MALAKI, NABII WA MWISHO KATIKA ISRAELI.

by Admin | 10 July 2020 08:46 pm07

Nabii Malaki alikuwa ni nabii kama walivyo manabii wengine katika biblia kama nabii Yeremia, nabii Isaya, nabii Samweli, Nabii Danieli..Biblia haijaeleza maisha yake kama ilivyoelezea kwa baadhi ya manabii wengine kama Samweli, Yeremia na Danieli. Nabii Malaki ni nabii ambaye maisha yake hayapatikani katika vitabu vingine vya biblia. Na ndiye nabii wa mwisho aliyeandika kitabu cha mwisho katika agano la kale. Kitabu cha Malaki kiliandikwa kati ya mwaka 441-400KB. Na kina Sura nne tu, lakini zilizoshiba Jumbe nzito.

Sasa tunaposema ni nabii wa mwisho haimaanishi kwamba hawakutokea manabii wengine baada yake..la!..walitokea wengine waliotumwa na Mungu, katikati ya hicho kipindi cha miaka 400 lakini Bwana Mungu hakuruhusu jumbe zao ziwe miongoni mwa orodha ya vitabu hivyo vya agano la kale. Na kama havijaruhusiwa kuwekwa kwenye orodha na Roho Mtakatifu mwenyewe hatupaswi sisi kuvitafuta na kuvipachika, wala hatupaswi kutafuta majina ya hao manabii ni wakina nani..Tukifanya hivyo tutafungua mlango wa roho ya Ibilisi kutupotosha…Roho Mtakatifu alikuwa na maana yake kubwa kuzuia visiwekwe kwenye orodha.

Hivyo kitabu cha Malaki ndio kitabu cha mwisho katika vitabu vya agano la kale, vingine vinavyochomekwa sasa ni batili.

kitabu cha malaki

kitabu cha malaki

Sasa tukirudi kwa huyu Nabii Malaki,  ndiye Nabii pekee aliyepewa ufunuo wa kurudi kwa Roho ya Eliya duniani tena….hakuna Nabii mwingine yeyote aliyefunuliwa ufunuo huo zaidi yake yeye,

Malaki 4:5 “Angalieni, nitawapelekea Eliya nabii, kabla haijaja siku ile ya Bwana, iliyo kuu na kuogofya.

6 Naye ataigeuza mioyo ya baba iwaelekee watoto wao, na mioyo ya watoto iwaelekee baba zao, ili nisije nikaipiga dunia kwa laana”.

Na unabii huo wa Ujio wa Eliya, ulikuja kutimia kwa  Yohana Mbatizaji kwa sehemu ya kwanza na kwa sehemu ya pili ulikuja kutimia kwa Mjumbe wa kanisa la mwisho la Laodikia (William Branham)

Mathayo 17:10 “Wanafunzi wake wakamwuliza, wakisema, Basi kwa nini waandishi hunena ya kwamba imempasa Eliya kuja kwanza?

11 Naye akajibu, akawaambia, Kweli Eliya yuaja kwanza, naye atatengeneza yote,

12 ila nawaambia, ya kwamba Eliya amekwisha kuja, wasimtambue, lakini wakamtenda yote waliyotaka. Vivyo hivyo Mwana wa Adamu naye yuaenda kuteswa kwao.

13 Ndipo wale wanafunzi walipofahamu ya kuwa amesema nao habari za Yohana Mbatizaji”.

Nabii Malaki pia kwa ufunuo wa Roho ndiye nabii aliyezungumzia ZAKA kwa kina, Bwana alimfunulia kuwa wote wanaokwepa kulipa zaka, ni kama wezi mbele zake.

Malaki 3:8 “Je! Mwanadamu atamwibia Mungu? Lakini ninyi mnaniibia mimi. Lakini ninyi mwasema, Tumekuibia kwa namna gani? Mmeniibia zaka na dhabihu.

9 Ninyi mmelaaniwa kwa laana; maana mnaniibia mimi, naam, taifa hili lote.

10 Leteni zaka kamili ghalani, ili kiwemo chakula katika nyumba yangu, mkanijaribu kwa njia hiyo, asema Bwana wa majeshi; mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha, au la”.

Nabii Malaki ndiye nabii pekee ambaye alifunuliwa hisia za Mungu kipekee sana tofauti na manabii wengine…Mungu alimfunulia ni vitu gani vinavyomchosha yeye kutoka kwa wanadamu, na vitu vinavyomchukiza ambavyo wengi hawajui kama vinamchukiza Mungu. Kwamfano suala la kuachana, wengi hawajui kwamba linamchukiza Mungu kwa kiwango kikubwa sana…

Malaki 2:16 “Maana mimi nakuchukia kuachana, asema Bwana, Mungu wa Israeli; naye aifunikizaye nguo yake kwa udhalimu namchukia, asema Bwana wa majeshi; basi jihadharini roho zenu, msije mkatenda kwa hiana”.

Na pia kuna mambo tuyafanyayo yanayomchosha Mungu wetu pasipo sisi kujua..

Malaki 2:17 “Mmemchokesha Bwana kwa maneno yenu. Lakini ninyi mwasema, Tumemchokesha kwa maneno gani? Kwa kuwa mwasema, Kila atendaye mabaya ni mwema machoni pa Bwana, naye huwafurahia watu hao, au, Mungu mwenye kuhukumu yuko wapi?”

Na pia Nabii Malaki alionyeshwa kuwa kuna maneno tuyazungumzayo ambayo ni magumu kwa Mungu wetu, ambayo hatupaswi kuyasema…

Malaki 3:13 “Maneno yenu yamekuwa magumu juu yangu, asema Bwana. Lakini ninyi mwasema, Tumesema maneno juu yako kwa namna gani?

14 Mmesema, Kumtumikia Mungu hakuna faida; na, Tumepata faida gani kwa kuyashika maagizo yake, na kwa kwenda kwa huzuni mbele za Bwana wa majeshi?

15 Na sasa twasema ya kwamba wenye kiburi ndio walio heri; naam, watendao uovu ndio wajengwao; naam, wamjaribuo Mungu ndio waponywao.

16 Ndipo wale waliomcha Bwana waliposemezana wao kwa wao. Naye Bwana akasikiliza, akasikia; na kitabu cha ukumbusho kikaandikwa mbele zake, kwa ajili ya hao waliomcha Bwana, na kulitafakari jina lake.

17 Nao watakuwa wangu, asema Bwana wa majeshi, katika siku ile niifanyayo; naam, watakuwa hazina yangu hasa; nami nitawaachilia, kama vile mtu amwachiliavyo mwanawe mwenyewe amtumikiaye”.

Hivyo Neno la Mungu ni taa..kuna mambo mengi ya kujifunza katika kitabu cha Malaki, hayo ni baadhi tu machache…lakini kila mmoja wetu akitenga muda kukisoma, huku akimruhusu Roho Mtakatifu awe mwalimu wake, yapo makubwa ya kunufaika na ya kulinufaisha kanisa la Kristo, Bwana atusaidie katika kulisoma Neno lake na kulitendea kazi.

Malaki 1

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

UTASIMAMA PEKE YAKO SIKU ILE.

JE! ULEVI NI DHAMBI?.

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 7 (Yeremia na Maombolezo)

Biblia ni nini?

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/07/10/malaki-nabii-wa-mwisho-katika-israeli/