Mahuru ndio nini?

by Admin | 20 April 2020 08:46 pm04

SWALI: Mahuru ndio nini? Kama Bwana alivyosema katika Mathayo 17:26, Na ni jambo gani tunajifunza pale?


JIBU: Tusome;

Mathayo 17:25 “Naye alipoingia nyumbani, Yesu alitangulia kumwuliza, akisema, Waonaje, Simoni? Wafalme wa dunia hutwaa kodi ama ushuru kwa watu gani? Kwa wana wao au kwa wageni?

26 Naye aliposema, Kwa wageni, Yesu alimwambia, Basi, kama ni hivyo, WANA NI MAHURU.

27 Lakini tusije tukawakwaza, enenda baharini ukatupe ndoana, ukatwae samaki yule azukaye kwanza; na ukifumbua mdomo wake utaona shekeli ichukue hiyo ukawape kwa ajili yangu na kwa ajili yako”.

Ukisoma mstari huo..Bwana alikuwa anazungumzia juu ya wale wanaostahili kulipishwa kodi kulingana na tamaduni za wakati huo…Kwamba kwa wakati huo watu wanaotoka mji mmoja kuingia mwingine ambao si wa kwao walikuwa wanatozwa ushuru…lakini wale wenyeji walipokuwa wanarudi kuingia kwao hawatozwi ushuru kwasababu wao ni wenyeji au wana wa huo mji…

Hivyo hapa Bwana alikuwa ametoka na wanafunzi wake kutoka mji mmoja kwenda mwingine ndani ya Mkoa wake mwenyewe ulioitwa Galilaya…lakini wakataka kumtoza nusu shekeli na ilihali yeye ni mwenyeji wa Mkoa ule na wala si mgeni (Galilaya ilikuwa inajumuisha majimbo ya Nazareti, Korazini, Kapernaumu, Tiberia, Naini, Magdala na mengine machache madogo madogo), na Galilaya yote ilikuwa chini ya Mfalme Herode wa kirumi. Hivyo yoyote aliyekuwa mzawa wa majimbo hayo alikuwa huru kwenda popote katikati ya hayo majimbo pasipo kutozwa ushuru wowote…

Ni sawa na sisi tulivyo na uhuru wa kusafiri mkoa wowote bila vizuizi.

Lakini hawa walipomwona Yesu waliingiwa na tamaa ingawa walijua kabisa ni mzawa, lakini waliingiwa na tamaa labda pengine walimwona anafuatwa na watu wengi wakadhani atakuwa na pesa nyingi hivyo wakawa wanatafuta sababu za kupata fedha kutoka kwake..

Sasa Bwana ndio anamwuliza Petro je wanaotozwa ushuru ni wageni au WANA ?(neno wana ni sawa na wenyeji)…Ndio Petro anamjibu kwamba ni Wageni ndio wanaopaswa kutozwa ushuru na si wenyeji…Ndipo Bwana akamwambia basi kama ni hivyo Wana au kwa lugha nyingine wenyeji ni MAHURU..yaani maana yake wazawa WAPO HURU…Hawapaswi kutozwa chochote kulingana na sheria ya nchi.

Lakini kwasababu Bwana ana hekima nyingi na siku zote anampendeza Mungu na wanadamu hakutaka kuwakwaza kwa vyovyote vile..ndio akamwambia Petro akavue na samaki atakayezuka wa kwanza mdomoni atakuta fedha aje kuilipa kwaajili yake na ya Petro.

Tunajifunza hapo na sisi…sio kila vita vya kupambana nayo…vingine mwachie Bwana akupiganie..Hebu jiulize hapa Petro angeanza kugoma..oo hapana hiyo sio haki, mnatuonea, mnatunyanyasa..sisi ni wenyeji n.k Bila shaka asingeuona ule muujiza Bwana alioufanya…Na kama ukichunguza pale hawakuwa hata na senti..ndio maana Bwana akamwambia Petro akavue…Sasa kwa utulivu wa Petro faida aliyoipata ya kuwa mtulivu na kumtii Bwana na kumwamini alipoenda kuvua ili aje kulipa ushuru ambao si halali yake kuulipa.. alipata faida mara mbili..

Faida ya kwanza aliyoipata ni kwenda kulilipa lile deni alilokuwa anadaiwa ambalo halikuwa halili kwake kulilipa…na faida ya pili na ya muhimu ni Yule samaki…pengine alikwenda kumuuza au kumtumia kwa kitoweo baada ya kumtoa ile sarafu mdomoni…

Vivyo hivyo wakati mwingine tunaweza kusingiziwa kesi au madeni ambayo si halali kwetu kuyalipa…usining’unike katika hali kama hiyo..umejaribu kuonyesha kwamba sio halali lakini hueleweki usianze kunung’unika na kulalamika mpaka kuonekana sasa huna imani na maana..mpaka watu wakaanza kushangaa kama kweli wewe ni mkristo au la!..kwa matusi hayo na manung’uniko hayo..

Wewe unachopaswa kukifanya nenda katafute namna ya kulipa deni lile au kuikabili kesi ile, hata kulipa kile chote wanachokushitaki..na huko huko njiani Mungu atakufanyia muujiza wa kuilipa ile na utapata cha ziada.

Hizo zilikuwa ni kanuni za Bwana wakati wote, nasi tupate kitu kidogo cha kujifunza hapo..

Luka 6: 29 “Akupigaye shavu moja, mgeuzie la pili, naye akunyang’anyaye joho yako, usimzuilie na kanzu.

30 Mpe kila akuombaye, na akunyang’anyaye vitu vyako, usitake akurudishie”.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

TAHADHARI YA NEEMA YA MUNGU.

MOJA YA HIZI SIKU TUTAONA MABADILIKO MAKUBWA SANA.

Roho, Nafsi, na Mwili vina utofauti gani?

Je kupiga miayo ni ishara ya mapepo?

NIMEOKOKA, ILA MUNGU NDIYE ANAYEJUA NITAKWENDA WAPI.

KARAMU YA MWANA-KONDOO.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/04/20/mahuru-ndio-nini/