Ni kweli Waliolala Katika Kristo Wamepotea?(1Wakor 15:18)

by Admin | 25 March 2021 08:46 am03

SWALI: Bwana Yesu Asifiwe Naombeni Ufafanuzi Je Maneno Haya Yana Maana Gani

1wakoritho15:18-19 “na Hapo Wao Nao Waliolala Katika Kristo Wamepotea , 19 “kama Katika Maisha Haya Tu Tumemtumaini Kristo, Sisi Tu Maskini Kuliko Watu Wote”


JIBU: Ni rahisi, kudhani mistari hiyo inathibitisha kuwa wale waliokufa katika Yesu Kristo wamepotea katika uwongo wa kiimani. Lakini mistari hiyo haimaanishi hivyo, ukianzia vifungu vya juu, na ukiendelea mpaka vile vya chini utalithibitisha hilo. Tusome..

1Wakorintho 15:12 “Basi, ikiwa Kristo anahubiriwa ya kwamba amefufuka katika wafu, mbona baadhi yenu husema kwamba hakuna kiyama ya wafu?

13 Lakini kama hakuna kiyama ya wafu, Kristo naye hakufufuka;

14 tena kama Kristo hakufufuka, basi, kuhubiri kwetu ni bure na imani yenu ni bure.

15 Naam, na sisi tumeonekana kuwa mashahidi wa uongo wa Mungu; kwa maana tulimshuhudia Mungu ya kuwa alimfufua Kristo, ambaye hakumfufua, ikiwa wafu hawafufuliwi.

16 Maana kama wafu hawafufuliwi, Kristo naye hakufufuka.

17 Na kama Kristo hakufufuka, imani yenu ni bure; mngalimo katika dhambi zenu.

18 Na hapo wao nao waliolala katika Kristo wamepotea.

19 Kama katika maisha haya tu tumemtumaini Kristo, sisi tu maskini kuliko watu wote.

20 Lakini sasa Kristo amefufuka katika wafu, limbuko lao waliolala.

Unaona, mistari hiyo inatuonyesha kuwa, wakati ule kulizuka kundi la Wakorintho ambao walianza kuamini kuwa hakuna kiyama ya wafu(yaani hakuna ufufuo wa wafu), Imani kama ile waliokuwa nayo masadukayo, kwamba mtu akifa amekufa, habari yake imeishia hapo. Isipokuwa tu tofauti yao na masadukayo ni kuwa masadukayo walikuwa hawamwamini Kristo, lakini hawa walikuwa wanamwamini, na tena walikuwa wanaamini kuwa alikufa akafufuka.

Sasa ndio hapo ukisoma mstari wa 13-18 utaona mtume Paulo anawauliza maswali, yanayokinzana na Imani yao, anawauliza kama hawamini kuwa kuna kiyama wa wafu, kwanini waamini kuwa Kristo alifufuka?. Na kama hakufufuka, basi Imani yao ni bure, hata hao waliolala katika Kristo wamepotea. Hawapaswi kuamini hata ufufuo wa Yesu.

Mpaka hapo utakuwa umeona kuwa, mstari huo wa 18 haumaanishi kuwa wale waliolala katika Kristo wamepotea.

Lakini mstari wa 19 anamalizia na kusema..

19 Kama katika maisha haya tu tumemtumaini Kristo, sisi tu maskini kuliko watu wote.

Neno maskini kama lilivyotumika hapo ni Zaidi ya kukosa fedha.. Yaani sisi tuliomwamini Kristo, kwasababu ya maamuzi yetu hayo ya kumwishia yeye, tutakuwa kama watu waliodharaulika, au watu waliotupwa chini kuliko watu wote ulimwenguni. Japo tu juu ya wote.

Swali ni je! Na wewe leo hii Unaogopa kuchekwa kwa ajili ya Yesu? Au kudharauliwa, au kutengwa, au kufukuzwa kazi kwa ajili yake? Mitume hawakujali hilo, kwanini wewe uogope?..Kumbuka kumwamini Yesu ni pamoja na kukubali shutma kwa ajili ya jina lake. Huko ndiko kujitwika msalaba wako alikokuzungumzia Bwana Yesu

Alisema.

Marko 8:38 “Maana kila mtu atakayenionea haya mimi, na maneno yangu, katika kizazi hiki cha uzinzi na dhambi, Mwana wa Adamu atamwonea haya mtu huyo, atakapokuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika watakatifu”.

Lakini Zaidi ya yote alisema maneno haya kwa wale watakaoshinda….

Ufunuo 3:21 “Yeye ashindaye, nitampa kuketi pamoja nami katika kiti changu cha enzi, kama mimi nilivyoshinda nikaketi pamoja na Baba yangu katika kiti chake cha enzi”.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

MZAZI, JALI MAISHA YA KIROHO YA MTOTO WAKO.

VIKAANGUKA MACHONI PAKE VITU KAMA MAGAMBA.

KITABU CHA YUDA: SEHEMU YA 1

NITAUPATAJE UPENDO WA KI-MUNGU NDANI YANGU?

Je ni kweli imani ya mtu ndiyo itakayomuokoa, na si kitu kingine?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/03/25/ni-kweli-waliolala-katika-kristo-wamepotea1wakor-1518/