AINA TATU ZA WAKRISTO.

by Admin | 18 December 2020 08:46 pm12

Nakusalimu katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo. Karibu tujifunze maneno matukufu ya uzima, maadamu tumeiona leo.

Wakristo wameganyika katika makundi makuu matatu, makundi hayo yanafananishwa na miti ya matunda.

Na Miti ya matunda ipo ya aina tatu;

  1. Miti inayozaa matunda halisi
  2. Miti isiyozaa matunda yoyote
  3. Miti inayozaa matunda mwitu.

Hii Ndio ile miti ambayo Bwana Yesu aliizungumzia katika mfano ule mfano wa mpanzi, akasema mbegu zake ndio zile zilizopandwa katika udongo mzuri ambazo nyingine zilizaa 30 nyingine 60 nyingine 100 (Mathayo 13:8). Akasema hao ni wakristo ambao, walistahimili vishindo vyote vya ibilisi, kwa kuvumilia ndipo wakaweza kumzalia Mungu matunda.

Luka 8:15 “Na zile penye udongo mzuri, ndio wale ambao kwa unyofu na wema wa mioyo yao hulisikia neno, na kulishika; kisha huzaa matunda KWA KUVUMILIA”.

Walivumilia nini?

 Walivumilia  dhiki na udhia shetani alizowaletea kutokana na ukristo wao, waliweza kulitunza Neno la Mungu mioyoni mwao, kwa kutoruhusu  masumbufu ya maisha haya kuwaingilia sana, mpaka kuwafanya wasilitendee kazi Neno., Na kundi hili lipo dogo sana. Na Kristo ameahidi kulipalilia, na kulisafisha ili liendelee kumzalia zaidi. (Yohana 15:2)

Mfano wa miti huu, ndio ile ambayo Bwana Yesu aliutolea mfano huu;

Luka 13:6 “Akanena mfano huu; Mtu mmoja alikuwa na mtini umepandwa katika shamba lake la mizabibu; akaenda akitafuta matunda juu yake, asipate.

7 Akamwambia mtunzaji wa shamba la mizabibu, Tazama, miaka mitatu hii naja nikitafuta matunda juu ya mtini huu, nisipate kitu; uukate, mbona hata nchi unaiharibu?

8 Akajibu akamwambia, Bwana, uuache mwaka huu nao, hata niupalilie, niutilie samadi;

9 nao ukizaa matunda baadaye, vema! La, usipozaa, ndipo uukate”.

Hawa ni wakristo, ambao mara baada ya kuokoka, wana-relax, wanadhani wokovu ni kukiri tu kwa kinywa na kuamini, basi, na baada ya hapo unaendelea na mambo yako mwenyewe. Hawataki kujishughulisha kutafuta mambo ya rohoni baada ya kuamini na kubatizwa, licha ya kwamba, Mungu anawatia samadi kila siku kwa kuwafundisha na kuwahubiria njia zake, lakini wao hawaonyesha badiliko lolote, Hawapo kwenye maovu, wala hawapo kwenye mema. Lakini wakati wote, wanasikiliza Neno la Mungu na kulipokea, kundi hilo lipo kubwa sana.

Kristo ameahidi kutochukuliana nalo muda mrefu sana, utafika wakati litakatwa, na ukishakatwa, ndio habari yako imeishia hapo, unakuwa umekufa kiroho, haijalishi utasema niliokoka zamani. Bwana Yesu anatazamia, tunapookoka, tuonyeshe matendo yanayotendana na wokovu wetu, kuanzia huo wakati, tuwe waombaji, wafungaji, tuwaambie na wengine habari njema za wokovu, tuchangie kwa mapato yetu kazi ya Mungu isonge mbele, n.k. Lakini tukiwa sisi ni wa kupokea tu vya Mungu, lakini hatumtolei na yeye, tujue kuwa safari yetu haitakuwa ndefu.

Mfano wa miti hii, ndio kama huu Ambao Mungu aliizungumza katika Isaya sura ya 5.

