Nyamafu ni nini?

by Admin | 6 September 2020 08:46 pm09

JIBU: Nyamafu ni nyama ya mnyama aliyekufa (kibudu) bila kuuliwa kwa asili (yaani kuchinjwa). Mungu aliwakataza wana wa Israeli katika agano la kale wasile nyama ya mnyama yoyote aliyekufa bila kuchinjwa..

Walawi 17: 15 “Tena kila mtu atakayekula NYAMAFU, au nyama aliyeraruliwa na wanyama, kama ni mzalia, kama ni mgeni, atafua nguo zake, na kuoga majini, naye atakuwa najisi hata jioni; ndipo atakapokuwa safi.

16 Lakini kwamba hazifui, wala haogi mwili, ndipo atakapochukua uovu wake”.

Mistari mingine ya biblia inayozungumzia maagizo kama hayo ni kama ifuatavyo (Kumbukumbu 14:21, Walawi 22:8, Ezekieli 4:14, Ezekieli 44:31)..Unaweza ukaipitia binafsi upatapo muda.

Lakini Mungu aliwakataza wasile nyamafu kwasababu ni nyama ambayo ina damu ndani yake..

Utauliza kwani kuna nyama isiyo na damu na ambayo ina damu?

Jibu ni ndio!..Ipo tofauti kati ya nyama ya mnyama aliyechinjwa na damu yake kutoka na ile ya Mnyama ambaye hajachinjwa na wala damu yake haijatoka..wanjichaji wanajua zaidi. Sasa sio kwamba nyama ya mnyama aliyechinjwa itakosa damu kabisa, itakuwa na damu lakini sio kiwango cha kama ile ambayo haijachinjwa.

Sasa Bwana Mungu aliwakataza wana wa Israeli wasile nyama na damu yake, ndio maana akawapa maagizo ya kuwachinja Wanyama na damu yao waimwage juu ya nchi..

Mwanzo 9: 3 “Kila kiendacho kilicho hai kitakuwa chakula chenu, kama nilivyowapa mboga za majani, kadhalika nawapeni hivi vyote. 4 Bali nyama pamoja na uhai, yaani, damu yake, msile”

Ezekieli 33:25 “Basi, waambie, Bwana MUNGU asema hivi; MNAKULA NYAMA PAMOJA NA DAMU YAKE, na kuviinulia vinyago vyenu macho yenu, na kumwaga damu; je, mtaimiliki nchi hii”

Na pia sio usafi kumla mnyama ambaye kafa mwenyewe!.. hata katika hali ya kawaida Mwili unakataa wenyewe! Hata hamu haipo!, hiyo ni kuonyesha kwamba sio kitu cha kufaa kula, kwasababu hujui mnyama kafaje kafaje, pengine kwa kula sumu au.

Hivyo hiyo ndio maana ya nyamafu (Ni nyama ya mnyama aliyejifia mwenyewe bila kuchinjwa).

Lakini katika kumnjicha mnyama ni kitu gani cha rohoni tunajifunza?

Ilikuwa ili mwili wa Bwana wetu Yesu Kristo uweze kukubalika na kuleta matokeo makubwa ya ukombozi, ilipaswa naye pia auawe, na damu yake imwagike!, ndipo ilete uhai kwetu sisi.. Hivyo mwili wa Kristo ni chakula cha ulimwengu, ambaye ni mfano wa kondoo aliyechinjwa na kuandaliwa vyema na si nyamafu. Kwa kupigwa kwake sisi tumepona.

Yohana 6:31 “Baba zetu waliila mana jangwani kama vile ilivyoandikwa, Aliwapa chakula cha mbinguni ili wale.

32 Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Siye Musa aliyewapa chakula kile cha mbinguni, bali Baba yangu anawapa ninyi chakula cha kweli kitokacho mbinguni

33 Kwa maana chakula cha Mungu ni kile kishukacho kutoka mbinguni na kuupa ulimwengu uzima.

34 Basi wakamwambia, Bwana, sikuzote utupe chakula hiki.

35 Yesu akawaambia, Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe.”

Je na wewe leo umekipata hichi chakula halali kilichoshushwa kutoka mbinguni? Au unakula nyamafu?..Nyamafu ni kitu chochote ambacho hakikufa kwa kumwaga damu yake kwa ajili yako, hakijachinjwa kwaajili yako.

Kuutumainia ulimwengu ni kujilisha nyamafu, kuzitumainia fedha zako, au umaarufu wako, au kumtumainia mwanadamu yoyote ambaye hajui hata mapigo ya moyo wako yanadundaje ni kujilisha nyamafu na hivyo ni machukizo kwa Mungu.

Mtegemee Yesu, Mwamini Yesu, HUYO PEKE YAKE NDIYE CHAKULA KILICHOSHUSHWA KUTOKA MBINGUNI, Mwanakondoo halisi aliyechinjwa Kalvari kwaajili yetu, (na si kibudu), huyo pekee ndiye anayeweza kutupa uzima.

Kama hujampokea, Leo anakuita, unachotakiwa kufanya ni kukiri tu wewe ni mwenye dhambi, hicho tu! (Anahitaji rehema na si sadaka)..ndicho anachokitafuta kutoka kwetu..Baada ya kukiri na kukubali, basi unaomba msaada kutoka kwake, kwamba akurehemu na kukusaidia, na ukiisha kumwomba rehema..thibitisha ulichokiomba kwa kuyaacha mabaya yote uliyokuwa unayafanya yasiyompendeza yeye..kama ulikuwa mlevi, mwizi, mzinzi n.k yaache yote.

Na yeye ni mwaminifu, kwasababu kabla hata hujamaliza kusema Amen, katika sala yako hiyo ya toba tayari atakuwa ameshakusamehe na kuingia moyoni mwako, kwasababu anakupenda upeo, na anatupenda wote. Na atakupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu ambaye atakusaidia kukuongoza katika kuijua kweli yote ya biblia. Pia unahitaji kubatizwa katika ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi na kwa jina la Yesu Kristo sawasawa na Matendo 2:38, Kama utakuwa tayari kufanya hivyo, basi wasiliana na sisi Inbox, tutakuongoza ni wapi utabatiziwa.

Usikubali kula au kulishwa nyamafu wakati chakula halisi kipo!

Bwana atubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255693036618/ +255 789001312

Mada Nyinginezo:

MWILI NA DAMU YA YESU KRISTO.

Herode aliliwa na chango, Je, chango ni nini kibiblia?

Kula uzao wa tumbo lako maana yake nini? (Kumbukumbu 28:53)

UFUNUO: Mlango wa 19

Huyu Azazeli ni nani tunayemsoma katika(Walawi 16:8)

Kwanini Bwana aliwalenga mbwa na nguruwe tu katika Mathayo 7:6?

Bumbuazi la moyo ni nini?(Kumbukumbu 28:28)

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/09/06/nyamafu-ni-nini/