WAPENZI, MSIIAMINI KILA ROHO.

by Admin | 16 August 2021 08:46 pm08

Wakati tunaoishi ni wakati ambao kuna machafuko mkubwa sana ya rohoni kuliko hata nyakati nyingine zilizowahi kupita huko nyuma,. Na muasisi wa hayo  ni shetani kwasababu anajua katika agano letu jipya kiini cha Kanisa ni ROHO MTAKATIFU. Hivyo anajua akiruhusu Roho wa Mungu peke yake alitawale kanisa, atawakosa watu wengi sana.

Hivyo tangu ule wakati wa mitume, alibadilisha mbinu zake za kivita, akitaka kulishambulia kanisa, haji tena mwilini, bali, ni anakuja na roho za udanganyifu zinazofanana sana na Roho Mtakatifu wa kweli kumbe sio.

Hivyo kuanzia ule wakati alianza kutoa matoleo mengi sana ya roho hizo. Mpaka sasa matoleo aliyonayo ni ya hali ya juu sana, kiasi kwamba usipokuwa makini utaweza ukavamiwa na roho za udanganyifu ukadhani ni Roho Mtakatifu kumbe ni uongo. Tupo katika wakati ambao si wa kiziamini kila roho zinazohubiriwa na watu.

Na ndio maana mitume walituonya na kusema..

1 Yohana 4:1 “Wapenzi, msiiamini kila roho, bali zijaribuni hizo roho, kwamba zimetokana na Mungu; kwa sababu manabii wa uongo wengi wametokea duniani”.

Sasa ili tuwe salama ni vizuri tukajua tabia za kweli za  Roho Mtakatifu zipoje, ili tuwe na amani na tulichokipokea.

  1. Tabia ya kwanza ni kuwa Atakufanya uwe Mtakatifu: 

Kama jina lake lilivyo, “Roho Mtakatifu”, ndicho anachokifanya ndani ya mtu pale anapokuja juu yake rasmi, Atamfanya awe mtakatifu. Kama alivyosema katika 1Wakorintho 3:16, kuwa miili yetu ni lazima iwe mitakatifu kwasababu huyo Roho anayekaa ndani yetu ni Mtakatifu. Hivyo Ni lazima ahakikishe kuwa yale matunda yote ya roho yapo ndani yako sawasawa (Wagalatia 5:22-23)

Hivyo ukiona umepokea Roho, ambayo ndani yako haikupi kiu ya kuwa mtakatifu, yaani kuacha anasa, kuacha uvaaji mbovu, kuacha, miziki ya kidunia, kuacha vimini, na milegezo, kuwa na upendo, na kiasi, basi ujue hiyo sio Roho ya Mungu, haijalishi utanena kwa lugha muda mrefu kiasi gani.. Kimbia hapo, haraka sana.

2) Atakuongoza katika kuijua kweli yote(Yohana 16:13): 

Kazi nyingine ya Roho wa kweli wa Mungu, ni kuwa hatakuacha katika hali hiyo hiyo,ya ujinga wa kiroho uliokuwa nao sikuzote, ni lazima akupigishe hatua za kiufahamu mpaka kufikia kusimama imara katika maandiko. Lakini ukiona umeokoka na miaka nenda rudi, hujui chochote kuhusiana na Neno la Mungu, wewe unachojua ni habari za wachawi na mapepo, ujue kuwa Huyo sio Roho Mtakatifu uliyempokea bali ni roho nyingine ya adui ipo ndani yako.

3) Atamshuhudia Kristo ndani yako : 

Roho Mtakatifu kazi yake ni kutoa ushuhuda wa Kristo katikati ya kanisa lake, na sio wa mwanadamu yoyote. Ikiwa na maana kiini cha kanisa ulilopo, au huduma, unayoitumikia msingi wa hapo ni lazima awe Bwana Yesu Kristo. Na sio mwanadamu Fulani, au mtakatifu Fulani. Ukiona Kristo hapewi kipaumbele chochote, au anachukuliwa kama mtu wa ziada tu, ujue roho ya mpingakristo ipo hapo.

1Yohana 4:2 “Katika hili mwamjua Roho wa Mungu; kila roho ikiriyo kwamba Yesu Kristo amekuja katika mwili yatokana na Mungu.

3 Na kila roho isiyomkiri Yesu haitokani na Mungu. Na hii ndiyo roho ya mpinga Kristo ambayo mmesikia kwamba yaja; na sasa imekwisha kuwako duniani”.

4) Ataweka karama au huduma ndani yako (1Wakorintho 12):

Karama hiyo/ huduma hiyo Roho Mtakatifu anaiweka kwa lengo la kulijenga kanisa la Mungu. Haiwezekani, ukawa umeokoka muda mrefu na miaka mingi, na umesema umepokea Roho Mtakatifu lakini kazi yako katika ufalme wa mbinguni haionekani. Wakati mojawapo ya kazi ya Roho Mtakatifu ni kuweka vipawa ndani yetu.

Hivyo kama hutakuwa mchungaji, au nabii, au mwinjilisti, au shemasi, au mwenye karama ya lugha, n.k basi utakuwa ni nyingine yenye faida katika kanisa kama kukirimu, kuimba, kufadhili n.k. Lakini haiwezekani kiungo kikawa hakina kazi kabisa katika mwili wa Kristo, kama mshirika anayekuja na kuondoka, miaka yote, ukiona hivyo ujue kuwa Roho uliyempokea si wa Mungu, bali ni wa adui.

5) Atachochea kuomba ndani yako. (Warumi 8:6)

Maandiko yanasema Roho Mtakatifu anaugua ndani yetu, kwa namna isiyoweza kutamkwa. Ikiwa na maana Mkristo wa kweli aliyepokea Roho, hataona amani kukaa wiki, miezi, miaka bila kuomba. Ile furaha ya wokovu itaondoka tu ndani yake, Hivyo atalazimika, kuwa mwombaji mzuri, kuhudhuria mikesha, na kufunga wakati mwingine.

Lakini ukiona unayo amani, kukaa mwezi mzima bila kuomba, na ndani yako husikii chochote, au mzigo wowote, hapo umepokea Roho nyingine ya adui. Jitathimini tena.

Tabia hizi tano (5), ukiziona ndani yako. Basi ujue Roho uliyempokea ni kweli Roho Mtakatifu, uwe na amani. Lakini kama hivyo vyote havipo ndani yako, Roho uliyepokea ni ya adui ibilisi. Unachopaswa ufanye ni umaanishe kuokoka katika maisha yako.

Maana yake, utubu dhambi zako kweli kweli, kisha ukabatizwe katika ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi na kwa jina la YESU KRISTO (Matendo 2:38). Kisha baada ya hapo, Roho wa kweli ataingia ndani yako, kuanza kukupigisha hizo hatua.

Kumbuka hizi ni siku za mwisho, na tumeaswa sana tuzijaribu hizo roho, usiridhike, na tabia mojawapo tu, jiulize je! Zote hizo zinaonekana ndani yako?

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

JE! UMEPOKEA KWELI ROHO MTAKATIFU?

TUJIFUNZE JAMBO KWA WANAWAKE HAWA WAWILI:

Je aliyezungumza na Musa kule jangwani ni Mungu mwenyewe au malaika wake?

ZIFAHAMU KAZI TATU ZA ROHO MTAKATIFU KATIKA ULIMWENGU.

AHADI YA ROHO ILIYOSALIA SASA KWA KIPINDI CHETU.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/08/16/wapenzi-msiiamini-kila-roho/