NI NANI ATAKAYETUTENGA NA UPENDO WA KRISTO?

by Admin | 26 April 2020 08:46 pm04

Warumi 8:35 “Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga?”

Mstari huu ukiusoma kwa haraka haraka ni rahisi kuutafsiri hivi… “Ni nini kitakachotufanya sisi tuache kumpenda Yesu, au tumwache Yesu..je ni dhiki au shida au njaa au adha au uchi?”…Lakini hiyo sio tafsiri yake, wala Mtume Paulo hakuuandika mstari huo kwa msaada wa Roho Mtakatifu kulenga hiyo tafsiri, wala hakumaanisha hivyo…Kwasababu hakuna mtu yeyote duniani ambaye kwa nguvu zake mwenyewe anaweza kupitia njaa, au dhiki, au shida na asijitenge na Kristo…hakuna!. Lakini je mstari huo una maana gani?

Tafsiri ya mstari huo ni hii… “Ni nani au ni kitu gani kitachachotufanya sisi tusipendwe na Kristo au tuchukiwe na Kristo?, je ni njaa, dhiki, shida, uchi, hatari au upanga?”..Hii ndio tafsiri yake.

Upendo uliozungumziwa hapo si upendo wetu kwa Kristo bali ni upendo wa Kristo kwetu. Maana yake ni kwamba tunapopitia njaa Kristo hawezi kujitenga na sisi, tunapopitia shida Kristo hawezi kutukimbia wala kutuchukia, tunapopitia taabu bado atakuwa Pamoja na sisi kutufariji na kujishughulisha na mambo yetu, tutakapopitia upanga bado atakuwa upande wetu kutushika mkono na kutuongoza safarini kama maandiko yanavyosema katika..

Zaburi 23:4 “Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya; Kwa maana Wewe upo pamoja nami, Gongo lako na fimbo yako vyanifariji.

5 Waandaa meza mbele yangu, Machoni pa watesi wangu. Umenipaka mafuta kichwani pangu, Na kikombe changu kinafurika.

6 Hakika wema na fadhili zitanifuata Siku zote za maisha yangu; Nami nitakaa nyumbani mwa Bwana milele”.

Hivyo kama tumemwamini Kristo basi tufahamu kuwa Pendo lake limemiminwa juu yetu…Hivyo kamwe hawezi kutuacha katika mapito yoyote tutakayopishana nayo…Kwasababu majaribu tumewekewa, ni lazima tuyapitie lakini yeye ameahidi kuwa na sisi na kutupa ushindi..Kwasababu hakuna chochote kile kitakachotutenga na Upendo wake.

Lakini kama hujampokea Yesu, bado hujaingizwa katika Pendo lake hili…upo nje ya Mlango…Kristo hawezi kuwa upande wako kwasababu wewe humwamini na humtaki..Lakini anakuita leo..usifanye moyo wako kuwa mgumu..Unachotakiwa kufanya bila kupoteza muda ni leo kukata shauri la kuokoka..Maana yake ni kwamba unamkiri yeye kwa kinywa chako kwamba ni Bwana na mwokozi wa Maisha yako, na kisha unatubu (Kutubu maana yake ni kugeuka/kughairi maovu na mabaya yote uliyokuwa unayafanya yasiyompendeza Mungu)..maana yake ni kwamba kama ulikuwa ni mwasherati unageuka na kuuacha uasherati wako..kama ulikuwa unakwenda kuiba, unaacha hiyo safari na wizi wote kwa ujumla, kama ulikuwa ni muuaji unaacha mauaji..na mambo mengine yote yasiyompendeza Mungu unayaacha…

Sasa ukishayaacha hayo yote kwa vitendo namna hiyo, hapo ndipo utakuwa umetubu..na kama umetubu Mungu atakuwa tayari kukurehemu na kukusamehe uzinzi wako wote uliokuwa unaufanya huko nyuma, na rushwa zako na matusi yako na kila kitu ulichokuwa unakifanya kilicho kinyume na mapenzi yake…Baada ya rehema hiyo kuingia ndani ya moyo wako..kuna AMANI fulani isiyokuwa ya kawaida ambayo Mungu anaiachia kwa mara ya kwanza kwa wale wote waliotubu kwa kumaanisha kabisa…Amani hiyo isiyoelezeka itaingia ndani yako…utaona kama kuna kifungo fulani kimeachia ndani yako…Hiyo amani ndiyo uthibitisho wa msamaha wako…

Sasa ili usiizimishe amani hiyo nenda katafute ubatizo haraka sana. Ubatizo sahihi na wa kimaandiko ni ule wa maji tele (Yohana 3:23) na kwa jina la Yesu Kristo (Matendo 2:38, Matendo 8:16, Matendo 10:48, na Matendo 19:5)..Ambalo ndio jina la Baba, Mwana na Roho Mtakatifu. Ukifanya hivyo amani hiyo itadumu ndani yako siku zote. Amani hiyo ndio pendo hilo la Kristo ambalo hata utakapopitia magumu, au shida au mateso au raha au mafanikio haitaondoka kamwe ndani yako. Itakulinda mpaka siku ya mwisho.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

BASI TUENDELEE KUMJUA MUNGU,NAYE ATATUJILIA KAMA MVUA YA VULI.

UPENDO NI NINI NA JE! KUNA AINA NGAPI ZA UPENDO?

NINI KINAFUATA SIKU ILE ILE YA KUOKOKA!

ANGALIA UZURI WAKO, USIGEUKE KUWA KITANZI CHAKO.

MOJA YA HIZI SIKU TUTAONA MABADILIKO MAKUBWA SANA.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/04/26/ni-nani-atakayetutenga-na-upendo-wa-kristo/