KWANINI UBATIZO NI WA MUHIMU.

KWANINI UBATIZO NI WA MUHIMU.

Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe.

Karibu tujifunze biblia na kujikumbusha mambo yale yale ambayo tumekwisha kujifunza huko nyuma kupitia sehemu mbalimbali..

Wengi wanajiuliza je ubatizo ni wa muhimu?..Jibu ni NDIO ni wa muhimu sana na si kidogo. Shetani hapendi wengi wajue siri iliyopo katika ubatizo sahihi kwasababu anajua madhara yake.

Wakati wana wa Israeli wanatoka Misri, Farao bado alikuwa anawafuatilia fuatilia..lakini walipovuka tu bahari ya shamu na majeshi ya Farao yote kuzama kwenye ile bahari ya shamu ndio ikawa mwisho wa Farao na majeshi yake kuwafuatilia wana wa Israeli.

Kutoka 14:26 “Bwana akamwambia Musa, Nyosha mkono wako juu ya bahari, ili maji yarudi tena juu ya Wamisri, juu ya magari yao, na juu ya farasi zao.

27 Musa akaunyosha mkono wake juu ya bahari, na kulipopambazuka, bahari ikarudi kwa nguvu zake; Wamisri wakakimbia mbele yake; na Bwana akawakukutia mbali hao Wamisri kati ya bahari.

28 Yale maji yakarudi yakafunikiza magari na wapanda farasi, hata jeshi lote la Farao lililoingia katika bahari nyuma yao; hakusalia hata mtu mmoja.

29 Lakini wana wa Israeli wakaenda katika nchi kavu katikati ya bahari; na hayo maji yalikuwa ni kuta upande wao wa kuume, na upande wao wa kushoto.

30 Ndivyo Bwana alivyowaokoa Israeli siku ile mikononi mwa Wamisri; Waisraeli wakawaona Wamisri ufuoni kwa bahari, wamekufa”.

Sasa siri ilikuwa ni nini mpaka Mwisho wa Farao ukawa kwenye hiyo bahari ya Shamu?..Jibu ni rahisi: Ni huo ubatizo wana wa Israeli waliobatizwa kwa kupita katikati ya bahari hiyo.

Utauliza je!..ina maana wana wa Israeli walibatizwa katika bahari ya Shamu?..Jibu ni ndio!..

1Wakorintho 10:1 “Kwa maana, ndugu zangu, sipendi mkose kufahamu ya kuwa baba zetu walikuwa wote chini ya wingu; wote wakapita kati ya bahari;

2 wote wakabatizwa wawe wa Musa katika wingu na katika bahari;”

Unaona hapo?..kitendo cha Wana wa Israeli kupitishwa katika yale maji ya Shamu, pasipo kupatikana na madhara ndiko kunakofananishwa na ubatizo. Hivyo ule ubatizo ndio uliohitimisha kazi ya shetani na majeshi yake kuwafuatilia, haijalishi kuwa tayari walishapewa ruhusu huko nyuma ya kuondoka.

Hali kadhalika, ubatizo sahihi wa maji mengi sasa unafanya kazi hiyo hiyo. Unapoingia katika yale maji na kubatizwa katika jina la Yesu na kutoka katika yale maji…wewe utatoka salama ukiwa na furaha, na amani lakini nyuma yako yale majeshi ya mapepo wabaya yaliyokuwa yanakufuatia yanakufa na maji huko nyuma.

Hivyo maji ni ishara ya wokovu kwako na maangamizi kwa shetani na majeshi yake. Ndio maana Bwana Yesu alisema katika Roho kwamba pepo amtokapo mtu hupitia mahali pasipo maji(maana yake mahali ambapo hapana maji) ili apumzike na akirudi na kukuta nyumba yake imefagiliwa anakwenda kuwachukua pepo wengine saba walio waovu kuliko yeye, na hali ya mwisho ya Yule mtu inakuwa mbaya kuliko ya kwanza.

Maana yake ni kwamba pepo likimtoka mtu na Yule mtu kama hatachukua uamuzi wa kuukamilisha wokovu wake ikiwemo kubatizwa ubatizo sahihi wa kuzama mwili mzima kulingana na maandiko na kudumu katika usafi..Mtu huyo yupo hatarini kurudiwa na zile zile nguvu za giza zilizomwacha hapo kwanza. Hivyo ubatizo sahihi ni wa muhimu sana…Na ubatizo sio dini mpya bali ni maagizo ya  Bwana wetu Yesu…na kwa faida yetu kama ilivyokuwa kwa faida kwa wana wa Israeli wakati wanatoka Misri, kama sio yale maji Farao angeendelea kuwafuatilia daima.

Shetani na mapepo yake yataendelea kumfuata Yule mtu ambaye hajakamilisha wokovu wake…Na Bwana alishatuambia katika Neno lake, kwamba “aaminiye na kubatizwa ataokoka”..maana yake mambo hayo mawili yanakwenda pamoja, hayaachani, vinginevyo ni ngumu sana kuokoka na mkono wa Adui.

Kama unakumbuka kile kisa cha Yule mtu aliyekuwa na mapepo yaliyojitambulisha kama JESHI. Mtu Yule aliingiwa na mapepo, na mapepo yale yalipomtoka yaliwaingia nguruwe…Jinsi wale Nguruwe walivyokwenda kuangamia majini ni mfano wa Farao na majeshi yake yalivyozama majini…Kwahiyo unaweza kuona kuna uhusiano mkubwa sana wa maji na majeshi ya Adui. Hivyo ubatizo ni wa muhimu sana. Pale tu mtu anapoamini na kutubu anapaswa akabatizwe bila kuchelewa…

Itakuwa ni jambo la kushangaza, mtu utasema umeokoka, halafu miezi inapita, miaka inapita, bado hujabatizwa, unaishi kwa kanuni ipi ya wokovu?

Bwana akubariki sana.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

MUNGU KUSEMA NA WEWE PEKEE, HAITOSHI KUKUPA USHINDI.

JINA LA MUNGU NI LIPI?

KUTAKUWA NA MATETEMEKO YA NCHI, NJAA NA TAUNI.

USITUPE LULU ZAKO MBELE YA NGURUWE.

KUOTA MAFURIKO,KUOTA MAJI MENGI,KUOTA MAWIMBI.

HISTORIA YA WILLIAM BRANHAM

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments