UMUHIMU WA KUBATIZWA.

by Admin | 4 February 2022 08:46 pm02

Ubatizo ni agizo la msingi sana, si la kulipuuzia hata kidogo!, na kwasababu shetani anajua ni agizo la msingi basi atatufuta kila njia watu wasibatizwe kabisa, au wabatizwe isivyopaswa na mioyoni waendelee kuamini kuwa tayari wameshabatizwa.

Faida za ubatizo zipo nyingi sana, lakini leo tutajifunza faida moja kuu ya ubatizo. Ambapo baada ya kuijua hiyo, basi sisi wenyewe tutafanya maamuzi tukabatizwe au tusibatizwe!.

Na faida yenyewe ni KUOKOLEWA NA GHADHABU YA MUNGU JUU YA MAADUI ZETU NA MAADUI WA BWANA.

Mungu alipotaka kumwokoa Nuhu, ilimbidi aigharikishe dunia yote na yeye Nuhu akiwa ndani yake!, lakini siri ni kwamba maji yaliwaua maadui zake Nuhu na maadui za Bwana huko nje!, lakini yakamwacha Nuhu salama.

Kwaufupi tendo hilo biblia inalifananisha na Ubatizo kwa Nuhu.

Ndio maana maandiko yanasema…

1Petro 3:20 “watu wasiotii hapo zamani, uvumilivu wa Mungu ulipokuwa ukingoja, siku za Nuhu, safina ilipokuwa ikitengenezwa; ambamo ndani yake wachache, yaani, watu wanane, waliokoka kwa maji.

21 MFANO WA MAMBO HAYO NI UBATIZO, UNAOWAOKOA NINYI PIA SIKU HIZI; (siyo kuwekea mbali uchafu wa mwili, bali jibu la dhamiri safi mbele za Mungu), kwa kufufuka kwake Yesu Kristo”.

Hivyo ubatizo wa Nuhu na nyumba yake, ulikuwa ni kwa lengo la kuuondoa Uovu uliokuwa unamzunguka.

Kadhalika wakati Mungu alipotaka kuliharibu jeshi la Farao moja kwa moja lisiwasumbue Israeli tena, hakutumia ugonjwa wa Tauni, wala hakushusha moto, bali alikwenda kuligharikisha katika bahari ya Shamu, na ndio ikawa mwisho wa waMisri kuwafuatilia wana wa Israeli. (Tendo hilo pia linafananishwa na ubatizo wa wana wa Israeli).

1Wakorintho 10:1 “Kwa maana, ndugu zangu, sipendi mkose kufahamu ya kuwa baba zetu walikuwa wote chini ya wingu; wote wakapita kati ya bahari;

2 WOTE WAKABATIZWA WAWE WA MUSA KATIKA WINGU NA KATIKA BAHARI”

Sasa gharika iliua maadui wote wa Bwana na kumwacha Nuhu mwenyewe salama, vile vile Bahari ya Shamu iliwaua maadui wote wa Bwana na kuwaacha Israeli salama. Vivyo hivyo Ubatizo wa maji mengi leo unawaua maadui wote wa Bwana juu ya mtu, wanaotufuatilia na kutuacha sisi salama.

Unapozamishwa katika maji mengi na kuibuka juu, hapo ni sawa na umepita katika ile bahari ya Shamu yenye maji mengi na kwasababu upo ndani ya kuta zinazozuia maji (yaani upo ndani ya Yesu) unakuwa unatoka salama bila kufa, lakini maadui zako ambao ni (madhaifu ya yule adui, tabu, mapepo, shida, na mambo mengine yote kutoka kwa yule adui), hayatatoka salama kwenye hayo maji. Yatakuwa ndio mwisho wao, kama majeshi ya Farao yalivyogharikishwa, kwasababu yale maji si kwa lengo la kukuangamiza wewe, bali kuyaangamiza majeshi yote ya adui.

Nuhu alipita katikati ya maji mengi lakini yale maji hayakumuua, bali yaliwaangamiza wale watu waliokuwa wanamdhihaki, waliokuwa wamtesa kutokana na Imani yake, pengine waliokuwa wanamfunga, waliokuwa wanamfanyia dhuluma n.k.

Na maji ya ubatizo si kwa lengo la kukudhuru wewe, bali kukuokoa na kuyaharibu majeshi ya Adui ambayo yakibaki yatakuletea madhara katika safari yako.

Ndio maana maandiko yanasema..

1Petro 3:21 “MFANO WA MAMBO HAYO NI UBATIZO, UNAOWAOKOA NINYI PIA SIKU HIZI…”

Je! na wewe unataka majeshi ya Adui yasiendelee kukufuata, baada ya kumpokea Kristo!, tafuta ubatizo wa maji mengi na kwa Jina la Yesu, (Au kama ulibatizwa isivyo sahihi kwa kunyunyiziwa au kwa jina lingine lisilo la Yesu, basi rekebisha ubatizo huo kama wale watu wa Efeso katika Matendo 19:1-5)

Na ni kwanini ubatizo ni kwa jina la YESU na si kwa jina lingine?, ni kwasababu maandiko yanasema wakati ule  wa nawa Israeli wanavuka Shamu “WOTE WAKABATIZWA WAWE WA MUSA KATIKA WINGU NA KATIKA BAHARI”. Na Musa wetu sasahivi watu wa agano jipya ni BWANA YESU, ambaye anatutoa sisi kutoka Misri ya kiroho na kutupeleka Kaanani(mbinguni), na anatuagiza kila mmoja wetu tubatizwe kwa jina lake ili tuwe wake, ndio maana tunabatizwa kwa jina la Bwana Yesu kila mmoja (soma Matendo 2:38, Matendo 8:16, Matendo 10:48 na Matendo 19:5).

Zipo faida nyingi sana za ubatizo, hii ni mojawapo tu, tenga muda tafuta kuzijua zote!, kwamaana ni muhimu sana kuzijua.

Kama bado hujaabatizwa tafuta kanisa ukabatizwe, au hapo hapo kanisa ulipo ulizia ubatizo (lakini hakikisha ni ubatizo sahihi wa maji tele na kwa jina la Yesu)!, Fanya hivyo haraka iwezekanavyo,

Na ubatizo ni bure!, na wala hauhitaji madarasa ya kupitia. Yule Mkushi aliyebatizwa na Mtume Filipo, hakupitishwa kwenye darasa lolote, pale alipoamini tu!, tayari alikidhi vigezo vyote vya kubatizwa, na akabatizwa!

Bwana akubariki.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

JE! UMEBATIZWA UBATIZO SAHIHI?

Neno “Via” linamaanisha nini katika biblia?

Nini maana ya “Roho za manabii huwatii manabii?

IFAHAMU HUZUNI NA FURAHA YA MALAIKA.

FUMBO ZA SHETANI.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/02/04/umuhimu-wa-kubatizwa/