Isaya 5:1 “Na nimwimbie mpenzi wangu wimbo wa mpenzi wangu katika habari za shamba lake la mizabibu. Mpenzi wangu alikuwa na shamba la mizabibu, Kilimani penye kuzaa sana;

2 Akafanya handaki kulizunguka pande zote, Akatoa mawe yake, Akapanda ndani yake mzabibu ulio mzuri, Akajenga mnara katikati yake, Akachimba shinikizo ndani yake; Akatumaini ya kuwa utazaa zabibu, Nao ukazaa zabibu-mwitu.

3 Na sasa, enyi wenyeji wa Yerusalemu, nanyi watu wa Yuda, amueni, nawasihi, kati ya mimi na shamba langu la mizabibu.

4 Je! Ni kazi gani iliyoweza kutendeka ndani ya shamba langu la mizabibu nisiyoitenda? Basi, nilipotumaini ya kuwa litazaa zabibu, mbona lilizaa zabibu-mwitu?

5 Haya basi, sasa nitawaambieni nitakalolitenda shamba langu la mizabibu; nitaondoa kitalu chake, nalo litaliwa; nitabomoa ukuta wake, nalo litakanyagwa;

6 nami nitaliharibu; wala halitapogolewa wala kulimwa, bali litamea mbigili na miiba; nami nitayaamuru mawingu yasinyeshe mvua juu yake.

7 Kwa maana shamba la mizabibu la Bwana wa majeshi ndilo nyumba ya Israeli, na watu wa Yuda ni mche wake wa kupendeza; akatumaini kuona hukumu ya haki, na kumbe! Aliona dhuluma; alitumaini kuona haki, na kumbe! Alisikia kilio”.

Kundi hili ndilo baya zaidi, kwasababu, ni kundi ambalo linazaa matunda ya upande mwingine,. Hawa ni wakristo ambao mara baada ya kuokoka, mara baada ya kukaa kanisani kwa muda mrefu, mambo wanayoyaonyesha kwa matendo yao ni kinyume kabisa na ukristo unavyopaswa uwe.. Utakuta mtu ni mzinzi wa muda mrefu, mwingine ni mtukanaji, mwingine ni mwizi, mwingine ni tapeli n.k. na bado  anasema nimeokoka, nimebatizwa, nimepokea Roho Mtakatifu, Yaani kwa ufupi yale mambo ambayo wanayafanya watu wa kidunia na yeye anayafanya, vivyo hivyo, hakuna tofauti yoyote.

Kundi hili nalo ni kubwa sana na Mungu  ameahidi kuliondolea kitalu chake (Kuliua)..

Tukiyajua hayo ni wajibu wako wewe kama mkristo kujichunguza ni kundi lipi unaloangukia, na matokeo yake mbeleni yatakuwaje, , Fahamu tu upo wakati mwenye shamba atakuja kukupeleleza,  Kwahiyo ni wajibu wako wewe kujua kuwa upo hapa duniani kwa malengo, na Mungu anatarajia kuona badiliko katika maisha yako katika kipindi alichokuweka hapa duniani. Kama upo miaka mingi katika wokovu na huoni kama kuna chochote unakifanya kinampendeza Mungu, au kinaisaidia injili yake isonge mbele, jiulize unaekea wapi? Je, ni wa Kukatwa au kupaliliwa. Jibu unalo, jibu ninalo.

Hivyo tubu ugeuke, umpokee Kristo kwa kumaanisha, na kuonyesha bidii katika kusoma Neno lake, kuomba, na kumfanyia ibada, ndipo utakapopata nguvu ya kumzalia yeye Matunda.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

MATUNDA 9 YA ROHO MTAKATIFU

TUTAWEZAJE KUMZALIA MUNGU MATUNDA?:

NAWE UTAGEUZWA KUWA MTU MWINGINE.

KUNA MAJIRA MUNGU ATAIVURUGA MIPANGO YETU.

JIFUNZE KUTOA KATIKA HAZINA YAKO VITU VIPYA NA VYA KALE.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/12/18/aina-tatu-za-wakristo/