IMANI NI KUWA NA UHAKIKA WA MAMBO YATARAJIWAYO.

IMANI NI KUWA NA UHAKIKA WA MAMBO YATARAJIWAYO.

Waebrania 11:1 “Basi imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana”.

Hebu tujifunze kitu kuhusu milango mitano ya ufahamu tunayoijua…ambayo ni Pua, ngozi, ulimi, macho na masikio…milango hii kazi yake ni kukupa uhakika au kukujulisha mambo yanayoendelea katika mazingira yanayokuzunguka hata kabla hujayakufikia..

Hebu tuchukue mfano unatembea barabarani kwa miguu na mbele yako umbali wa kama  mita 100 kuna moto mkubwa umewashwa….Sasa kwa kutumia macho yako mawili unaweza kuuona ule moto na kuepukana nao kabla hata hujaufikia…maana yake ni kwamba macho yamekupa uhakika ya hatari itarajiwayo kabla hujaifikia..

Hali kadhalika unaweza ukafumbwa macho lakini kwa kutumia masikio yako ukasikia sauti ya moto ukiteketeza kitu kwa mbali na hivyo ukachukua tahadhari katika hiyo njia unayoiendea kabla hata hujafika eneo la tukio…hapo napo masikio yamekupa uhakika wa hatari uliyopo mbele yako kabla hata hujaifikia.

Sio hilo tu!..unaweza kufumbwa macho na ukazibwa masikio lakini kwa kutumia pua yako unaweza kuunusa moto mita kadhaa mbele kabla hata hujaufikia…ukasikia harufu ya moshi na vitu vinavyoteketea na hata ukajua ni nini kinaungua kama ni takataka au miti au vitu vya plastiki n.k…Lakini ukajua kabisa kuwa kuna moto mkubwa mbele na hivyo ukajihadhari kabla hata hujafika eneo la tukio..

Na pia sio hilo tu peke yake…unaweza ukafumbwa macho, ukazibwa masikio na pua zako zisifanye kazi lakini kwa kutumia ngozi ukapata majibu yale yale ambayo pua, macho na masikio yaliyapata..kwa kutumia ngozi unaweza ukahisi joto linaongezeka kila unapozidi kukaribia tukio na hivyo ukachukua tahadhari aidha ya kusimama au kubadili njia au kuahirisha safari…Na hivyo ukapata uhakika wa hatari inayokuja…

Sasa huo ni mfano tu mmoja  mwepesi ambao umetumia hisia nne..ipo inayotumia hisia zote tano..sasa mfano huo ni unaonyesha ni namna gani inawezekana kabisa kulitambua jambo hata kabla halijafikiwa…ni utashi wa mwili ambao Mungu kamwekea kila mwanadamu kwamba kabla mabaya hayajamfikia kwa ghafla achukue tahadhari…na kama umechunguza Mungu hajamzuia mtu kuifuata hatari..alichofanya ni kumpa hisia za kuihisi kabla haijamfikia au hajaifikia…kujamzuia mtu kuingia kwenye moto unaowaka mbele yake…huo ni uchaguzi wa mtu binafsi…(ukikuta moto unawaka mbele yako na wewe ukajitupa juu yake, huo ni uchaguzi wako). Ukikaa kwenye reli na unaiona Treni inakuja kwa kasi na honi inapiga tangu mbali lakini hutaki kutoka pale, ni uchaguzi wako.

Hali kadhalika biblia imeyafananisha maisha yetu na safari…katika safari yetu ya maisha…Ni roho zetu ndizo zinazosafiri…Miili yetu ipo hapa hapa duniani, inazunguka katika shughuli za kila siku za maisha, lakini roho zetu zinasafiri…Na mbele ya safari yetu (yaani huko tunakoelekea) kuna mambo makubwa mawili 1) MOTO na 2) MBINGU.

Kama vile mwili ulivyo na hisia na Mungu kaziwekea roho zetu hisia vivyo hivyo…Na hisia hizo naamini pia zipo nyingi kama vile hisia za mwili zilivyo nyingi….Hizi hisia za roho ni kutusaidia tujue hatari au baraka zilizopo mbele yetu…na kuchukua uamuzi wa kuziendea au kuzikwepa.

