Biblia ilimaanisha nini watu wasitoe vizazi vyao kwa Moleki?

by Admin | 6 March 2021 08:46 pm03

Moleki ni nani? Na Kwanini Mungu alikataza watu kutoa vizazi vyao na kuwapa Moleki?

Walawi 20: 1 Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia,

2 Tena uwaambie wana wa Israeli, Mtu awaye yote miongoni mwa wana wa Israeli, au miongoni mwa wageni waketio katika Israeli, atakayetoa katika kizazi chake na kumpa Moleki, sharti atauawa; wenyeji wa nchi watampiga kwa mawe.


Moleki ni mungu aliyeabudiwa katika nchi ya kaanani na nchi za kando kando, kama vile Amoni, mungu  huyu alikuwa tofauti na miungu mingine ya kipagani, kama vile Baali, kwani huyu, alihitaji kafara za watu ili kuwapa watu mahitaji yao. Walichokuwa wanakifanya ni kuwapitisha watoto wao katika moto na kuwatoa kafara.

Jambo ambalo Mungu aliwaonya na kuwakataza sana, wana wa Israeli tangu wakiwa jangwani, kabla hawajaiingia hiyo nchi ya ahadi kwamba watakapofika wasijihusishe na miungu hiyo ya uongo kwa namna yoyote ile, kwani Mungu alijua watu wake watakutana nayo.

Utalisoma hilo tena katika..

Walawi 18:21 “Nawe usitoe kizazi chako cho chote na kuwapisha kwa Moleki, wala usilinajisi jina la Mungu wako; mimi ndimi Bwana”.

Lakini pamoja na hayo, wana wa Israeli waliyakaidi maagizo ya Mungu wakaanza kuiga taratibu hizo za kishirikina za kuwatoa watoto wao kafara. Jambo hilo tunaweza kuona lilianzana  kwanza na mfalme Sulemani, ambaye ndiye aliyekuwa wa kwanza kabisa kumjengea madhabahu  mungu huyo katika Israeli, na hivyo ikawa chukizo kubwa sana. Na hiyo ndio ilikuwa sababu ya Mungu, kumshusha viwango mfalme Sulemani.

1Wafalme 11:7 “Sulemani akamjengea Kemoshi, chukizo la Wamoabi, mahali pa juu, katika mlima uliokabili Yerusalemu, na Moleki, chukizo la wana wa Amoni”.

Mambo hayo waliendelea kufanyika Israeli kwa kipindi kirefu, wengine wakidhani kuwa ni Mungu kaagiza, au kwamba Mungu ndio anavutiwa na kafara hiyo kuliko ya mbuzi na kondoo. Lakini hawakujua kuwa ni mambo ambayo yalikuwa ni machukizo makubwa sana kwa Mungu.

Yeremia 32:35 “Tena walijenga mahali palipoinuka kwa Baali, palipo katika bonde la mwana wa Hinomu, ili kuwapitisha wana wao na binti zao katika moto kwa ajili ya Moleki, jambo nisilowaagiza; wala halikuingia moyoni mwangu kwamba walitende chukizo hilo; wapate kumkosesha Yuda”.

Ni nini Bwana anataka tujifunze kwa watu hawa?

Kuchanganya desturi za miungu ya kipagani na ibada za Mungu muumba wa mbingu na nchi, ni mambo ambayo yanaendelea hata sasa hivi katika agano jipya.

Kwamfano kitendo cha kuweka sanamu za watakatifu walitaongulia, na kuabudu kupitia hizo, kufuatana na desturi zao, ambazo hazipo katika maandiko, ni machukizo makubwa sana. Kusali Rozari, ni machukizo kwa Mungu, vilevile kudhani kuwa wapo wapatanishi wengi kati ya Mungu na wanadamu, na Yesu ni mmojawapo tu ya wapatanishi hao,hayo ni makufuru mbele za Mungu. Kwani biblia inasema mpatanishi kati ya Mungu na mwanadamu ni mmoja tu, naye ni Yesu Kristo hakuna mpatanishi mwingine.

Hivyo ni lazima tuwe makini sana na tunachokiabudu, kwasababu hapo ndipo wivu wa Mungu unapolala. Tukijifanya hatuoni, tujue kuwa Mungu hatauvumilia upumbavu wetu, kama alivyofanya kwa wana wa Israeli. Kwasababu yeye mwenyewe ametuita tumwabudu katika Roho na Kweli na si katika ujinga na upagani.

Jina la Bwana libarikiwe.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

Maashera na Maashtorethi ni nini?

Je! Bikira Maria ni MALKIA WA MBINGUNI?

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 1

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 2

Vyombo vya uzuri ni vipi vinavyotajwa katika biblia?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/03/06/kwanini-mungu-alikataza-watu-kutoa-vizazi-vyao-kwa-moleki/