USIPUNGUZE MAOMBI.

by Admin | 16 June 2020 08:46 pm06

Katika Maisha usijaribu kufanya kosa la kupunguza maombi…Ni heri ukapunguza muda wa kufanya mambo mengine ambayo unaona ni ya muhimu lakini usipunguze kuomba hata kidogo!..Kama tayari ulishaanza kuwa muombaji, halafu ukaanza kupunguza unamtengenezea adui nafasi ya kufanya uharibifu mkubwa sana katika maisha yako.

Kuna siri moja Bwana aliwaambia wanafunzi wake kuhusu maombi.. alisema “KESHENI, MWOMBE, MSIJE MKAINGIA MAJARIBUNI; roho i radhi, lakini mwili ni dhaifu (Mathayo 26:41)”

Hilo Neno “msije mkaingia majaribuni” ni neno kubwa sana…Hivi unajua ni kwanini Bwana alisema “hata nywele zetu zote za kichwani zimehesabiwa (Mathayo 10:30 )?”….Ni kwasababu kuna kiumbe kingine ambacho kinatutafuta sana hata kwa vitu vidogo…na hicho si kingine zaidi ya ibilisi….wengi hawajui kuwa shetani hata baada ya kufa maiti yako bado ina thamani kwake..sasa si zaidi nywele zako?, si Zaidi mate yako?, si Zaidi vidole vyako, si Zaidi mikono yako?..naam vyote hivyo anavihitaji sana…Ndio maana biblia inasema hapo, hata nywele zetu zote zimehesabiwa (maana yake zinalindwa zisipotee hata moja wala zisitumike na adui).

Shetani akikukosa kukuua na ajali siku hiyo, atatafuta hata ujikate na kisu tu wakati unaosha vyombo, akikosa kukutoboa jicho siku hiyo atatafuta hata uchubuke tu!..akikukosa kukupatia ugonjwa fulani wa mauti kama HIV, atafanya juu chini siku hiyo angalau upate tu mafua yatakayokusumbua, na akikukosa kwenye mafua pia hataridhika atatafuta njia hata uchomwe na mwiba barabarani! Ili uumie tu!,…hivyo vile vitu vidogo unavyovidharau ambavyo unahisi shetani hawezi kujishuhulisha navyo, yeye kwake bado anavyo nafasi navyo.

Lakini mtu ukiwa mwombaji kila siku…kabla ya kulala au wakati wa asubuhi, au mchana upatapo nafasi nzuri ya utulivu…unampa shetani wakati mgumu wa kupata  nafasi katika Maisha yako. Lakini usipokuwa mwombaji matukio ya ajabu ajabu yatajifululiza katika Maisha yako ambayo hutajua hata chanzo chake ni nini?…kama ni mfanyakazi unaweza kujikuta unagombana kazini tu au unagombezwa!, au unafika huko jambo lile ambalo ulikuwa umelipanga liende vizuri halijaenda vizuri, umeamka mzima jioni unarudi ni mgonjwa wa kupindukia..na mambo kama hayo (hayo ni majaribu ya kimaisha)…sasa majaribu ya kiimani ndio hayo unajikuta umeingia katika mazingira ya kuikana Imani au kuisaliti…

Unakumbuka dakika chache baada ya Bwana Yesu kumwambia Petro na wenzake waamke wasali ili wasije wakaingia majaribuni, walipopuuzia ni nini kilifuata?…masaa kama matatu baadaye kabla hata jogoo hajawika na hata kabla ya usingizi wao kuisha waliamshwa na kikosi cha watu wenye marungu na mapanga…na moja kwa moja baadhi ya wanafunzi wakakimbia mpaka mwingine alikimbia uchi wakamwacha Bwana peke yake (hiyo tayari ni kuikana imani)..Na sio hilo tu!…Petro naye kwa kujifanya shujaa kwamba anaweza kushinda majaribu bila nguvu ya maombi, alipomfuata Bwana kule alipopelekwa yeye naye akaikana Imani, (alimkana Bwana mara tatu kwamba hamjui).

Na sisi ni hivyo hivyo, usipokuwa mwombaji…asubuhi utaamka na ujumbe wa watu wanaokutaka uwape rushwa ili jambo lako Fulani lifanikiwe….Lakini kama ukiwa mwombaji, mambo hayo Mungu anakuepusha nayo!..utaona yule ambaye angepaswa akuombe rushwa, unashangaa hata hakuombi na bado anakupa haki yako ile ile…

Ukiona umepunguza kuomba jua tayari umeanza kurudi nyuma kiimani…hiyo ni dalili ya kwanza, dalili ya pili ni kupunguza kusoma neno.

Maombi yanafananishwa na lile tukio la Nabii Musa, aliponyoosha mikono yake juu wakati wa vita…alipoionyoosha juu wana wa Israeli kule vitani walikuwa wanapata nguvu ya kuwapiga maadui zao na kuwashinda…lakini alipoishusha nguvu ziliwaondokea wana wa Israeli na kuhamia kwa adui zao na kuwashinda wana wa Israeli..Na sisi ni hivyo hivyo nguvu za Mungu zinashinda juu ya Maisha yetu dhidi ya nguvu za Adui endapo tu na sisi kila siku/kila wakati tutakuwa tumeinyanyua mikono na mioyo yetu juu kuomba…Hizo ni faida chache tu za maombi zipo nyingi hatuwezi kuwa na muda wa kuzichambua zote hapa.

Hivyo usiache kuomba kabisa!..na kumbuka ndugu kuomba sio sala ile ya kuombea chakula!..au sio ile sala la “Baba yetu”…Hiyo haitoshi…kiwango cha chini kabisa biblia imetuambia angalau lisaa limoja kwa siku, ukienda masaa 3 au 4 ni vizuri Zaidi…na pia maombi sio kwenda kuombewa na mtumishi Fulani wa Mungu au ndugu yako!!..Maombi ni wewe kama wewe kusimama mwenyewe kuomba kwa bidii!.

Kumbuka tena, shetani anashida na nywele zako, ana shida na Maisha yako na anashida na viungo vyote katika mwili wako, na sio hata kwa njia ya uchawi au kwa kuwatumia wachawi…anayo idadi kubwa ya mapepo kuliko wachawi..hivyo kazi zake nyingi anatumia mapepo yake kuzifanya hata zaidi  ya wachawi….asilimia kubwa sana ya watu wanasumbuliwa na mapepo wakidhani ni wachawi!

Hivyo ng’oa nanga leo anza safari ya maombi ya kina kila siku!..kama umerudi nyuma rudia desturi yako kabla mambo hayajazidi kuwa mabaya.

Kama hujampa Bwana Maisha yako!..hizi ni siku za mwisho, Kristo anakaribia kurudi…hivyo geuka leo mkabidhi Maisha yako naye atakusamehe.

Bwana akubariki na Bwana atubariki sote.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312



Mada Nyinginezo:

HISTORIA YA ISRAELI.

KWANINI UBATIZO NI WA MUHIMU.

MAMBO MENGINE HAYATOKI ISIPOKUWA KWA KUFUNGA.

SHETANI ANAITHAMINI HATA MAITI YAKO.

UCHAWI WA BALAAMU.

WANA JUHUDI KWA AJILI YA MUNGU, LAKINI SI KATIKA MAARIFA.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/06/16/usipunguze-maombi/