ANGALIA USIJE UKANG’OA NGANO KATIKATI YA MAGUGU.

by Admin | 3 February 2020 08:46 pm02

Naomba watu wote tusome hii…

Hakuna mtu asiyejua kuwa shetani, naye hujigeuza na kuwa mfano wa malaika wa Nuru (2Wakorintho 11:14)? Lakini tunapaswa tujiulize lengo la yeye kujibadilisha vile ni nini? Utagundua kuwa Hana lengo lingine zaidi ya kuuchafua utakatifu wa malaika ili na wao pia waonekane kuwa ni waovu. Vivyo hivyo na watumishi wake nao wanafanya kazi hiyo hiyo .. Ili mwisho wa siku tuhitimishe kuwa wote ni wabaya, wote ndio wale wale wapotoshaji.

Embu jaribu kuufikia tena vizuri ule mfano Bwana Yesu aliousema..

Mathayo 13:24 “Akawatolea mfano mwingine, akisema, Ufalme wa mbinguni umefanana na mtu aliyepanda mbegu njema katika konde lake;

25 lakini watu walipolala, akaja adui yake akapanda magugu katikati ya ngano, akaenda zake.

26 Baadaye majani ya ngano yalipomea na kuzaa, yakaonekana na magugu.

27 Watumwa wa mwenye nyumba wakaenda wakamwambia, Bwana, hukupanda mbegu njema katika konde lako? Limepata wapi basi magugu?

28 Akawaambia, Adui ndiye aliyetenda hivi. Watumwa wakamwambia, Basi, wataka twende tukayakusanye?

29 Akasema, La; msije mkakusanya magugu, na kuzing’oa ngano pamoja nayo.

30 Viacheni vyote vikue hata wakati wa mavuno; na wakati wa mavuno nitawaambia wavunao, Yakusanyeni kwanza magugu, myafunge matita matita mkayachome; bali ngano ikusanyeni ghalani mwangu”.

Umeelewa hapo? Ni kwanini magugu yaliachwa yaendelee kuwepo shambani hadi wakati wa Mavuno? Unadhani mwenye shamba alikuwa anapenda kuyaona yakiendelea kustawi shambani muda wote huo?, jibu ni la! lakini ilimpasa atumie hekima kwasababu alijua kama akitaka tu kuyashughulika kuyafyeka atajikuta anazing’oa na ngano ndani yake na mwisho wa siku atapata hasara kubwa ya kazi yake aliyoitaabikia..

Kwasababu wanasema wakati magugu yakiwa machanga, huwa yanatabia ya kushikamana sana na ngano, vilevile yanafanana mno kiasi kwamba kutofautisha gugu katikati ya ngano ni kazi sana..Hivyo ukijaribu kung’oa tu gugu moja, pembeni yake unaweza kuta zilikuwa ngano 6 zimejishikamanisha nayo, na mwisho wa siku ni hasara…Hivyo si kazi rahisi kama unavyofikiria, mahali pekee ambao utaweza kuziona na kuzing’oa bila kuathiri ngani ni wakati wa mavuno tu, kwasababu maumbile yako yanajitofautisha kabisa na ngano..

Ndugu yangu, tusiwe wepesi wa kutoa hukumu ya moja kwa moja kuwa makanisa yote ya kiroho, yanapotosha, makanisa madogo madogo ambayo hajasajiliwa yote ni feki, wachungaji wote ambao wanawaombea watu shida zao ni bandia, watu wote wanaokesha makanisani na kumwomba Mungu usiku na mchana ni wajinga, hawana akili, wote wanaomlilia Mungu ni wapumbavu, masikini waliokosa uelekeo wa maisha, wenye stress za maisha, wavivu na wasiojituma, wamekata tamaa, hawapendi kufanya kazi, wanapenda vya bure..

Ikiwa ni wapumbavu, wewe unataka wafanye nini ili wawe na hekima? Unataka waache kumlilia Mungu wao wakaililie pesa? Hiyo ndiyo iliyowaleta duniani?…Unataka Watumishi waache kuhudumu madhabahuni wote waondoke na wewe waende ofisi kutafuta pesa, ni nani basi atakayekaa kukuletea wewe injili,? Hata elimu yako inakufundisha kitu kinachoitwa Opportunity cost, ili uweze kufanya jambo moja kikamilifu ni lazima uache kufanya lingine..Huwezi kushika mawili kwa wakati mmoja..Na wengi wanaosema mambo kama hayo asilimia kubwa ni wale ambao hata Kristo hajaumbika vizuri ndani yao, wala hawayajua maandiko yanaagiza nini kuhusu mambo ya ibada..Si wote wanaomlilia Mungu hawajasoma kama wewe unavyofikiri, si wote wanaomtafuta Mungu, ni maskini kama wewe unavyodhani, si wote wanaokesha kuomba hawajui kuwa kuna kufanya kazi..

Tusitumie vigezo vya watu wachache wanaotumiwa na shetani kuliharibu kanisa la Mungu na kuhitimisha na wengine wote hawafai.. Wanaotumia mafuta ya upako, chumvi,sabuni, balbu, maji, wanaohubiri habari za mafanikio wakati wote, wanasahau toba ya msamaha, hao wote ndio mapando ya shetani yaliyowekwa ili kuwafanya watumishi wengine wote waonekane kuwa ni wa uongo…

Embu fumba kinywa chako, ishia tu kukemea, kukaripia na kuhubiri lakini usishiriki katika kuchua hatua yoyote ya nguvu, ili kutokomeza hilo suala na kuyaita makanisa yote ya kiroho ni (vibanda-Imani), na kutaka yote yafungiwe, au yawekwe masharti katika kuabudu.. wewe mwachie Mungu, yeye ndio atakayeshughulika nao, na yeye ndiye atakayewapukutisha mmoja baada ya mwingine, hiyo sio kazi yako rafiki.

Lakini ukijiona wewe una hekima zaidi ya Mungu..Angalia kuna roho ya mpinga-kristo inakunyemelea nyuma yako. Na Siku utakapoimpa ibilisi nguvu ya kutosha basi ujue kuwa wakati utafika hutaweza kuuza wala kununua wala kufanya jambo lolote kama hutakuwa na ile chapa ya mnyama…ambayo chumbuko lake litakuwa katika mambo kama hayo hayo ya ibada za sharti..

Maran Atha.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe au piga namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

JIEPUSHE NA MANENO YA MANABII WA UONGO.

UNAWAFAHAMU MANABII WA UONGO?

CHAPA YA MNYAMA

DHIKI KUU INAKUJA NA UNYAKUO UPO KARIBU.

JE! WEWE NI MBEGU HALISI YA KRISTO?

TOFAUTI KATI YA HEKALU, SINAGOGI NA KANISA NI IPI?

DANIELI: Mlango wa 12.

MAMBO 5 AMBAYO KILA MKRISTO ANAPASWA KUFAHAMU.

 

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/02/03/angalia-usije-ukangoa-ngano-katikati-ya-magugu/