NAYE ALIKUWA HANA BUDI KUPITA KATIKATI YA SAMARIA.

by Admin | 7 May 2022 08:46 pm05

Nakusalimu katika jina kuu la Yesu Kristo Bwana, nakukaribisha tena, katika kuyatafakari maneno ya uzima, maadamu siku ile inakaribia.

Bwana wetu Yesu Kristo alipokuja hapa duniani, dira yake ya kwanza haikuwa kwa kila mtu duniani, bali ilikuwa kwanza kwa Wayahudi, kisha watu wengine baadaye, ndio maana hata watu wa mataifa walipomfuata awaponye aliweka ugumu mkubwa kidogo kwao, na aliwaeleza waziwazi kabisa kuwa sikutumwa kwa ajili yenu bali kwa wayahudi.( Soma Mathayo 15:22-28),

Hata kipindi kingine, alipowatuma wanafunzi kuhubiri, aliwakataza kabisa wasiwafuate mataifa ikiwemo wasamaria, waliokuwa Israeli wakati huo, bali wayahudi tu.

Mathayo 10:5 “Hao Thenashara Yesu aliwatuma, akawaagiza, akisema, Katika njia ya Mataifa msiende, wala katika mji wo wote wa Wasamaria msiingie.

6 Afadhali shikeni njia kuwaendea kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli”.

Umeona, kwahiyo kusudi la awali la Kristo lilikuwa ni kumalizana kwanza na wayahudi.. Lakini kuna wakati, ratiba zake zilivurugwa, Hivyo akalazimika tu kutumiza kusudi lake la kuokoa kwa muda kwa watu wa mataifa aliokutana nao..

Embu tusome..

Yohana 4:3 “aliacha Uyahudi, akaenda zake tena mpaka Galilaya.

4 NAYE ALIKUWA HANA BUDI KUPITA KATIKATI YA SAMARIA.

5 Basi akafika kunako mji wa Samaria, uitwao Sikari, karibu na lile shamba ambalo Yakobo alimpa Yusufu mwanawe.

6 Na hapo palikuwa na kisima cha Yakobo. Basi Yesu, kwa sababu amechoka kwa safari yake, akaketi vivi hivi kisimani. Nayo ilikuwa yapata saa sita.

7 Akaja mwanamke Msamaria kuteka maji. Yesu akamwambia, Nipe maji ninywe”.

Umeona hapo, tafakari vizuri, Bwana hakuwa na lengo la kuzungumza chochote pale Samaria, bali, mawazo yake yalikuwa ni kwenda Galilaya kwa wayahudi..Lakini sasa ili kufika Galilaya ilimlazimu apitie Samaria., Hakuna namna.. Samaria ilikuwa ni njia panda ya kufika Galilaya..

Na alipofika pale biblia inatuambia, alikuwa amechoka sana, lakini je! Alale tu? Kisa hakutumwa kwao? Au akae tu apumzikie, huku akitazama roho za makafiri zikipotea?.. Ni wazi kuwa hata kama ni mimi, ningekuwa sijatumwa mahali Fulani, halafu nimechoka, ya nini kujisumbua kufanya nisiyoagizwa? Ningelala zangu..

Lakini kinyume chake, ilimpasa aghahiri hata kula chakula, aghahiri hata uchovu wake, aanzane na yule mwanamke mwenye dhambi pale kisimani, jambo lililomfanya sio tu yule mwanamke mwenyewe kumshangaa, bali pia mitume wake paliporudi, kumwona anawahubiria mataifa tena mwanamke jambo ambalo yeye mwenyewe alilikataza, huko nyuma.

Yohana 4:9 “Basi yule mwanamke Msamaria akamwambia, Imekuwaje wewe Myahudi kutaka maji kwangu, nami ni mwanamke Msamaria? (Maana Wayahudi hawachangamani na Wasamaria.)

10 Yesu akajibu, akamwambia, Kama ungaliijua karama ya Mungu, naye ni nani akuambiaye, Nipe maji ninywe, ungalimwomba yeye, naye angalikupa maji yaliyo hai”.

Ni nini Bwana anataka tujifunze?

Ili ufikie Galilaya yako, huna budi kupitia Samaria, Ni Mungu mwenyewe ndio anayeruhusu hiyo hali, unasema nina mipango ya kwenda kuhubiri injili kwa watu Fulani mijini au vijijini, malengo ambayo ni mazuri, lakini leo hii unajikuta upo katika mazingira ya shule, ambayo hayatimizi malengo yako, Hapo hapo shuleni, kuwa muhubiri wa Injili, wahubirie wanafunzi wenzako, kwasababu imekupasa kwanza upitie hapo ndipo ufikie kule Mungu alikokuonyesha, au unakokutazamia.

Leo umejikuta katika mazingira ya kazini, usisubirie tu wakati Fulani kufika, ukasema bado bado. Kristo hakuwa na mawazo hayo. Alijua kabisa Samaria ni anapita tu, hana kusudi lolote pale, lakini aliwashuhudia Habari za wokovu, na hadi mwisho watu wengi wakamwamini hadi wakataka kumfanya awe mfalme wao, akakataa.

Kwahiyo wakristo wengi, sasa tumekuwa ni wa kusubiri suburi, tukisema ngoja kwanza nitoke hapa, au ngoja kwanza nimalize hiki au kile, ndio nitaanza kuifanya kazi ya Mungu.. Hujui ni kwanini Mungu kakupitisha hapo, tumia nafasi hiyo kumuhubiri Kristo,

Tumeambiwa, tuwe tayari wakati wote..ufaao na usiofaa.

2Timotheo 4:2 “lihubiri neno, uwe tayari, wakati ukufaao na wakati usiokufaa, karipia, kemea, na kuonya kwa uvumilivu wote na mafundisho”.

Halikadhalika Bwana Yesu mwenyewe  alituambia tujifunze kwake,(Mathayo 11:29)..Na hili ni somo mojawapo tunapaswa tulitafakari kutoka kwake, ili mahali popote tulipo tuwe watu wa kumzalia matunda, bila kungojea tufike Galilaya yetu.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

BADO UPO YERUSALEMU TU..GALILAYA HUTAKI KWENDA?

OLE WAKO KORAZINI NA BETHSAIDA.

TAFUTA UZIMA WA MILELE NA SI UZIMA TU!

JE MGOGORO WA URUSI NA UKRAINE,UMETABIRIWA KIBIBLIA?

Ni mlima gani Yule Mwanamke Msamaria aliokuwa anaumaanisha? (Yohana 4:19)

Ayari ni nini kama tunavyosoma katika biblia?

Kiburi cha Uzima ni nini? (1Yohana 2:16)

Hema ya kukutania ni nini, na ilikuwaje?

NDIPO HUENDA AKACHUKUA PEPO WENGINE SABA.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/05/07/naye-alikuwa-hana-budi-kupita-katikati-ya-samaria/