JE KUCHOMA MAITI NI DHAMBI?

by Admin | 19 December 2019 08:46 am12

Je kuchoma maiti ni dhambi? mpaka iteketee kabisa na kuwa jivu?..Kwamfano maiti ya mtu aliyeokoka kuichoma kama wanavyofanya wahindu ni dhambi?..je hizo ni ibada za wafu?..mtu akifa roho yake inakwenda wapi?

JIBU: Kila kitu kinachofanywa na wanadamu kina sababu…hakuna kitu kinachofanyika bila sababu..katika Maziko, watu wanaoosha maiti kuna sababu kwanini wanafanya vile..kadhalika watu wanaoosha maiti na yale maji kupikia pia ipo sababu ya wao kufanya hivyo..Wanaokata kipande cha nyama ya maiti na kula kabla ya kumzika ipo sababu ya wao kufanya hivyo..

Kwahiyo hata wanaochoma maiti ipo sababu ya wao kufanya hivyo.. hawachomi basi tu kufanya mazingira yawe masafi..hapana! bali wanasababu kubwa kufanya hivyo..Na sababu hiyo ni ya kiroho…

Wahindu wanaamini kwamba mtu akifa roho yake inakuwa inaelea hapa hewani…lakini roho ya mtu yule bado inakuwa ina uwezo wa kuona na kuhisi mazingira iliyokuwepo..Na hiyo ni kutokana na ule mwili ulioacha hapo chini. Mwili ule unaizuia ile roho kuendelea na safari yake ya kwenda mbinguni..Kwahiyo ili kuifanya ile roho isibakie hapo juu muda mrefu..wahindu wanauchoma ule mwili kwa moto wote uteketee..ili roho isibaki kuutazama mwili na kuendelea kuishi katikati ya mazingira iliyokuwa inaishi.

Na baada ya mwili ule kuchomwa basi ile roho itakwenda mbinguni kwa haraka.

Je Mtazamo huo ni sahihi?

Jibu ni la!..Mtu akishakufa kama ni mwenye haki roho yake inakwenda moja kwa moja mahali panapojulikana kama paradiso au peponi…na anakuwa hana mawasiliano tena na mwili wake. Kadhalika aliyekufa katika dhambi anakwenda mahali pajulikanapo kama kuzimu/jehanamu. Naye pia anakuwa hana mawasiliano na mwili wake uliokufa.

Kwahiyo ni uongo wa shetani kusema kwamba mwili unazuia roho kwenda mbinguni..hivyo unapaswa uchomwe moto!..Hizo ni IBADA ZA WAFU. Kama zinavyofanywa na kanisa katoliki za kuwaombea wafu!.

Hivyo shetani amewadanganya watu wafanye hivyo (wachome maiti)..Kwasababu anajua kitendo hicho ni kama sadaka…Kumbuka sadaka zote katika agano la kale zilikuwa zinafanyika kwa kuchomwa…Sadaka ya kuteketezwa ilikuwa inafanyika kwa kumchukua aidha mwanakondoo au mbuzi na kumchinja na hatimaye kumkatakata na kuuweka mwili wake juu ya madhabahu na kuuchoma kwa moto mpaka uteketee kabisa..Na kitendo hicho kilikuwa kinaleta matokeo makubwa sana katika ulimwengu wa roho. Na madhabahu ilikuwa inatengenezwa kwa mawe kadhaa na juu ya mawe hayo zinapangwa kuna na kondoo anawekwa juu  yake…kama tu wahindu wanavyoteketeza maiti zao.

Katika agano la kale Ili dhambi ifunikwe ni lazima sadaka ya kuteketezwa ifanyanyike..Na mambo mengine yote ili yafanikiwe ni lazima sadaka ya kuteketezwa itumike.

Sasa baada ya Agano jipya kuja..sadaka hizo Mungu alizifuta!…Yesu Kristo kwa kupigwa kwake na kufa kwake pale msalabani yeye ndiye akafanyika kuwa sadaka kwa ajili yetu.(Soma Waebrania 10:1-10)..Hatuhitaji tena maiti ya kondoo kuteketezwa kwa moto juu ya madhababu ndipo tupate msamaha wa dhambi…Damu ya Yesu Kristo inatosha.

