KATIKA MLIMA WA BWANA ITAPATIKANA.

by Admin | 19 June 2021 08:46 pm06

Jina la Bwana wetu Yesu, libarikiwe, karibu tujifunza biblia..

Mwanzo 22: 6 “ Basi Ibrahimu akazitwaa kuni za hiyo sadaka, akamtwika Isaka mwanawe; akatwaa moto na kisu mkononi mwake, wakaenda wote wawili pamoja.

7 Isaka akasema na Ibrahimu baba yake, akinena, Babangu! Naye akasema, Mimi hapa, mwanangu. Akasema, Tazama! Moto upo, na kuni zipo, lakini yuko wapi mwana-kondoo kwa sadaka ya kuteketezwa?

 8 Ibrahimu akasema, Mungu atajipatia mwana-kondoo kwa hiyo sadaka, mwanangu. Basi wakaendelea wote wawili pamoja.

9 Wakafika mahali pale alipoambiwa na Mungu, Ibrahimu akajenga madhabahu huko, akaziweka tayari kuni, kisha akamfunga Isaka mwanawe, akamweka juu ya madhabahu, juu ya zile kuni.

 10 Ibrahimu akanyosha mkono wake, akakitwaa kisu ili amchinje mwanawe.

11 Ndipo malaika wa Bwana akamwita kutoka mbinguni, akasema, Ibrahimu! Ibrahimu! Naye akasema, Mimi hapa.

12 Akasema, Usimnyoshee kijana mkono wako, wala usimtendee neno; kwa maana sasa ninajua ya kuwa unamcha Mungu, iwapo hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee.

 13 Ibrahimu akainua macho yake, akaangalia, na tazama, kondoo mume yuko nyuma yake, amenaswa pembe zake katika kichaka. Basi Ibrahimu akaenda akamtwaa huyo kondoo, akamtoa awe sadaka ya kuteketezwa badala ya mwanawe.

14 Ibrahimu akapaita mahali hapo Yehova-yire, kama watu wasemavyo hata leo, Katika mlima wa BWANA itapatikana”.

Kabla ya kufika mlimani Isaka alimwuliza Baba yake “Tazama! Moto upo, na kuni zipo, lakini yuko wapi mwana-kondoo kwa sadaka ya kuteketezwa?”.. Lakini Ibrahimu hakuwa na jibu la uhakika!.. Akaishia tu kusema.. “Bwana atajipatia mwanakondoo”..lengo la Ibrahimu kusema vile ni kumfumba tu macho!, mwanae Isaka asijue kuwa yeye ndiye anayekwenda kuchinjwa..

Na walipofika katika mlima wa Bwana, Ibrahimu tayari akiwa ameshamfunga mwanawe kwaajili ya kumchinja, tunasoma… Malaika wa Bwana alimzuilia na kumfumbua macho amwone mwanakondoo  aliyekuwa amenaswa pembe zake kwenye kichaka kilichopo nyuma yake.

Kondoo yule haijulikani alitoka wapi, pengine alipotea wakati wachungaji walipokuwa wanachunga huko milimani, na kunaswa kwenye kichaka kimoja wapo katika huo mlima, mahali pale pale Ibrahimu alipofika..Hivyo kwa vyovyote vile ilivyokuwa, lakini mwisho wa siku tunaona, tayari Mungu alikuwa amemwandaa mwanakondoo yule kwaajili ya sadaka ya kuteketezwa..

Nanichotaka uone ni kuwa sadaka inayompendeza Bwana haipatikani chini, bali inapatikana juu katika Mlima wa Bwana… Ndio maana hapo katika mstari wa mwisho tunasoma…

“Ibrahimu akapaita mahali hapo Yehova-yire, kama watu wasemavyo hata leo, Katika mlima wa BWANA itapatikana”…

Kumbuka sio katika mlima mwingine wowote itapatikana, la! Bali katika MLIMA WA BWANA TU!..Ndio maana hapo anasema “kama watu wasemavyo”..maana yake watu walishafanya utafiti na kugundua kuwa Baraka za Mungu hazipatikani mahali pengine popote, au katika mlima mwingine wowote isipokuwa katika Mlima wa Bwana. Sasa tangu huo wakati wayahudi wakapaheshimu mahali hapo Ibrahimu alipomchinja huyo mwana kondoo, na mahali hapo ndipo pakajulikana kama Mlima wa Bwana tangu wakati huo, na ndipo hekalu la Mfalme Sulemani lilipojengewa.. Hivyo baraka zote walikuwa wanazipata kutoka katika nyumba ile ya Mungu, ambayo ilijengwa juu ya m lima wa huo wa Bwana, uliojulikana kama Mlima Moria..(ndipo mahali pa juu Bwana alipopachagua)

Lakini baada ya Bwana Yesu kuja, Mlima wa Bwana ulibadilika kutoka “kuonekana kwa macho” mpaka “kutokuonekana kwa macho”

Tusome,

Yohana 4:20 “Baba zetu waliabudu katika mlima huu, nanyi husema ya kwamba huko Yerusalemu ni mahali patupasapo kuabudia.