Ndugu mbeleni kuna ziwa la moto…kama hujapewa macho ya kuiona kuzimu katika maono/ndoto, basi Mungu atakujulisha kwa masikio ya rohoni..katika maisha yako utasikia tu habari za kuzimu na ukali wake na zitakupa uhakika kabisa kwamba kuzimu ipo…Hiyo sauti ni lazima utaisikia katika maisha yako….Hali kadhalika kama hutaisikia sauti inayokupa uhakika ya kwamba unalisogelea ziwa la moto…basi utaisiki harufu ya kulikaribia ziwa la moto…na ndio maana katika Maisha yako ya ulevi, ya wizi, ya uasherati, ya kutomcha Mungu, kuna alamu fulani ndani inakuambia kabisa ukiendelea kuishi hivyo utaishia pabaya, hapo ni hisia ya harufu inafanya kazi yake katika roho yako..n.k N.K.

Lakini ukizipuuzia hizo hisia ndugu yangu..na kusema mimi siamini kama kuna kuzimu kwasababu sijawahi kuiona kwa macho…nakuambia ukweli hujawahi kuiona kweli kwa macho yako lakini umeisikia na kuihisi…macho yako yamefumbwa kweli lakini bado hisia nyingine zinakupa uhakika kwamba unaliendea ziwa la moto!…kwasababu huwezi kuuhisi moto mbele yako na kusikia harufu yake na kisha kuzama huko..na kujitetea kwamba hukuuona kwa macho!…ulipaswa uchukue tahadhari kwa kutumia hisia nyingine..ambazo zilikuwa zinakutahadharisha kwamba huko unakoelekea sio!

Ndugu KUZIMU IPO!..Na MBINGU pia IPO!..Ukisubiri uone ndipo uamini utapotea…

Nakushauri kama hujampa Kristo maisha yako au kama bado ni VUGUVUGU hebu chukua muda kasome mistari hii (Ufunuo 3:15-17)...na usiseme nitampa Kristo maisha yangu kesho au nitafanya mabadiliko kesho!…biblia inasema hujui yatakayozaliwa ndani ya siku moja…(Mithali 27:1)..maana yake ni kwamba hata leo unaweza ukafa ghafla au parapanda ya mwisho ikalia..Je utakuwa wapi??..Macho yako hayajaiona mbingu bado…lakini hisia nyingine zilikuambia mbingu ipo….Jiulize Unaposoma ujumbe huu hisia nyingine inakuambia nini?..Je utamlaumu nani siku ile utakapojikuta kwenye ziwa la moto milele?..

Dhambi inavutia sana..na shimo la kuzimu ni kama mtego…hata kabla hujaufikia vizuri ukisema utajikuta limekuvuta ghafla na kuzimu haishibi watu biblia inasema hivyo…Shetani hakupendi hata kidogo..anachokifanya ni kupeleka wengi kuzimu kwasababu anajua yeye hawezi kuokolewa tena!..hivyo anaona wivu kukuona wewe binti/kijana uliyezaliwa tu juzi kukuona utaishi milele..Hivyo geuka leo kwa dhati kama hujageuka, na ukatubu na kubatizwa na kupokea Roho Mtakatifu kabla wakati wa hatari haujafika. Mbinguni tumeandaliwa mambo mazuri sana, hata hisia zetu zimeshaanza kuzihisi.

Kumbuka aliyekabidhiwa mamlaka yote ya mbinguni na duniani (yaani Yesu Kristo) anakuja upesi…na anasema maneno haya…

Ufunuo 22.12 “Tazama, naja upesi, na ujira wangu u pamoja nami, kumlipa kila mtu kama kazi yake ilivyo.

13 Mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho, wa kwanza na wa mwisho.

14 Heri wazifuao nguo zao, wawe na amri kuuendea huo mti wa uzima, na kuingia mjini kwa milango yake.

15 Huko nje wako mbwa, na wachawi, na wazinzi, na wauaji, na hao waabuduo sanamu, na kila mtu apendaye uongo na kuufanya.

16 Mimi Yesu nimemtuma malaika wangu kuwashuhudia ninyi mambo hayo katika makanisa. Mimi ndimi niliye Shina na Mzao wa Daudi, ile nyota yenye kung’aa ya asubuhi.

17 Na Roho na Bibi-arusi wasema, Njoo! Naye asikiaye”

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

 Je! Ni sahihi kutumia maji ya upako,katika kufanya maombezi?

ZIKIMBIE TAMAA ZA UJANANI! NA MTU YEYOTE ASIUDHARAU UJANA WAKO.

USIPUNGUZE MAOMBI.

JE! PAKA KULIA USIKU NI ISHARA YA UCHAWI?

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
1 Comment
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Rowland,asante Robert
Rowland,asante Robert
4 years ago

Shalom pastr, naomba kutumiwa masomo kwa njia ya whatsap, +255 768 165 739