Lakini shetani kazi yake ni kucopy vitu na kuvigeuza na kuvitumia kwa faida zake..Naye pia akaiga mfano huo wa sadaka za kwanza za kuteketezwa kufanya shughuli zake…leo mtu akienda kwa waganga ataambiwa apeleke mbuzi, au kuku achinjwe na damu ipatikane..sehemu nyingine ataambiwa amchinje na kumchoma moto…majivu akatupe baharini n.k

Sasa shetani kwa kuimarisha uchawi wake akaona maiti za mbuzi na kuku hazitoshi…sasa akahamia kwa maiti za watu…Na hizo atazipataje kirahisi?..kwa kuanzisha mafundisho hayo potofu ya roho kuelea hewani… ili watu wachome maiti na kafara iwe imeshafanyika… Na matokeo ya kafara hizo ni kuingiza mapepo ndani ya watu hususani wafiwa na washiriki wa kafara hiyo.

Baada ya kumaliza kafara hiyo mtu yule aliyeshiriki..hali yake ya kiroho inakuwa mbaya zaidi kuliko alivyokuwa hapo kwanza.

Sasa sisi wakristo hatupaswi kabisa kufanya hayo mambo…kwasababu yanahusiana na ibada za wafu..Na biblia imetuonya tusifanye hivyo au mambo yanayokaribiana kufanana na hayo..

Ezekieli 20:31 “Tena mtoapo matoleo yenu, na kuwapitisha watoto wenu motoni, je! Mnajitia unajisi kwa vinyago vyenu vyote hata leo? Na mimi je! Niulizwe neno nanyi, Enyi nyumba ya Israeli? Kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, sitaulizwa neno na ninyi”.

Soma tena..

2 Wafalme 17:16 “Wakaziacha amri zote za Bwana, Mungu wao, wakajifanyizia sanamu za kusubu, yaani, ndama mbili, wakafanya na Ashera, wakaliabudu jeshi lote la mbinguni, wakamtumikia Baali.

17 Wakawapitisha watoto wao, waume na wake, motoni, wakapiga ramli, wakafanya uchawi, wakajiuza nafsi zao wapate kufanya yaliyo maovu machoni pa Bwana, hata kumkasirisha.

18 Kwa hiyo Bwana akawaghadhibikia Israeli sana, akawahamisha mbali na uso wake; wala hapana aliyesalia ila kabila ya Yuda peke yake”

Hivyo si sahihi kuchoma maiti..(kuchoma maiti ni dhambi!).. Maiti ikiungua yenyewe labda kwa ajali ya moto mpaka kufikia jivu..hapo hakuna ibada yoyote iliyohusika..majivu yake yatakwenda kuzikwa na hakuna ibada yoyote ya kiroho hapo… lakini kama ikihusisha masuala ya imani au ibada tayari ni dhambi kubwa mbele za Mungu.

Bwana akubariki.

Je umeokoka?..Au bado unaupenda ulimwengu?..kumbuka shetani yupo kasambaza kila kona upotofu wake..Na tunaishi katika siku za mwisho za kurudi Yesu Kristo. Unyakuo upo karibu sana kutokea na watakatifu watakwenda na Bwana. Je utakuwa miongoni mwao?..Hivyo tubu leo kama hujatubu na Bwana atakupokea, na kukupa Roho wake Mtakatifu.

Maran atha! jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Nyinginezo:

NINI KINATOKEA BAADA YA KIFO?

https://wingulamashahidi.org/2018/06/27/maswali-na-majibu/

Bwana alimaanisha nini kusema “waache wafu wazike wafu wao.(Mathayo 8:21)?

HERI WAFU WAFAO KATIKA BWANA

KUZIMU ni mahali pa namna gani, Je! huko wanaishi watu wakifa na kwenda kupata mateso au ni vinginevyo?

Roho za Wanyama zinakwenda wapi baada ya kifo? Je! Watafufuliwa?

Wokovu wa milele/ Ulinzi wa daima (eternal security) Je! ni neno la kimaandiko?

MKUU WA ANGA.

NGUVU ILIYOPO KATIKA MAAMUZI.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/12/19/je-kuchoma-maiti-ni-dhambi/