NGUVU YA UPENDO WA KRISTO.

by Admin | 5 July 2021 08:46 pm07

Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe, karibu katika kuyatafakari maandiko.

Je! Umewahi kujiuliza kwanini biblia inasema upendo una nguvu kama mauti?.

Wimbo ulio bora 8:6 “Nitie kama muhuri moyoni mwako, Kama muhuri juu ya mkono wako; Kwa maana UPENDO UNA NGUVU KAMA MAUTI, Na wivu ni mkali kama ahera. Mwako wake ni mwako wa moto, Na miali yake ni miali ya Yahu”

Upendo wa Mungu kwetu! Unafananishwa na upendo wa Mtu kwa mpenzi wake. Jinsi mwanaume anavyompenda mke wake ndivyo Kristo anavyotupenda sisi. Na mtu anapozama sana katika upendo huwa anakitu kingine kinachofuatana na huo mpendo, na hicho si kingine zaidi ya Wivu!.. hivi vitu viwili ni Pacha!.. vinakwenda pamoja..

Kadhalika Kristo naye analipenda kanisa na sio tu analipenda bali pia analionea wivu. Endapo watu wake aliowapenda wakikengueka na kujitenga naye, basi wivu wake unawaka!, na kuweza kufanya lolote, kama vile mtu aliyesalitiwa na mke wake.

Lakini leo tutajifunza ni kwa namna gani upendo wa Kristo ulivyo na nguvu!.

Hapo biblia inasema “Upendo una nguvu kama mauti”. Maana yake tukiielewa nguvu ya mauti, basi tutaielewa nguvu ya upendo wa Kristo kwetu.

Kama tunavyojua Mtu anayekumbwa na Mauti, anakuwa haishi tena, anakuwa amepotea moja kwa moja, kumbukumbu lake linapotea duniani, hawezi kutenda jambo lolote wala shughuli yoyote ya huu ulimwengu.

Kadhalika mtu anayeingia na kuzama katika pendo la Kristo, ule upendo wa Kristo unamuua na mambo yote ya kidunia.. unamfanya anakufa kwa habari ya dhambi, anapotea kabisa kwenye dira ya mambo ya ulimwengu huu, anakuwa katika umoja na Kristo, ambao hakuna mtu anayeweza kuukaribia.. na hakuna kitu chochote kinachoweza kumtenga yeye na Kristo..

Warumi 8:33 “Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki.

34  Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.

35  Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga?”

Je  na wewe leo umeingia katika pendo la Mwana wa Mungu??..

Kumbuka huwezi kuushinda ulimwengu kama hutakufa kwa habari za uliwengu.

Yohana 15:9  “Kama vile Baba alivyonipenda mimi, nami nilivyowapenda ninyi, kaeni katika pendo langu.

10  Mkizishika amri zangu, mtakaa katika pendo langu; kama vile mimi nilivyozishika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo lake.

11  Hayo nimewaambia, ili furaha yangu iwe ndani yenu, na furaha yenu itimizwe”.

Ni kwanini leo hii huwezi kushinda ulevi?, ni kwasababu pendo la Kristo halijaingia ndani yako, ambalo lingeweza kuua nguvu yote ya ulevi, vile vile kwanini leo huwezi kuacha uzinzi, ukahaba, wizi, uuaji n.k?.. ni kwasababu bado Pendo la Kristo halijamiminwa ndani yako, ambalo lingekufanya ufe kwa habari ya dhambi ndio maana bado ulimwengu una nguvu juu yako.

Lakini habari njema ni kwamba, Kristo mpaka sasa yupo hai na anaokoa!.. utakapompokea kwa kumaanisha kutubu na kuacha dhambi, basi ataingia moyoni mwako, na lile pendo lake litaua kazi zote za ibilisi ndani yako, na kukuacha huru, na hutaona uzito wala ugumu katika kuishi maisha yanayompendeza Mungu. Kumbuka “UPENDO UNA NGUVU KAMA MAUTI”.

Hivyo ukitaka mauti katika kazi zote za ibilisi juu ya maisha yako, zama katika pendo la Kristo. Kwasababu Kristo mwenyewe hawezi kuruhusu wewe usumbuliwe na mambo ya ulimwengu huu!, hivyo lazima aue  kazi zote za ibilisi ndani yako..

Kama hujaingia katika pendo hili, basi tubu leo kwa kumaanisha kuziacha dhambi zako zote, na kisha tafuta ubatizo sahihi, ambao ni ule wa maji mengi na kwa jina la Yesu Kristo. Na kwasababu Kristo ni mwenye upendo, atakuingiza katika pendo lake na kukupa uzima wa milele.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Group la whatsapp Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp


Mada Nyinginezo:

JINSI YA KUEPUKA KUUMIZWA MOYO KUSIKOKUWA NA SABABU.

NITAUPATAJE UPENDO WA KI-MUNGU NDANI YANGU?

JE UPENDO WAKO UMEPOA?

WALA MSIUANGALIE MWILI, HATA KUWASHA TAMAA ZAKE.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/07/05/nguvu-ya-upendo-wa-kristo/