Naomba kujua nini maana ya kuteguka uvungu wa paja?

Naomba kujua nini maana ya kuteguka uvungu wa paja?

SWALI: Yakobo aliposhindana na Malaika alishikwa uvungu wa paja akateguka…Naomba kujua nini maana ya kuteguka uvungu wa paja?

Mwanzo 32:24 “Yakobo akakaa peke yake; na mtu mmoja akashindana naye mweleka hata alfajiri.

25 Naye alipoona ya kuwa hamshindi, alimgusa panapo uvungu wa paja lake; ukateguka uvungu wa paja la Yakobo alipokuwa akishindana naye.

26 Akasema, Niache, niende, maana kunapambazuka. Akasema, Sikuachi, usiponibariki.

27 Akamwuliza, Jina lako n’nani? Akasema, Yakobo.

28 Akamwambia, Jina lako hutaitwa tena Yakobo, ila Israeli, maana umeshindana na Mungu, na watu, nawe umeshinda”.


Jibu: Uvungu wa paja, ni eneo la juu ya paja ambapo mfupa wa paja umekutana na ule wa kiuno. Kama tunavyosoma hapo Yakobo baada ya kushindana na Yule malaika kwa masaa mengi sana usiku kucha bila kuwa na dalili yoyote ya kumwacha, tunaona biblia inatuambia Yule malaika, alimtengua uvungu wa paja lake.

Kumbuka kutegua/kutengua ni tofauti na kuvunja,..Kitu kikivunjwa maana yake ni kinaharibiwa, kinahitaji kuunganishwa, lakini kikitenguka maana yake ni kinahama eneo lililopo kwa muda tu.. Hivyo kwa namna ya kawaida mwanadamu maeneo yote ambayo mifupa miwili inakutana huwa ni rahisi kutenguka, husani pale anapoanguka sehemu ndefu, au kubanwa au kuvutwa kwa nguvu mahali penye maongeo,  kwa mfano goti, au viwiko vya mikono au miguu, vidole, bega au kwenye paja..  Na huwa inaambatana na maumivu makali sana, ambayo maumivu yake yanafanana tu ya yale ya kuvunjika, wakati mwingine yanamfanya mtu asindwe kabisa kutembea kama sio kuchechemea, na mpaka yaishe inaweza kuchukua wiki mbili mpaka tatu au Zaidi.

Sasa Yakobo yeye, alitenguliwa kwenye huu mfupa mkubwa wa paja, ambao ndio mkubwa na maumivu yake ndio  makali kushinda yote.

Lakini kwanini Mungu afanye vile, Ni jambo gani tunajifunza hapo?

Baraka za Mungu ni za kuzipigania, na sio hilo tu, bali pia zinaambatana na maumivu.. Ukitaka Mungu akubariki kubali kukutana na mapigano na maumivu  fulani, Jina la Israeli halikuja hivi hivi, lilikuwa ni la jasho na maumivu. Vivyo hivyo na sisi, tusikubali kuambiwa njoo, ubarikiwe, na huku, hatutaki kusikia gharama za kubarikiwa, ambazo ni kuishi maisha ya kubarikiwa.

Maisha ya kubarikiwa ni kama haya:

Bwana Yesu alisema Mathayo  6:38 “Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa”.

Lakini kama ulichonacho unajilimbikizia wewe tu mwenyewe, Na hapo hapo bado unataka nawe pia ubarikiwe, hilo jambo halipo!. Ipo mifano mingi sana..Ikiwa humtolei Mungu, tena kile kinachokugharimu kabisa, mpaka unaona maumivu rohoni, ni ngumu kubarikiwa na Mungu.

Si wakati wote unahitaji kuomba ili Mungu akuone, unahitaji kufanya zaidi..Pale ulipo unaanza, Mtume Yohana alimwambia Gayo, maneno haya 1Yohana 1:2 “Mpenzi naomba ufanikiwe katika mambo yote na kuwa na afya yako, kama vile roho yako ifanikiwavyo”.

Utajiuliza huyu Gayo ni nani, kwanini hakumwandikia kila mtu waraka ule wa mafanikio, bali Gayo tu peke yake, Hivyo ukitaka kujua ni kwanini alimwandikia yeye na si wengine, nenda kasome sura ile yote ujue ni mambo mangapi alijitoa kwa Mungu katika kuwahudumia watakatifu na kuwakaribisha wageni wale waliokuwa wanasafiri kuipeleka injili na kuwapatia mahitaji yao, mpaka sifa zake zikavuma katika kanisa lote.. Hapo ndipo Mtume Yohana kwa uongozo wa Roho Mtakatifu akaongozwa kumwandikia maneno  yale ya baraka.

Lakini hiyo ilikuwa ni mashindano na maumivu makali ya kuinyima nafsi yake.

Vivyo hivyo na sisi, tukumbuke kuwa Baraka za Mungu zitaambatana na kutenguliwa miguu yetu..Kama tupo tayari kwa hayo basi tuingie mapambano, Na tunaingia mapambanoni, sio kwa maneno bali kwa matendo.

Bwana atubariki sote, katika safari yetu ya imani.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

https://wingulamashahidi.org/ushirikina-na-madhara-yake/

NI NANI ATAKAYETUTENGA NA UPENDO WA KRISTO?

Nifanye nini ili niishi maisha ya ushindi siku zote?

Nyamafu ni nini?

“Ninyi ni chumvi ya dunia” Andiko hilo lina maana gani?

HISTORIA YA ISRAELI.

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments