UFANYE NINI KAMA MKRISTO WAKATI HUU WA JANGA LA CORONA?

UFANYE NINI KAMA MKRISTO WAKATI HUU WA JANGA LA CORONA?

Watu baadhi kutoka nchi mbalimbali wamenitumia ujumbe wanasema, mtumishi huku kwetu hali sio nzuri hatuwezi kwenda kanisani kama tulivyozoea, hatuwezi kufanya chochote isipokuwa tu ni kukaa nyumbani, na wala hakuna dalali ya jambo hilo kuisha hivi karibuni…Tufanye nini?

Shalom, ndugu,

Ipo Habari moja katika biblia tunapaswa tujue na  tujifunze kama wakristo katika wakati huu ambao dunia ipo katika taharuki kubwa, Tukisoma kitabu cha matendo ya Mitume, kuna wakati ambapo mitume wa Bwana walipitia kipindi fulani cha ukimya mkubwa sana, jambo ambalo liliwapasa wasifanye kitu kingine Zaidi ya kwenda kujifungia gorofani. Kwanini walilazimika kuwa vile, ni kwasababu ni kipindi ambacho, Sio  YESU tu peke yake ambaye walizoea kumwona na kutembea naye kila siku hakuwa nao, bali pia Roho Mtakatifu ambaye walisikia habari zake alikuwa bado hajashuka juu yao.. walikuwa katikati ya pengo, kama vile mayatima fulani..

Kitu pekee kilichowafanya wawezi kukivuka hicho kipindi kifupi cha ukimya, ilikuwa ni ile AHADI TU, waliopewa na Bwana Yesu siku ile aliyokuwa anapaa..

Hiyo ndio iliyokuwa salama yao kwa wakati huo waliokuwa wanapitia..Kumbuka hawakujua ahadi hiyo itatimia lini, lakini maaadamu wana Neno la Ahadi, basi hiyo iliwafanya wapate nguvu siku baada ya siku, wavumilie hicho kipindi cha mpito mbele yao wakitumai kuwa siku si nyingi itatimia, na AHADI yenyewe ilikuwa ni kungojea YERUSALEMU, mpaka wakatakapopokea kipawa cha Roho Mtakatifu..Basi.

Matendo 1:3 “wale aliowadhihirishia nafsi yake, kwa dalili nyingi, baada ya kuteswa kwake, ya kwamba yu hai, akiwatokea muda wa siku arobaini, na kuyanena mambo yaliyouhusu ufalme wa Mungu.

4  Hata alipokuwa amekutana nao aliwaagiza wasitoke Yerusalemu, bali waingoje ahadi ya Baba, ambayo mlisikia habari zake kwangu;

5  ya kwamba Yohana alibatiza kwa maji, bali ninyi mtabatizwa katika Roho Mtakatifu baada ya siku hizi chache”.

Hivyo baada ya ile siku ya 40, hawakumwona, wala hawakusikia chochote, wala hawakuoona uwepo wowote, wala hawakuwa na shughuli nyingine yoyote ya kuhubiri, au kushuhudia kama pale mwanzo, au kuzunguka huku na huko kuhubiri..Bali iliwagharimu kwenda kukaa tu sehemu moja..na zaidi ya yote biblia inasema nje kulikuwa na hofu ya wayahudi.

Lakini biblia inatuonyesha ahadi hiyo haikuchelewa, bali ndani ya siku 10 mbeleni ilitimia, ambayo ndio iliyokuwa siku ya Pentekoste, Roho Mtakatifu aliwashukia mitume wake kwa nguvu ya ajabu, na hapo ndipo Mungu akaleta uamsho mwingine tena ambao uliitikisa dunia nzima katika historia..

Sasa swali ni Je ndani ya kipindi kile cha mpito ambacho hakukuwa na sapoti yoyote ya kimbinguni mitume walikuwa wanafanya nini ndani, Je! walikuwa wamelala tu au wameacha wakovu wao sasa wafikirie mambo yao ya kale, au walikuwa wamekaa wanapiga tu story na kuzungumzia Maisha ya wengine, au wanaangalia movie, au wanachat whatasapp kila wakati au wanacheza magemu, au wanafanya nini??

Embu Tusome..

Matendo 1:10  “Walipokuwa wakikaza macho mbinguni, yeye alipokuwa akienda zake, tazama, watu wawili wakasimama karibu nao, wenye nguo nyeupe,

11  wakasema, Enyi watu wa Galilaya, mbona mmesimama mkitazama mbinguni? Huyu Yesu aliyechukuliwa kutoka kwenu kwenda juu mbinguni, atakuja jinsi iyo hiyo mlivyomwona akienda zake mbinguni.

12  Kisha wakarudi kwenda Yerusalemu kutoka mlima ulioitwa wa Mizeituni, ulio karibu na Yerusalemu, wapata mwendo wa sabato.

13  Hata walipoingia, wakapanda orofani, walipokuwa wakikaa; Petro, na Yohana, na Yakobo, na Andrea, Filipo na Tomaso, Bartholomayo na Mathayo, Yakobo wa Alfayo, na Simoni Zelote, na Yuda wa Yakobo.

