MAUTI YA PILI NI NINI?

by Admin | 17 December 2019 08:46 am12

Mauti ya pili ni nini?.. Ni  mauti inayofuata baada ya hii mauti ya kwanza…Mauti ya kwanza ni pale roho ya Uhai inapoutoka mwili..Yaani pale tu Roho inapotengana na mwili hiyo ndiyo mauti ya kwanza. Lakini mauti ya pili ni roho kujitenga na nafsi.

Mauti ya kwanza inaweza kusababishwa na mambo mbali mbali..Inaweza kusababishwa na aidha ugonjwa fulani, au ajali fulani ambayo mtu anaweza kuipata…Lakini pia inaweza isisababishwe na ajali wala ugonjwa ikasababishwa na jambo lingine…

Hivyo mtu anapokufa katika hii mauti ya kwanza..(Yaani roho inapotengana na mwili)..Mtu huyo mwili wake unakwenda kuzikwa kaburini, unaoza na kuliwa na funza na kuwa mavumbi…lakini nafsi yake na roho yake zinakuwa hazijafa hivyo zinakwenda mahali pa wafu…

Mahali pa wafu nako kumegawanyika katika sehemu mbili..Sehemu ya kwanza ni mahali ambapo wafu waliokufa katika Kristo wanahifadhiwa..ambapo kwa lugha nyingine panaitwa peponi au paradiso..ni mahali pa raha sana na hapana mateso…

Na sehemu ya pili ni mahali panapojulikana kama KUZIMU au Jehanamu..ni mahali ambapo roho za wanadamu wote waliokufa katika dhambi zinahifadhiwa kwa muda..ni sehemu ya mateso mabaya sana.

Siku ya unyakuo itakapofika roho zilizohifadhiwa paradiso zitafufuliwa na kupewa miili ya utukufu na kwenda mawinguni na Bwana Yesu…lakini zilizosalia ambazo zipo kuzimu..siku ya hukumu zitafufuliwa nazo na kuhukumiwa  kila mmoja sawasawa na matendo yake.

Yohana 5:28 “Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake.

29 Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu”.

Sasa roho hizi ambazo zilikuwa zipo jehanamu/kuzimu baada ya kuhukumiwa….zitakusanywa zote na kutupwa katika ziwa la moto..Ziwa la moto ni tofauti na jehanamu…Na zitaungua huko kwa muda mrefu sana…Zilizofanya maovu sana kuliko nyingine zitaungua kwa muda mrefu…na zilizofanya machache zitaungua kwa muda pungufu kidogo wa hizo nyingine…

Baada ya kipindi kirefu sana kisichoelezeka cha mateso ndani ya ziwa la moto hatimaye roho zote zilizotupwa katika ziwa la moto zitakufa..Atakayekufa wa mwisho katika jehanamu ya moto atakuwa ni shetani huyo ndiye mwenye adhabu kubwa kuliko wote..wakifuatiwa na mapepo wake, wakifuatiwa na wachungaji na waaalimu wa uongo na manabii wa uongo..na mwisho watu wengine waovu waliosalia kila mmoja kulingana na uovu alioufanya..Hiyo ndio itakuwa MAUTI YA PILI, yaani kifo katika ziwa la moto..Roho kutenganishwa na nafsi.

Ufunuo 20:12 “Nikawaona wafu, wakubwa kwa wadogo, wamesimama mbele ya hicho kiti cha enzi; na vitabu vikafunguliwa; na kitabu kingine kikafunguliwa, ambacho ni cha uzima; na hao wafu wakahukumiwa katika mambo hayo yaliyoandikwa katika vile vitabu, sawasawa na matendo yao.

13 Bahari ikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake; na Mauti na Kuzimu zikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake. Wakahukumiwa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake.

14 Mauti na Kuzimu zikatupwa katika lile ziwa la moto. Hii ndiyo mauti ya pili, yaani, hilo ziwa la moto.

15 Na iwapo mtu ye yote hakuonekana ameandikwa katika kitabu cha uzima, alitupwa katika lile ziwa la moto”.

Inajulikana na wengi kwamba ziwa la moto ni la milele lakini kiuhalisia sio la milele…Milele ilivyotumika katika kitabu cha ufunuo ni Everlasting…Yaani maana yake “kudumu muda mrefu” na si “eternal” ambayo maana yake ni milele…

Sasa kama mtu atakuwepo kuzimu milele tayari maana yake anao uzima wa milele…kitu ambacho sio kweli…Mwenye uzima wa milele ni Mungu tu..Na wana wa Mungu waliookolewa hao ndio watakaopata uzima wa milele..(yaani wataishi milele) Lakini roho zote zilizoasi zitakufa!. Biblia inasema hivyo..hata shetani naye pia atakufa…hana uzima wa milele.

Hivyo tofauti na wengi wanadhani kwamba adhabu kuu atakayoipata mwanadamu aliyeasi ni kuchomwa moto kuzimu…La! Hiyo sio adhabu…Adhabu kubwa au pigo kubwa  hasa ni kuupoteza uzima wa milele..Yaani kufa na kutoweka kana kwamba hujawahi kuwepo kabisa…Na kifo hicho ni katika ziwa la moto. Hebu tafakari unakuwa haupo!

Hivyo Uzima sio kitu cha kufanyia mchezo kabisa…Tukose kila kitu lakini si uzima wa milele. Na uzima huu unapatikana kwa Yesu Kristo mwenyewe…Hivyo kama hujaokoka..mlango upo wazi sasa ila hautakuwa hivi siku zote..Tubu kwa kudhamiria kuacha kabisa dhambi, na kisha kabatizwe katika ubatizo sahihi ambao ni wa maji mengi na kwa jina la Yesu kama hujabatizwa. Na Roho Mtakatifu atakuongoza katika kweli yote na kukusaidia katika kuishi maisha masafi yanayompendeza Mungu.

Lakini kama usipotubu na kuipenda dunia..na kuendelea kuwa mlevi, mzinzi, mwasherati, mwizi, msengenyaji, mwongo, muuaji, mchawi, mla rushwa na mtoaji mimba…Biblia imeweka wazi sehemu ya watu wa namna hiyo ni ziwa la moto (Hivyo mauti ya pili ni nini?)

unapozungumzia ziwa la moto maana yake ni mauti ya pili.

Ufunuo 21:8 “Bali waoga, na wasioamini, na wachukizao, na wauaji, na wazinzi, na wachawi, na hao waabuduo sanamu, na waongo wote, sehemu yao ni katika lile ziwa liwakalo moto na kiberiti. Hii ndiyo mauti ya pili”.

Bwana atusaidie. jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP

Tafadhali share na wengine na Bwana azidi kukubairiki.


Mada Nyinginezo:

Jehanamu ni nini?

KARAMA YA MUNGU NI UZIMA WA MILELE.

HATARI YA KUHUBIRI INJILI TOFAUTI NA ILIYOANDIKWA KWENYE BIBLIA.

KITABU CHA UZIMA

PENGINE MUNGU ALISHASEMA NAWE KWA NJIA HII.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/12/17/mauti-ya-pili-ni-nini/