KU WAPI, EWE MAUTI, KUSHINDA KWAKO?

by Admin | 2 August 2021 08:46 am08

Ipo siku moja mauti itashindwa kabisa kabisa…

Siku moja tutavikwa miili mipya ya utukufu!, katika siku hiyo, parapanda ya Mungu italia, na wote tuliomwamini Yesu, tulio hai..kama hatutakufa mpaka siku ile ya kurudi kwake, basi tutamwona Bwana akitokea mawinguni, na kisha wafu waliopo makaburini nao pia wataisikia sauti ya parapanda, na wao pia watafufuka.

Katika siku hiyo, kama mtu alikufa katika udhaifu fulani labda alikufa akiwa kiwete, au kiziwi au kipofu, au alikufa na ugonjwa wa kansa, lakini alikuwa ndani ya Imani, basi atafufuliwa na kurudi katika mwili wake, akiwa mzima kabisa, akiwa si kipofu tena, wala si kiziwi tena, wala si kiwete tena, wala si mgonjwa tena, kama mtu alikufa na Kisukari, basi atafufuliwa bila huo ugonjwa..

Siku hiyo kama vile Bwana alivyomfufua Lazaro ambaye alikufa pengine katika ugonjwa Fulani uliomsababishia mauti, lakini alipofufuliwa alifufuka katika uzima! Hakuwa na huo ugonjwa tena, vinginevyo angerudia kufa tena wakati ule ule!, kadhalika kabla ya kufufuliwa alikuwa kaburini ananuka, lakini baada ya kufufuka ile harufu ilipotea!, vinginevyo asingeweza kuishi na watu tena..

Hivyo ndivyo itakavyokuwa siku ile.. Wote waliokufa katika dhiki zao watafufuliwa katika uzima, wote waliokufa katika huzuni watafufuliwa katika ushindi na amani.. na baada ya kuvikwa miili mipya ya utukufu wataimba maneno haya… KU WAPI! EWE MAUTI KUSHINDA KWAKO?, KU WAPI EWE MAUTI KUSHINDA KWAKO??… MAUTI IMEMEZWA KWA KUSHINDA.

Ni kweli walikufa katika udhaifu wao, lakini tumaini la ufufuo walikuwa nalo!. Kwamba siku moja wataishinda mauti, watarudi tena kuwa hai na hawatakufa tena!

1Wakorintho 15:51 “ Angalieni, nawaambia ninyi siri; hatutalala sote, lakini sote tutabadilika,

52  kwa dakika moja, kufumba na kufumbua, wakati wa parapanda ya mwisho; maana parapanda italia, na wafu watafufuliwa, wasiwe na uharibifu, nasi tutabadilika.

53  Maana sharti huu uharibikao uvae kutokuharibika, nao huu wa kufa uvae kutokufa.

54  Basi huu uharibikao utakapovaa kutokuharibika, na huu wa kufa utakapovaa kutokufa, hapo ndipo litakapokuwa lile neno lililoandikwa, MAUTI IMEMEZWA KWA KUSHINDA.

55  Ku wapi, Ewe mauti, kushinda kwako? U wapi, Ewe mauti, uchungu wako? ”

Swali la kujiuliza kwa wewe uliye nje ya wokovu, au uliye vuguvugu, siku hiyo utakuwa wapi wakati watakatifu wanafufuliwa na kuvikwa kutokuharibika??. Kwasababu watakaoshinda mauti si wote!, bali ni wale waliokufa katika Kristo tu!, walioyatakasa maisha yao walivyokuwa duniani.

Je umempokea Yesu? Je unauhakika siku ile, utaishinda mauti? kwa kufufuliwa na kuingia katika uzima??..au Kama ukikutwa ukiwa hai, utanyakuliwa na kwenda na Bwana mawinguni?.. Kuna huna uhakika sana, basi tayari huo ni uthibitisho kuwa hutaishinda mauti?, hutafufuliwa siku ile Bwana atakapokuja, na hata kama akija na kukukuta hai katika hali uliyopo hutanyakuliwa, badala yake utabaki na kukutana na dhiki kuu ya mpinga kristo na kufa katika ile siku ya Bwana.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

NGUVU YA UPENDO WA KRISTO.

Bwana Yesu alikufa akiwa na umri gani?

INJILI YA MANENO LAINI ITAKUGHARIMU.

Ahera ni wapi? Kama tunavyosoma katika biblia.

Nini maana ya “Ulipo mzoga, ndipo watakapokutanika tai?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/08/02/ku-wapi-ewe-mauti-kushinda-kwako/