 14  Hawa wote walikuwa wakidumu kwa moyo mmoja KATIKA KUSALI, pamoja nao wanawake, na Mariamu mama yake Yesu, na ndugu zake”.

Unaona, biblia inasema hapo walikuwa WAKIDUMU KWA MOYO MMOJA KATIKA KUSALI,..

Ndugu, wakati huu wa LOCKDOWN, na kuwa karantini kutokana na janga la Corona, nchi yoyote uliyopo. Wakati huu Wa kuzuiwa kufanya ibada, au kuzunguka huku na huko, wa kuzuiwa kwenda mtaani kuhubiri kama ulivyokuwa unafanya  hapo mwanzoni, wa kuzuiwa kuitishi mikutano ya injili, wa kuzuiwa kwenda kumwabudu Mungu kanisani, kwenda kwenye masomo ya biblia, kila baada ya siku mbili, sio wakati wako wa wewe kuwa na kisingizio cha kuacha kumtafuta Mungu, na kurudi nyuma kwenye ulimwengu ulipokuwepo, wa kurudi kuanza sasa kutokusoma biblia yako,..bali huu ndio unapaswa uufanye muda wakati wako wa kudumu katika KUSALI kwa bidii ukiingalia ahadi ya Mungu iliyo mbele yako, kwamba hivi karibuni atakwenda tena kutuachilia, lakini hatatuachilia hivi hivi, bali atatuachilia na UAMSHO MKUBWA WA ROHO ambao haujawahi kutokea..kama ilivyokuwa katika kipindi cha Pentekoste.

Hivyo huu sio wakati wa kuzimia mioyo,  wala sio wakati wa kuogopa maadamu tupo ndani ya Kristo, badala yake ndio tuongeze kutazama juu, tukiziangalia Ahadi za Bwana ndani ya kipindi hichi cha mpito, tukiongeza viwango vyetu vya kujisomea biblia nyumbani, na kusali sana tena Zaidi ya pale tulipokuwa mwanzoni, ikiwezekana kufunga, na kila wakati kumtafakari Mungu kweli kweli..

Sisi hatujapitia kipindi cha kuachwa na mbinguni kwa Muda kwa ilivyokuwa kwa mitume, lakini wao hawakuiacha Imani, badala yake walidumu katika kusali tena walipanda OROFANI, juu kabisa mahali ambapo hapana  usumbufu wa watu kuingia na kutoka, ili wamtuafakari Mungu vizuri na kusali..

Vivyo hivyo huu ni wakati wa wewe, kupanda OROFANI (mahali penye utulivu), Umtafute Mungu peke yako, kwasababu UAMSHO MKUU SANA, Unakwenda kuzuka duniani kote hivi karibuni. Kipindi cha nyuma pengine ulikuwa na visingizio vya kutokusali, kwamba upo bize kutafuta riziki na shughuli leo hii mazingira yanakulazimisha kukaa nyumbani, na tena kuna agizo limetolewa la kuomba, hivyo isiwe sababu ya wewe kuhukumiwa siku ile kwa kutokuomba sasahivi…Unayo sababu inayoeleweka kidunia ya wewe kutozurura zurura mtaani, basi kaa nyumbani kuomba…utajitetea vipi siku ile??..Utasema ulikosa muda? Utasema serikali ilikuzuia kuomba? Leo hii imekutangazia wewe kuomba?.. Utasema sikuomba kwasababu mazingira yalikuwa hayaruhusu?..jibu unalo.

Hivyo nakutia moyo wewe mkristo ambaye umeathiriwa na hali hii ya sasa duniani, Fahamu kuwa ni kipindi kifupi tu cha Siku 10 rohoni kinapita ambacho ni Mungu mwenyewe kakiruhusu..hivyo kuwa na akili, kujua nyakati na majira, ongeza viwango vyako vya utakatifu kama vile hukuwahi kuishi hivyo hapo kabla, ni wakati wa kutubu (kutubu maana yake ni kuacha yale uliyokuwa unayafanya yasiyo mpendeza Mungu) ili hiyo  PENTEKOSTE itakapokuja kwa watu wa Mungu duniani, uwe na wewe ni mmojawapo..

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

JINSI ROHO MTAKATIFU ANAVYOWAFUNULIA WATU MAANDIKO.

USIISHIE KUTAZAMA JUU, ENDELEA MBELE.

KWARESMA IPO KIMAANDIKO?

SIKU YA UNYAKUO ITAKUKUTAJE?

TAHADHARI YA NEEMA YA MUNGU.

YA KALE YAMEPITA, TAZAMA YAMEKUWA MAPYA

NAO WALIOKUWA WAMEKUSUDIWA UZIMA WA MILELE WAKAAMINI.

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
2 Comments
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Shaban Were
Shaban Were
4 years ago

Ahsante kwa ujumbe mzuri., naomba mafundisho kutoka kwenu.
Through whatsApp +254 712726420