USIWE NA HAKI KUPITA KIASI.

by Admin | 25 December 2019 08:46 am12

Shalom mtu wa Mungu karibu tujifunze Biblia…Neno la Mungu linatuambia katika kitabu cha.. Mhubiri 7:16 “Usiwe na haki kupita kiasi; Wala usijiongezee hekima mno; Kwani kujiangamiza mwenyewe?”.  Maana yake ni nini?

Hapo kuna maswali machache tunayoweza kujiuliza….Je ni kwanini inasema hivyo?..Kwani kuna ubaya gani kuwa mwenye haki kupita kiasi…Mbona ndio vizuri Zaidi kuwa mwenye haki kupita kiasi kuliko kuwa mwovu au kuwa mwenye haki kidogo?.

Ni kweli tukiusoma mstari huo kwa mantiki hiyo tunaweza kuchanganyikiwa na kuona kama biblia inajichanganya kuona sehemu moja inatuasa tuwe wenye haki na hapa inatuambia tusiwe wenye haki kupita kiasi….Lakini ukweli ni kwamba Biblia ni kitabu kilichohakikiwa na Roho wa Mungu aliye mmoja tu asiyeweza kukosea wala kufanya masahihisho..Na huyo sio mwingine zaidi ya Mungu aliyeziumba Mbingu na nchi, aliyefunuliwa ndani ya YESU KRISTO (Waebrania 1;1-2, 2Wakorintho 5:19).

Huyo hawezi kukosea embu jaribu kifiria tangu hii dunia iumbwe jua halijawahi kukosea majira yake, kwamba siku moja lichelewe lisionekane upande mmoja, au siku siku nyingine liwahi kupambazuka, miaka nenda rudi, majira yake hayabadiliki, hiyo ni kuthibitisha kuwa kazi ya Mungu haijawahi kuwa na mapungufu hata kidogo, siku zote sisi ndio tunaotazama mzunguko wa jua ili kurekebisha majira yetu, na sio jua kututegemea sisi…miungu mingine iliyotengenezwa kwa mchanga na ngano, na chokaa na vipande vya kuni hiyo ndiyo inaweza kukosea lakini si Mungu wetu Yehova tunayemwabudu kupitia Yesu Kristo kwake hakuna mapungufu..

Biblia iliposema tusiwe na haki kupita kiasi ilimaanisha…

“Tusiwe watu wa kujihesabia haki mno!”..Mtu anayejihesabia haki mno anakuwa na kiburi na kuishia kudharau wengine wote na kujiona yeye ni bora kuliko wengine..

Bwana Yesu aliwaona mafarisayo na masadukayo kwamba ni watu wenye kujihesabia haki mno.

Luka 18:9 “ Akawaambia mfano huu watu waliojikinai ya kuwa wao ni wenye haki, wakiwadharau wengine wote.

10  Watu wawili walipanda kwenda hekaluni kusali, mmoja Farisayo, wa pili mtoza ushuru.

11  Yule Farisayo akasimama akiomba hivi moyoni mwake; Ee Mungu, nakushukuru kwa kuwa mimi si kama watu wengine, wanyang’anyi, wadhalimu, wazinzi, wala kama huyu mtoza ushuru.

12  Mimi nafunga mara mbili kwa juma; hutoa zaka katika mapato yangu yote.

13  Lakini yule mtoza ushuru alisimama mbali, wala hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni, bali alijipiga-piga kifua akisema, Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi.

14  Nawaambia, huyu alishuka kwenda nyumbani kwake amehesabiwa haki kuliko yule; kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa”.

Umeona?..Haki yetu haipaswi kuzidi mipaka hiyo hadi kufikia hatua ya kujikweza na kuwa na kiburi na kuwadharau wengine wote…Elimu yetu ya dini isitufanye tujione tu wenye haki kuliko wengine wote…karama zetu zisitufanye tujione sisi ni bora mbele za Mungu kuliko wengine wote…hata usafi na utakatifu tulio nao usizidi mipaka ya kujiona tu wenye haki saana!..tukifanya hivyo tutakuwa tu wenye haki kupita kiasi. Kadhalika kama tuna hekima ya ki-Mungu basi tusijione ni wenye hekima sana ya Neno la Mungu kiasi kwamba hakuna kama sisi, wala hakuna mtu yeyote anayeweza kutuongezea  kitu…tukifanya hivyo tutakuwa tumejiongezea hekima kupita kiasi!..na hivyo tutajiangamiza wenyewe.

Mhubiri 7:16 “Usiwe na haki kupita kiasi; Wala usijiongezee hekima mno; Kwani kujiangamiza mwenyewe?”.

Mafarisayo na Masadukayo walijiangamiza wenyewe kwa haki yao iliyozidi na kujiona kwao wanajua maandiko kuliko wengine wote..Mwishowe wakajikuta badala ya kumwamini Mwokozi wa ulimwengu wakajikuta wanampinga na hata kwenda kumwua.

