ni mimi na wewe tuangukie katika kundi la wanaojitakasa..

Bwana akubariki.

Mada Nyinginezo:

MPAKA UTIMILIFU WA MATAIFA UTAKAPOWASILI.

UTAWALA WA MIAKA 1000.

CHUKIZO LA UHARIBIFU

MTINI, WENYE MAJANI.

Vichwa saba vya mnyama wa kwenye Ufunuo 13 na 17, Ni nini?

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/12/14/nitafanya-yerusalemu-kuwa-jiwe-la-kuwalemea/