JE UPENDO WAKO UMEPOA?

JE UPENDO WAKO UMEPOA?

Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe. Karibu tuyatafakari Pamoja maandiko.

Kuna hili andiko ambalo ni maarufu sana kwetu, ambalo ni unabii Bwana alioutoa na kusema kuwa utatimia kipindi kifupi sana kabla ya kurudi kwake mara ya pili duniani.. Na neno hilo tunalisoma katika Mathayo 24:12 inasema;

“Na kwa sababu ya kuongezeka maasi, UPENDO WA WENGI UTAPOA”.

Sasa mpaka biblia imesema upendo wa wengi utapoa, maana yake ni kwamba hapo kwanza walikuwa na upendo thabiti kabisa uliokubaliwa na Mungu lakini sasa, hawanao tena…Na kwa haraka haraka ni rahisi kufikiri, kuwa upendo wa kwanza unaozungumziwa hapo, ni ule wa kupendana sisi kwa sisi, Ndio! Huo ni upendo lakini sio wa kwanza bali ni wa pili…, Jicho la Mungu, halikuuona upendo huo, bali liliona upendo mwingine ulio mkuu kupita huo, ambao ni upendo wa KUMPENDA MUNGU.

Marko 12.28 “………..Katika amri zote ni ipi iliyo ya kwanza?

29 Yesu akamjibu, YA KWANZA ndiyo hii, SIKIA, ISRAELI, Bwana Mungu wetu ni Bwana mmoja;

30 nawe MPENDE BWANA MUNGU WAKO KWA MOYO WAKO WOTE, NA KWA ROHO YAKO YOTE, NA KWA AKILI ZAKO ZOTE, NA KWA NGUVU ZAKO ZOTE.

31 Na ya pili ndiyo hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Hakuna amri nyingine iliyo kuu kuliko hizi”

Hivyo upendo wa Kwanza unaozungumziwa kwamba utapoa kwa watu wengi, katika siku za mwisho ni UPENDO WA KUMPENDA MUNGU KWA MOYO WOTE, AKILI ZOTE na NGUVU ZOTE. Na baada ya huo ndio unafuata upendano wa sisi kwa sisi.

Na hao “wengi” waliozungumziwa hapo…sio watu wa kidunia, kwasababu watu wa kidunia kwa kuanzia tu, tayari hawampendi Mungu….Bali hao “wengi” wanaozungumziwa hapo kwamba hapo kwanza walikuwa na upendo wa kumpenda Mungu lakini sasa UMEPOA ni “wakristo (Yaani wale ambao tayari walikuwa wamemwamini Yesu)”, hao ndio wengi wanaozungumziwa kwamba siku za mwisho upendo wao wa kumpenda Mungu utapoa…

Maana yake ni hii, kipindi karibia na unyakuo (ambacho kipindi ndicho hichi tuishicho), kutakuwa na jopo kubwa la wakristo wanaorudi nyuma…Na hiyo ni kutokana na kuongezeka kwa maasi duniani. Wakristo wengi watakuwa vuguvugu..

Mtu hapo kwanza alikuwa ni mwombaji, lakini ghafla anaacha kuwa mwombaji, anakuwa bize kutafuta mambo mengine, hapo kwanza alikuwa ni mhubiri, sasa ni mhubiri wa mambo maovu, hapo kwanza alikuwa ni mnyenyekevu mbele za Mungu, lakini sasa ni mwenye kiburi, hapo kwanza alikuwa analisoma Neno kwa bidii, na kuweza hata kugundua mitego na mahubiri madanganyifu, lakini sasa hawezi tena, hapo kwanza alikuwa anajitoa kwa tabu usiku na mchana kuhakikisha injili inakwenda mbele lakini sasa hafanyi hivyo tena, hapo kwanza alikuwa mvumilivu, sasa ni mtu mwenye hasira na visasi, hapo kwanza alikuwa anapiga mbio katika Imani bila kuchoka, lakini sasa amepoa, na kuzimia… Hawa ndio ambao upendo wao umepoa.

Ufunuo 2:2 “Nayajua matendo yako, na taabu yako, na subira yako, na ya kuwa huwezi kuchukuliana na watu wabaya, tena umewajaribu wale wajiitao mitume, nao sio, ukawaona kuwa waongo;

3 tena ULIKUWA na subira na kuvumilia kwa ajili ya jina langu, wala hukuchoka.

4 LAKINI NINA NENO JUU YAKO, YA KWAMBA UMEUACHA UPENDO WAKO WA KWANZA.

5 BASI, KUMBUKA NI WAPI ULIKOANGUKA; UKATUBU, UKAYAFANYE MATENDO YA KWANZA. Lakini, usipofanya hivyo, naja kwako, nami nitakiondoa kinara chako katika mahali pake, usipotubu”,

Katika Mstari huo wa 3, Bwana Yesu anasema…tena “ulikuwa na Subira na kuvumilia …” maana yake ni kwamba kwasasa huna tena hiyo Subira na huna uvumilivu tena, umerudi nyuma.

Lakini kwasababu Yesu ni wa rehema, anatoa ushauri. Urudi, ukatubu, UKAFANYE MATENDO YAKO YA KWANZA, (rudi kuwa mwombaji kama hapo mwanzo, rudi kuwa mvumilivu kama kwanza, hubiri Habari njema za ufalme kama ulivyokuwa unafanya hapo mwanzo, rudi kuwa mpole kama kwanza, n.k). Itakuwa heri.

Lakini usipofanya hivyo anasema, atakuja kukiondoa kinara chako mahali pake, kama usipotubu.

Kinara, ni chanzo cha NURU katika Maisha yako.  Kila mwanadamu, na kila kanisa na kila nchi inayo kinara cha taa yake. Hiyo ni kwaajili ya kumpa Nuru mtu, au kanisa au nchi. Na nuru hiyo ni ya rohoni na mwilini. Kikiondolewa hicho kinara juu ya mtu, anakuwa hawezi kwenda mbele katika Maisha yake ya rohoni na mwilini…kiza kinaingia katika Maisha yake ya rohoni na mwilini.

Kadhalika kinara kikiondolewa katika kanisa, kiza kinaingia, kanisa hilo linapoteza uelekeo na kupotea na Taifa ni hivyo hivyo.. Wana wa Israeli kuna kipindi kinara chao kiliondolewa na matokeo yake ni Taifa zima kuuawa kikatili na waliosalia kupelekwa utumwani Babeli.

Hivyo usikubali kurudi nyuma ndugu yangu, unayesoma ujumbe huu..Kumbuka kinara bado kipo katika maisha yako ndio maana unaona angalau bado kuna neema katika Maisha yako, lakini usipuridi katika mstari uliouacha, upo hatarini kuingia gizani.Ukizingatia hizi ni nyakati za maasi kuzidi ulimwenguni.

Bwana akubariki

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312 Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mada Nyinginezo:

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments