Je! kuna madhara kuchukiwa na kila mtu kwasababu huna mali?. Kama biblia inavyosema katika Mithali 14:20?.

by Admin | 3 June 2021 08:46 am06

Jibu: Tusome,

Mithali 14:20 “Maskini huchukiwa hata na jirani yake; Bali tajiri ana rafiki wengi”.

Na  pia

Mithali 19:4 Inasema  “Utajiri huongeza rafiki wengi; Bali maskini hutengwa na rafiki yake”.


Hizi ni Mithali ziliyoandikwa na Mfalme Sulemani, kwa hekima alizopewa na Mungu, na zipo Mithali nyingine nyingi alizoandika kwa mafunzo na maonyo. Lakini tofauti na inavyodhaniwa na wengi, Kuwa kila Mithali Sulemani aliyoiandika ilikuwa ni agizo! Hapana!. Sio kila mithali tunayoisoma katika kitabu cha Mithali ilikuwa ni agizo!. Mithali nyingi Sulemani alizoziandika zilikuwa zinahusu uhalisia wa jambo Fulani, na si agizo la jambo Fulani.

Kwamfano mimi leo nikisema “Watu wengi walio wapole wanaonewa na kudhulumiwa”. Hapo sijatoa agizo kwamba wapole wasiendelee kuwa wapole tena, waanze kuwa wakali na wakorofi. bali nimezungumza “uhalisia, jambo fulani ambalo lipo!”. Na huo umetokana na mimi kuchunguza mpaka nikaja na jawabu hilo.

Kadhalika Mithali nyingi Sulemani alizoziandika hazikuwa ni maagizo, bali ni uhalisia wa mambo fulani, ambayo yapo!!!  na huo unatokana na uchunguzi alioufanya!..Na mfano mmojawapo alioutoa ambao ulikuwa ni uhalisia na si agizo ndio huu tunaousoma..

Mithali 14:20 “Maskini huchukiwa hata na jirani yake; Bali tajiri ana rafiki wengi”.

Sasa hapa sio kwamba Sulemani, alitoa agizo kwamba.. “kuwa maskini watafute utajiri ili wawe na marafiki wengi”. Hapana hakumaanisha hivyo, Kwasababu ingekuwa ndivyo mbeleni asingekuja kusema tena haya maneno..

Mithali 28:6 “Afadhali maskini aendaye katika unyofu wake, Kuliko mpotofu wa njia angawa ni tajiri”

Umeona! alisema maneno kwasababu alichunguza na kuona kuwa Walikuwepo Maskini wenye busara na hekima, ambao katika haki yao yote bado hawakupendwa, walichukiwa… Na hapo hapo akaona walikuwepo matajiri wengi ambao katika udhalimu wao walipendwa na wengi. Jambo ambalo ni kawaida hata sasa, mtu aliye na mali hata kama ni mali za haramu atapata marafiki wengi!..(lakini ni marafiki wasiofaa)

Hebu tusome tena mahali pengine Sulemani alipochunguza jambo kama hilo..

Mhubiri 9:14 “Palikuwa na mji mdogo, na watu ndani yake walikuwa wachache; akaja mfalme mkuu juu yake, akauhusuru, akajenga ngome kubwa ili kuupiga.

 15 Basi, kulionekana humo MTU MASKINI MWENYE HEKIMA, naye kwa hekima yake akauokoa mji ule lakini hata hivyo HAPAKUWA NA MTU YE YOTE ALIYEMKUMBUKA YULE MTU MASKINI.

 16 NDIPO NILIPOSEMA, BORA HEKIMA KULIKO NGUVU; walakini hekima ya maskini hudharauliwa, wala maneno yake hayasikilizwi.

 17 Maneno ya wenye hekima yanenwayo taratibu husikiwa, Zaidi ya mlio wake atawalaye katikati ya wapumbavu.

18 Hekima NDIYO BORA KUPITA SILAHA ZA VITA; Lakini mkosaji mmoja huharibu mema mengi”

Umeona hapo?.. Sulemani anamsifu Maskini mwenye hekima, ambaye kwa hekima yake ameuokoa mji, anasema “Bora hekima kuliko nguvu, na hekima ni bora kuliko silaha za vita”.

Mithali 16:16 “Si afadhali kupata hekima kuliko dhahabu? Naam, yafaa kuchagua ufahamu kuliko fedha.

Na japokuwa anamwona maskini huyo hakumbukwi, wala hatapendwa na wengi, wala marafiki wengi, wala hakuna mtu aliyemkumbuka.. Lakini kwa hekima yake ameuokoa mji, na hivyo ipo thawabu yake baada ya maisha haya…

Mhubiri 4:13 “Heri kijana maskini mwenye hekima Kuliko mfalme mzee mpumbavu”.

Kwahiyo  ni vizuri kuzichambua vyema hekima za Sulemani na kuzielewa, kwasababu si kila kitu kilichoandikwa kule ni agizo!..

Tukirudi katika ukristo pia hatujaahidiwa kwamba tukimpokea Yesu tutakuwa na marafiki wengi, au ndio tutapendwa na watu wengi..la! kinyume chake ndio tutachukiwa.. Na kuchukiwa huko sio laana!, bali ndio muhuri wa wito wetu.

Luka 21:16  “Nanyi mtasalitiwa na wazazi wenu, na ndugu zenu, na jamaa zenu, na rafiki zenu, nao watawafisha baadhi yenu.

17  Nanyi mtachukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu”

Vile vile hatujaahidiwa kuwa tunapozaliwa mara ya pili ndio hatutapitia dhiki za hapa na pale.. vipindi vya dhiki vitakuwepo, lakini Bwana ameahidi kuwa atakuwa na sisi hatatuacha.

Bwana Yesu alisema maneno haya..

Ufunuo 2:9 “Naijua dhiki yako NA UMASKINI WAKO, (lakini u tajiri) najua na matukano ya hao wasemao ya kuwa ni Wayahudi, nao sio, bali ni sinagogi la Shetani.

10  Usiogope mambo yatakayokupata; tazama, huyo Ibilisi atawatupa baadhi yenu gerezani ili mjaribiwe, nanyi mtakuwa na dhiki siku kumi. Uwe mwaminifu hata kufa, nami nitakupa taji ya uzima”

Mathayo 16:2  “Watawatenga na masinagogi; naam, saa yaja atakapodhania kila mtu awauaye ya kuwa anamtolea Mungu ibada. Na hayo watawatenda kwa sababu hawakumjua Baba wala mimi”.

Bwana atubariki na kutusaidia.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

TENDA AGIZO LA YESU, HILO NDIO LITAKALOKULINDA.

LISHIKILIE SANA LILE AGIZO LA KWANZA.

Mego ni nini kama tunavyosoma katika biblia? (Mithali 17:1)

Mpumbavu ni nani katika biblia? (Zaburi 14:1, Mithali 10:14)

Nini maana ya Mungu amemfanya mwanadamu mnyofu?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/06/03/je-kuna-madhara-kuchukiwa-na-kila-mtu-kwasababu-huna-mali-kama-biblia-inavyosema-katika-mithali-1420/