21 Yesu akamwambia, Mama, UNISADIKI, SAA INAKUJA AMBAYO HAMTAMWABUDU BABA KATIKA MLIMA HUU, WALA KULE YERUSALEMU.

22 Ninyi mnaabudu msichokijua; sisi tunaabudu tukijuacho; kwa kuwa wokovu watoka kwa Wayahudi.

23 LAKINI SAA INAKUJA, NAYO SASA IPO, ambayo waabuduo halisi WATAMWABUDU BABA KATIKA ROHO NA KWELI. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu”.

Umepaona mlimani kwa Bwana leo?.. Si kule Yerusalemu, wala si katika mojawapo ya milima tunayopanda kwenda kuomba kila siku… bali ni katika Roho, na si katika Roho tu..bali katika Roho na kweli.

Unapompokea Yesu katika maisha yako, na kubatizwa na kupokea kipawa cha Roho Mtakatifu na kuishi katika Neno la Mungu.. Hapo tayari upo mlimani kwa Bwana. Kwasababu umebatizwa katika Roho Mtakatifu na vile vile unaishi katika Kweli ya Neno la Mungu.

Je leo upo mlimani kwa Bwana au bado upo chini?.. Kumbuka Baraka za kweli za Mungu zipo mlimani..huna budi kumchukua mwanao mpendwa na kuanza safari ya kwenda naye mlimani…Njia ya mlimani ni msalaba wa Bwana Yesu.

Mwanao mpendwa ni nini leo hii?..je! ni kazi yako?, elimu yako?, fedha zako?, hazina yako? Ndugu zako?.. Zichukue leo na kwenda naye kwa Bwana mlimani..kuwa radhi kuvipoteza vyote kwaajili ya Bwana kama Ibrahimu, na nakuambia badala ya kufikiri utavipoteza hivyo, kinyume chake utavipata kama Ibrahimu…

Lakini unapomfuata kuwa tayari kupoteza kila kitu!..ili upate kila kitu..

Mathayo 10:34 “Msidhani ya kuwa nimekuja kuleta amani duniani; la! Sikuja kuleta amani, bali upanga.

35 Kwa maana nalikuja kumfitini mtu na babaye, na binti na mamaye, na mkwe na mkwe mtu;

36 na adui za mtu ni wale wa nyumbani mwake.

37 Apendaye baba au mama kuliko mimi, hanistahili; wala apendaye mwana au binti kuliko mimi, hanistahili.

38 Wala mtu asiyechukua msalaba wake akanifuata, hanistahili.

39 Mwenye kuiona nafsi yake ataipoteza; naye mwenye kuipoteza nafsi yake kwa ajili yangu ataiona”

Na pia alisema…

Mathayo 16:24 “Wakati huo Yesu aliwaambia wanafunzi wake, Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake, anifuate.

25 Kwa kuwa mtu atakaye kuiokoa nafsi yake, ataipoteza; na mtu atakayepoteza nafsi yake kwa ajili yangu, ataiona.

26 Kwani atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi yake? Au mtu atatoa nini badala ya nafsi yake ?”

Hiyo ndio gharama ya kwenda mlimani kwa Bwana, ndio gharama ya kumwabudu Mungu katika Roho na Kweli.

Kama hujampokea Yesu na unataka kufanya hivyo leo, basi hapo ulipo jitenge dakika chache kisha piga magoti na zungumza na Bwana, kiri wewe ni mwenye makosa, na mwombe Bwana akurehemu, na baada ya hapo, dhamiria kuacha mambo yote maovu uliyokuwa unayafanya kwa wazi na kwa siri, kama ulevi, wizi, chuki, utukanaji, tamaa mbaya, kujichua, uasherati, usengenyaji n.k. Na baada ya hapo..Na baada ya hapo tafuta ubatizo sahihi, ambao ni wa maji mengi na kwa jina la Yesu Kristo, na Roho Mtakatifu atakuongoza katika kuijua kweli yote. Hapo utakuwa umefika mlimani kwa Bwana, na yale yote ambayo ulikuwa unadhani umeyapoteza..Bwana atayarejesha upya katika usahihi Zaidi.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

Mlima Gerizimu na Ebali ni ipi, na umuhimu wao rohoni ni upi?

Kama wakitenda mambo haya katika mti mbichi, itakuwaje katika mkavu?

Kwanini  vizazi vya ukoo wa Yesu vinajipinga katika Mathayo na Luka.

Maana Ya Maneno Katika Biblia.

Ni nani aliye kipofu, ila mtumishi wangu?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/06/19/katika-mlima-wa-bwana-itapatikana/