NI KWA NAMNA GANI ROHO HUTUTAMANI KIASI CHA KUONA WIVU?

by Admin | 16 October 2020 08:46 pm10

Shalom.

Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe, karibu tujifunze maandiko. Yapo mambo kadhaa ya kujikumbusha pale tunapokuwa wakristo.

Ni lazima tujue kuwa Tunaposema tumeokoka, maana yake ni kuwa  tunakuwa tumeingia katika maagano ya ndoa takatifu na Mungu wetu. Mungu anakuwa mume wetu (Yeremia 3:14), na sisi tunakuwa bibi-arusi wake katika roho. Sasa ipo tahadhari ambayo Mungu alishaitoa tangu zamani za kale kwa watu wake alioingia nao maagano, aliwaambia, Mimi ni Mungu mwenye WIVU. Soma Kutoka 20:4-6, utaliona hilo, na kwamba wivu wake ni mbaya na unaweza kwenda hata mpaka vizazi vine  mbeleni, kama watu hawatamgeukia yeye. Na hiyo ni kwa kosa tu la kufanya ibada za sanamu.

Unaweza ukajiuliza Mungu muumba wa mbingu na nchi anakuwaje na wivu? Jibu ni  kwamba wivu ni sehemu yake, kwasababu sisi wanadamu tuliumbwa kwa mfano wake, na sio yeye kwa mfano wetu, hivyo tabia ya kuwa na wivu katika mahusiano imetoka kwake na sio kwetu..

Na biblia inatuambia  ukali wa wivu unazidi hata ule wa ghadhabu au hasira..Ni heri ukutane na mtu mwenye hasira umemuulia ndugu yake, kuliko kukutana na mtu mwenye wivu wa mpenzi wake.

Mithali 27:4 “Ghadhabu ni kali, na hasira ni gharika; Lakini ni nani awezaye kusimama mbele ya wivu”.

Na ndio maana tunapaswa tuliweke hilo akilini sisi wakristo, kwasababu wivu wa Mungu ulio juu yetu sisi wa agano jipya ni mkali kuliko ule uliokuwa kipindi cha agano la lake.

 Unajua ni kwanini?

Ni kwasababu ya ROHO MTAKATIFU, basi. Ni heri wale waliomtia Mungu wivu jangwani kwa kutengeneza ndama wa dhahabu, na kumwabudu kuliko  sisi tunaomtia wivu Roho Mtakatifu leo hii. Pale tunaposema tunapoiacha njia ya wokovu na kwenda kusujudia sanamu tunazozoziita za watakatifu, au tunapokwenda kuzini, au kufanya uasherati, ni ishara kamili kuwa tunamtia wivu Roho Mtakatifu aliye ndani yetu.

1Wakorintho 10: 21 “Hamwezi kushirikiana katika meza ya Bwana na katika meza ya mashetani. 22 Au twamtia Bwana wivu? Je! Tuna nguvu zaidi ya yeye?”

Biblia inasema hivi;

Yakobo 4:4 “Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? Basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.

5 AU MWADHANI YA KWAMBA MAANDIKO YASEMA BURE? HUYO ROHO AKAAYE NDANI YETU HUTUTAMANI KIASI CHA KUONA WIVU?

Kama tunavyosoma katika maandiko hayo, kwa lugha rahisi ni kuwa pale Roho Mtakatifu anapoingia ndani yetu, anatupenda upeo, yaani anatupenda sana kiasi kwamba anatuonea wivu mkali pale tunapoyahalifu maagizo ya Mungu kwa makusudi.

Na wivu huo unaweza kumfanya achukue uamuzi wowote mbaya juu yetu; Baadhi yetu anaruhusu hata tupitie magonjwa, wengine hata vifo visivyokuwa vya wakati, na sio shetani bali ni Mungu mwenyewe kasababisha.

Waefeso 4:30 “Wala msimhuzunishe yule Roho Mtakatifu wa Mungu; ambaye kwa yeye mlitiwa muhuri hata siku ya ukombozi”.

Lakini Mungu wetu mara nyingi amekuwa ni wa rehema, anaipitishia ghadhabu yake mbali, akingojea mtu mmoja atubu amgeukie.

Hivyo kama wewe ni mmojawapo, ambaye ulikuwa umeokoka ukamuasi Mungu, ukamtia Roho Mtakatifu wivu mwingi kwa matendo yako, na kwamba ulistahili kuhukumiwa, lakini mpaka leo bado unaishi, ni kwa neema tu, hivyo kama upo tayari kugeuka kwa dhati, fahamu kuwa Mungu atakusamehe.

Kwahiyo unachopaswa kufanya ni wewe mwenyewe kufanya maamuzi ya kutubu, kwa  kwenda sehemu yako ya siri, utubu mbele za Mungu, kisha, na baada ya hapo anza kuishi kama mkristo wa kweli, kwasababu Mungu ataanza kuyaangalia matendo yako kama kweli umebadilika, hivyo ukiwa umecha kweli kweli, basi ataiondoa hasira ya wivu wake juu yako, na kukuponya kama alikuwa tayari ameshaanza kukurarua.

Hivyo sikuzote kumbuka: Roho hututamani kiasi cha kutuonea wivu. Ni wajibu wetu kuishi kwa makini sana katika ukristo wetu.

Kama umeguswa kushare somo hili au mengine kama haya kwenye magroup ya whatsapp na penginepo, utafanya vyema kufanya hivyo, lakini tunaomba ufanye hivyo bila kubadilisha chochote wala kuondoa anwani ya wingulamashahidi na kuweka namba zako za simu ili kuzuia mkanganyiko. Kwasababu tumepokea malalamiko, kuna watu wasio kuwa na nia ya Kristo, kuchukua masomo na mwisho kuondoa namba au anwani yetu na kuweka namba zao, lengo lao ni kutaka sadaka kutoka kwa watu. (Wingu La Mashahidi hatujawahi kumpigia mtu simu na kumwomba sadaka). Hivyo chukua tahadhari!.

Bwana atubariki sote na kutuzidishia neema yake.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

JIHADHARI NA DHAMBI YA WIVU/HUSUDA.

KWANINI NABII ISAYA ALIAGIZWA KUHUBIRI UCHI?

KWANINI MAISHA MAGUMU?

IFANYE KAZI YA MUNGU PASIPO HOFU!

IMANI NI KUWA NA UHAKIKA WA MAMBO YATARAJIWAYO.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/10/16/ni-kwa-namna-gani-roho-hututamani-kiasi-cha-kuona-wivu/