Kadhalika wewe ni Mchungaji, au Nabii au Mhubiri au Mwalimu au Una Neno la Hekima na Maarifa, au una karama ya uponyaji, au Imani au miujiza au ni Muumini ambaye kuna Neema ya kipekee ambayo Mungu kakukirimia ambayo inaweza kukutofautisha wewe na wengine kwa sehemu Fulani au popote pale ulipo…Neno hili usilisahau…“USIWE MWENYE HAKI KUPITA KIASI”. Kila siku jione wewe si kitu mbele za Mungu..ni kwa Neema tu za Mungu upo kama ulivyo na si kwa haki yako..wala kwa nguvu zako binafsi,. Haki yako isizidi mipaka na kujiona ni kwa jitihada zako umestahili kuwa hivyo ulivyo..Hakuna anayestahili hata mmoja wote ni makapi tu! tumechaguliwa na kuokolewa kwa Neema..hivyo hakuna cha kujisifia..

Waefeso 2:8  “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; 9 wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu”

Bwana akubariki.

Kama bado hujaokoka!..Dunia  hii inakwenda kuisha..Kipindi sio kirefu sana Dunia itakwenda kushuhudia mabadiliko makubwa ya ghafla!..Ghadhabu ya Mungu itamwagwa duniani kote na wale wote waliomkataa Mwana wa Mungu Yesu Kristo, wataangamizwa kwa maangamizo makubwa yasiyoelezeka kasome Ufunuo 16. Hivyo unyakuo upo karibuni sana kutokea ambapo watakatifu (Yaani wale wote waliompokea Yesu Kristo na kuishi maisha ya utakatifu) watanyakuliwa na kwenda mbinguni kwa Bwana kuipisha ghadhabu hiyo kupita. Je wewe utakuwa wapi?..kama leo hii bado unamkataa Kristo?..kama leo hii bado ni mlevi, ni mwasherati, mtazamaji wa picha chafu, mchatiji wa mambo machafu mitandaoni, mfanyaji masturbation, mtukanaji, mtoaji mimba, mvaaji nusu uchi, mpakaji malipstick, mvaaji mawigi, masuruali n.k?..Siku hiyo utakuwa wapi?

Leo isikupite kabla hujageuka, biblia inasema saa ya wokovu ni sasa..Unachopaswa kufanya hapo ulipo ni kujitenga peke yako, na kupiga magoti na kuomba toba mbele za Mungu..Mwombe Mungu akusamehe dhambi zako leo..na yeye ni mwaminifu atakusamehe..Baad a ya Toba hiyo anza leo kubeba msalaba wako na kumfuata Kristo..Futa leo miziki yote ya kidunia iliyopo kwenye simu yako na picha zote za uchafu pamoja na namba za wanaume/wanawake uliokuwa unachat nao..kadhalika kachome nguo zote fupi ulizonazo pamoja na vipodozi vyote na suruali..baki kama ulivyo katika uhalisia wako. Na mambo mengine yote yasiyompenda Mungu uliyokuwa unayafanya.

Ukishafanya hivyo..basi utakuwa umemwonyesha Kristo kwamba umeamua kweli kumfuata yeye kwa matendo yako..Na yeye akishaona hivyo..Neno lake linasema “Yoyote ajaye kwangu sitamtupa nje kamwe Yohana 6:37”. Hivyo atakuwa na wewe na utasikia Amani ya ajabu ambayo hujawahi kuisikia hapo kabla..

Na baada ya kumgeukia Yesu kwa vitendo namna hiyo..haraka sana katafute mahali ambapo unaweza kuukulia wokovu..na pia kubatizwa kama hukubatizwa..Kumbuka Ubatizo sahihi ni muhimu na ni ule wa maji mengi (Yohana 3:23) na wa Jina la Yesu Kristo (Matendo 2:38). Na Roho Mtakatifu ndani yako atakusaidia kupembua mema na mabaya baada ya hapo na kuendelea..atakuongoza mpaka kufikia utimilifu na Zaidi ya yote atakuwezesha kushinda dhambi na vishawishi vyote vya huu ulimwengu, na yale mambo maovu yaliyosalia ndani yako ambayo kwa nguvu zako ulishindwa kuyaondoa, yeye atayashughulikia yote..

Ukifanya hivyo kwa dhati kabisa utakuwa umezaliwa mara ya pili..na kuwa miongoni mwa wateule wapendwao na Bwana..Na hata unyakuo ukipita leo, nawe utakuwa miongoni mwa wale watakokwenda kuishuhudia karama ya mwana-kondoo ambayo Kristo alikuwa amekwenda kutuandalia kwa miaka elfu mbili sasa.

Maran atha.

Tafadhali share na kwa wengine


Mada Nyinginezo:

CHACHU YA MAFARISAYO NA CHACHU YA HERODE.

NGUVU ILIYOPO KATIKA MAAMUZI.

NYAKATI SABA ZA KANISA NA WAJUMBE WAKE.

DUNIANI MNAYO DHIKI.

kanisa la kwanza duniani ni lipi?

IELEWE SAUTI YA MUNGU.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/12/25/usiwe-na-haki-kupita-kiasi/