Sikukuu ya kutabaruku ni ipi?

by Admin | 7 November 2020 08:46 am11

Jibu: Kuna tofauti ya Neno “kutakabari” na “kutabaruku”. Kutakabari ni “kuwa ni majivuno yanayotokana na kiburi” unaweza kusoma kusoma kwa urefu hapa >> KUTAKABARI

Lakini “kutabaruku” ambako ndiko tunakokwenda kukuzungumzia leo, maana yake ni “KUWEKA WAKFU”.

Sasa sikuku ya kutabaruku maana yake ni “Sikukuu ya kuweka wakfu”. Sikukuu hii ilianza kusheherekewa na Wayahudi (yaani waisraeli), miaka kadhaa baada ya Nabii wa mwisho katika biblia kutokea (yaani Nabii Malaki).

Sikukuu hii haikuwa miongoni mwa zile sikukuu 7 ambazo Musa aliagizwa na Mungu awape wana wa Israeli. Hivyo sherehe hii ilikuja kutengenezwa na baadhi ya wayahudi wachache kama ukumbusho wa kilichotokea katika Hekalu lao.

Sikukuu hii iliidhinishwa na Myahudi mmoja aliyeitwa Yuda Makabayo, pamoja na wazee wengine wa Israeli  wachache, kipindi ambacho Mtawala Antiokia IV Epifane, alipozuka na kushuka Yerusalemu na kulitia unajisi Hekalu la Mungu, kama unabii unavyosema katika Danieli 8:9 (Ile Pembe ndogo).

Mtawala huyu aliwalazimisha wayahudi wote wasiabudu katika Nyumba ya Mungu, na badala yake kuwalazimisha kufuata desturi za kipagani,

Sasa ndipo wakatokea wayahudi hao wachache (Yuda Makabayo pamoja na wenzake) wakaingia porini kupambana naye na kumwondosha, na hatimaye KULIWEKA TENA WAKFU HEKALU ambalo alilichafua, huyu Antiokia IV Epifane. Na tangu muda huo wakaifanya hiyo tarehe, kuwa ni tarehe ya kuadhimishwa kwa jinsi Mungu alivyowafungulia mlango wa kurejeshwa kwa Ibada takatifu za Nyumba ya Mungu. Kwa urefu kuhusu Mtawala huyu pamoja na Yuda Makabayo fungua hapa >> Danieli Mlango wa 8

Sikukuu hii haina tofauti na ile ya akina Mordekai (Sikukuu ya Purimu). Ambayo Mordekai na Esta waliitengeneza kama kumbukumbu ya mambo Mungu aliyowafanyia, baada ya kuwaokoa na mkono wa Hamani, adui yao.

Esta 9: 27 “Wayahudi wakaagiza na kutadariki juu yao wenyewe, na juu ya wazao wao, na juu ya wote watakaojiunga nao, isikome, ya kwamba watazishika siku hizo mbili sawasawa na andiko lile, na kwa majira yake kila mwaka;

28 siku hizo zikumbukwe na kushikwa kwa vizazi vyote na kila jamaa, katika kila jimbo na kila mji; wala siku hizo za Purimu zisikome katikati ya Wayahudi, wala kumbukumbu lake lisiishe kwa wazao wao”

Sikukuu hii ya kutabaruku na hiyo ya Akina Mordekai zote hazikuwepo miongoni mwa sikukuu Bwana alizowaagiza kwa mkono wa Musa..Ni sikukuu zilizotengenezwa baada ya Mungu kuwafanyia mema watu wake, hivyo na wao wakazingeneza kama kurudisha shukrani kwa Mungu wao.

Ni jambo gani tunajifunza katika sikukuu hii ya kutabaruku?

Chochote tunachomfanyia Mungu, anakiheshimu.. Daudi alifikiria kumjengea Mungu nyumba, ingawa alijua kabisa Mungu hakai kwenye nyumba zilizotengenezwa na mikono ya wanadamu, lakini Mungu alimheshimu kwa mawazo yake hayo, na wala hakuidharau ile nyumba, zaidi ya yote aliitukuza sana kwa mwanawe Sulemani.

Vivyo hivyo hawa wakina Yuda Makabayo na wenzake, ambao walipenda kuadhimisha siku ya Nyumba ya Mungu kuwekwa tena wakfu, huku wakimshukuru kwa kumfanyia Ibada, Mungu aliiheshimu sikukuu yao hiyo..Ndio maana ilidumu mpaka wakati wa Bwana Yesu.

Yohana 10:22  “Basi huko Yerusalemu ilikuwa SIKUKUU YA KUTABARUKU; ni wakati wa baridi.

23  Naye Yesu alikuwa akitembea hekaluni, katika ukumbi wa Sulemani”.

Je umeokoka?..Kama bado unangoja nini?..kipindi si kirefu parapanda ya mwisho italia, na watakatifu ambao unadhani hawapo leo duniani, wataondolewa duniani…Na utakuwa umepoteza nafsi yako milele.. Hujui dakika tano mbele nini kitatokea..ukifa leo au parapanda ikilia leo utakuwa wapi?..kumbuka kuzimu ipo, na biblia inasema haishibi watu.. Mpokee leo Kristo kama bado hujafanya hivyo…

Kama upo tayari kutubu leo na kuanza safari mpya ya wokovu basi fungua hapa >> SALA YA TOBA

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

SIKUKUU 7 ZA KIYAHUDI ZINAFUNUA NINI KWETU?

SIKUKUU YA VIBANDA.

PASAKA NI NINI? NA JE TUNARUHUSIWA KUSHEHEREKEA PASAKA?

JE WAKRISTO TUNARUHUSIWA KUSHEHEREKEA VALENTINE’S DAY?

JE NI LAZIMA MKRISTO AOE/AOLEWE?

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/11/07/sikukuu-ya-kutabaruku-ni-ipi/