Nguo za magunia katika biblia ni zipi?

by Admin | 18 November 2020 08:46 am11

Nguo za magunia( au mavazi ya magunia) ndiyo mavazi ya namna gani ?

Magunia kama biblia inavyotafsiri ni tofauti na inavyotafsiriwa sasa, Leo hii ukizungumzia magunia unamaanisha labda mifuko aina ya Salfeti (Sulphate) ambayo yanatumika sana sana katika kuhifadhia nafaka, au utakuwa unazungumiza magunia yaliyoshonwa kwa nyuzi za katani.

Lakini mavazi ya magunia, biblia haiyatafsiri kama mavazi yaliyotengenezwa kwa mojawapo ya malighafi hizo (salfeti au nyuzi za katani). Bali mavazi ya magunia yaliyozungumziwa kwenye biblia ni mavazi yaliyotengenezwa kwa MANYOYA YA MBUZI.

Nguo hizo zilitengenezwa mahususi, kuashiria aidha vitu hivi viwili Maombolezo au Toba

   1. Maombolezo.

Watu zamani za biblia waliopitia misiba, au majanga walikuwa wanavaa nguo hizo za magunia kuonyesha hali ya maombolezo, kuonyeshwa kuguswa na tatizo hilo, na kwamba wapo katika huzuni na si furaha..

Mfano wa hao ni Rispa aliyeomboleza baada ya kufiwa na wanawe.

2Wafalme 21:10 “Naye Rispa, binti Aya, akatwaa nguo ya magunia akajitandikia mwambani, tangu mwanzo wa mavuno hata waliponyeshewa mvua toka mbinguni; wala hakuacha ndege wa angani kukaa juu yao mchana, wala wanyama wa mwitu usiku”

Tunaona mfano mwingine ni wana wa Israeli, baada ya kupata msiba wa kupelekwa utumwani..biblia inasema iliwapasa wavae mavazi ya magunia kwa maombolezo..

Yeremia 4: 8 “Kwa sababu hiyo jifungeni NGUO ZA MAGUNIA; ombolezeni na kulia kwa uchungu; kwa maana hasira kali ya Bwana haikugeuka na kutuacha”

Yeremia 6:26 “Ee binti wa watu wangu, ujivike NGUO YA MAGUNIA, na kugaagaa katika majivu; fanya maombolezo, kama maombolezo kwa ajili ya mwana wa pekee, maombolezo ya uchungu mwingi; maana mwenye kuteka nyara atakuja juu yetu ghafula”.

Mifano mingine watu waliovaa mavazi ya magunia, kuashiria maombolezo unaweza kuisoma katika mistari ifuatayo (2Wafalme 6:30, 2Wafalme 19:1)

        2. Toba

Watu pia walipotaka kujisongeza mbele za Mungu, kwa toba..walivaa nguo za magunia, kuashiria hali ya unyenyekevu, na kujishusha, kwamba wao si kitu mbele ya Mungu mkuu, na hivyo kutaka rehema kutoka kwake. Mfano wa watu hao ni nabii Danieli.

Danieli 9:3 “Nikamwelekezea Bwana Mungu uso wangu, ili kutaka kwa maombi, na dua, pamoja na kufunga, na KUVAA NGUO ZA MAGUNIA na majivu.

4 Nikamwomba Bwana, Mungu wangu, nikaungama, nikasema, Ee Bwana, Mungu mkuu, mwenye kutisha, ashikaye maagano na rehema kwao wampendao, na kuzishika amri zake”

Na mfano mwingine ni watu wa Ninawi..

Yona 3: 5 “Basi watu wa Ninawi wakamsadiki Mungu; wakatangaza kufunga, WAKAJIVIKA NGUO ZA MAGUNIA, tangu yeye aliye mkubwa hata aliye mdogo.

6 Habari ikamfikia mfalme wa Ninawi, naye akaondoka katika kiti chake cha enzi, AKAVUA VAZI LAKE, AKAJIVIKA NGUO ZA MAGUNIA, na kuketi katika majivu”

Na wengine mfano wa hao, unaweza kuwasoma katika mistari ifuatayo (2Wafalme 19:1, Nehemia 9:1).

Je wakristo sasa Nasi pia tunapaswa kuvaa mavazi ya magunia pindi tunapotubu kwa Mungu wetu au tunapomboleza pindi tunapopitia na misiba?.

Huo ni uchaguzi wa mtu avae au asivae. Lakini biblia haijatoa amri kwamba lazima mtu avae magunia anapotubu.. Ilichotia msisitizo ni hichi..

Yoeli 2:12 “Lakini hata sasa, asema Bwana, nirudieni mimi kwa mioyo yenu yote, na kwa kufunga, na kwa kulia, na kwa kuombolea;

13 RARUENI MIOYO YENU, WALA SI MAVAZI YENU, MKAMRUDIE BWANA, Mungu wenu; kwa maana yeye ndiye mwenye neema, amejaa huruma; si mwepesi wa hasira, ni mwingi wa rehema, naye hughairi mabaya”

Hapo inasema turarue mioyo yetu na si mavazi yetu…Kumbuka mavazi yanayozungumziwa hapo ndio hayo ya magunia, na si vile vimini, au mavazi yasiyo ya heshima yanayovaliwa na wadada. Hayo mtu anapookoka hapaswi kabisa kuendelea kuyavaa.

Je umeurarua moyo wako kwa Bwana? Kama bado Ni vyema ukafanya hivyo mapema

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

MAVAZI YA NDANI NA YA NJE.

MAVAZI YAPASAYO.

JE KUVAA PETE NI DHAMBI?

MWANAMKE ULIYEKOMAA KI-UMRI, ITAMBUE HUDUMA YAKO.

JE! UNAYATUNZA MAVAZI YAKO?

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/11/18/nguo-za-magunia-katika-biblia-ni-zipi/