JE MOYO WAKO NI MNYOFU MBELE ZA MUNGU

by Admin | 12 March 2020 08:46 pm03

Shalom, Nini kinachokufanya umfuate Yesu au uende kanisani?..Je moyo wako ni mnyofu mbele za Mungu?

Katika biblia, Agano jipya tunamsoma Mchawi mmoja aliyeitwa Simoni, ambaye alikuwa akifanya uchawi, na kuwadanganya watu, mpaka watu wakaamini kuwa anatumiwa na Mungu kufanya ishara zile, na alijigamba kuwa yeye ni Mtu Mkubwa (wa Mungu)...mpaka mji wote ukadanganyika na kumwamini. Lakini huyu Simoni aliposikia injili aliamini na akabatizwa…Lakini Nia yake ya ndani haikuwa kugeuka na kuacha dhambi zake za uchawi bali kuongeza nguvu zake za kichawi..Yaani maana yake alimwamini Yesu, ili apate kuongeza nguvu za kufanya miujiza na si kwasababu anautaka wokovu.

Ndugu mpendwa kigezo cha mtu kumkiri Yesu au kubatizwa sio tiketi pekee ya kukubaliwa na Bwana Yesu. Linahitajika jambo lingine na ziada, nalo ni “badiliko la kweli la ndani”.

Huyu Simoni mara ya kwanza alikuwa ni mchawi ambaye alijifanya ni mtumishi wa Mungu, lakini baadaye alipoona ukristo umeingia mahali pale akaona sasa ameshapata vazi jipya la kufunika kazi yake hiyo ya uchawi.

Hebu soma kwa makini habari ifuatayo usiruke kipengele hata kimoja…

Matendo 8:9 “Na mtu mmoja, jina lake Simoni, hapo kwanza alikuwa akifanya uchawi katika mji ule, akiwashangaza watu wa taifa la Wasamaria, akisema ya kuwa yeye ni mtu mkubwa.

10  Wote wakamsikiliza tangu mdogo hata mkubwa, wakisema, Mtu huyu ni uweza wa Mungu, ule Mkuu.

11  Wakamsikiliza, kwa maana amewashangaza muda mwingi kwa uchawi wake.

12  Lakini walipomwamini Filipo, akizihubiri habari njema za ufalme wa Mungu, na jina lake Yesu Kristo, wakabatizwa, wanaume na wanawake.

13  Na yeye Simoni mwenyewe aliamini akabatizwa, akashikamana na Filipo; akashangaa alipoziona ishara na miujiza mikubwa inayotendeka

14 Na mitume waliokuwako Yerusalemu, waliposikia ya kwamba Samaria imelikubali neno la Mungu, wakawapelekea Petro na Yohana;

15  ambao waliposhuka, wakawaombea wampokee Roho Mtakatifu;

16  kwa maana bado hajawashukia hata mmoja wao, ila wamebatizwa tu kwa jina lake Bwana Yesu.

17  Ndipo wakaweka mikono yao juu yao, nao wakampokea Roho Mtakatifu.

18  Hata Simoni alipoona ya kuwa watu wanapewa Roho Mtakatifu kwa kuwekewa mikono ya mitume, akataka kuwapa fedha akisema,

19  Nipeni na mimi uwezo huu, ili kila mtu nitakayemweka mikono yangu, apokee Roho Mtakatifu.

20  Lakini Petro akamwambia, Fedha yako na ipotelee mbali pamoja nawe, kwa kuwa umedhania ya kuwa karama ya Mungu yapatikana kwa mali.

21  Huna fungu wala huna sehemu katika jambo hili, kwa kuwa MOYO WAKO SI MNYOFU MBELE ZA MUNGU.

22  Basi, tubia uovu wako huu, ukamwombe Bwana, ili kama yamkini, usamehewe fikira hii ya moyo wako.

23  Kwa maana nakuona u katika uchungu kama nyongo, na tena u katika kifungo cha uovu”

Sasa watu wa namna hii wapo wengi katika kanisa. Hususani katika hizi siku za mwisho, ambapo kwa asili ni waganga wa kienyeji, wengine ni wachawi wana mapepo ya utambuzi na bado wanazipenda kazi zao za kuagua, zinawapatia faida nyingi..hivyo wanapouona ukristo wa kweli unahubiriwa wanaona kama ni vazi jipya na hivyo wanakwenda kubatizwa na kusimama mimbarani kuendelea na uaguzi wao, wengine sio wachawi lakini ni wanasiasa tu ambao wanaona wakifanya siasi kwa vazi la uanasiasa hawafikii kirahisi malengo yao, hivyo wanajigeuza na kuwa wakristo ili waendeleze siasa zao katika madhabahu ya Mungu.

Na sio tu kwenye eneo zima la utumishi, bali hata walio waumini, wapo wengine wengine wanakwenda tu kanisani kwasababu wanashida ya wachumba kwasababu wameambiwa wachumba wazuri watawapata kanisani, lakini mioyoni mwao hawana habari na Kristo. Wanakubali kubatizwa kuwasababu wamesikia kwa kufanya hivyo mambo yao ya kimaisha yataenda sawa, kama tu huyu Simoni mchawi.

 Wengine wanakwenda tu kwasababu ni siku nyingi hawajaenda kanisani, hivyo wanataka angalau waende mara moja moja kwa mwezi au mwaka, lakini ndani ya mioyo yao hawana nia na Mungu wala hawana mpango wa kubadilisha mtindo wa Maisha yao na kufanyika kiumbe kipya kwasababu mioyo yao sio minyoofu mbele za Mungu.

Wengine wanakwenda kwa nia tu ya kuonyesha mavazi yao, kila wanaponunua vazi jipya, wanawaza ni wapi watakwenda kujionyesha?..wanagundua ni kanisani..Hivyo kanisa ni kama kioo chao,…wengine wanapenda tu kukusanyika kwenye jumuiya ya watu wengi hawapendi kukaa wenyewe wenyewe, wanapenda kwenda kusikiliza vichekesho na kupata burudani za nyimbo za kwaya..wengine wanapenda kufanyiwa uaguzi, akipitia vita kidogo, au hasara kidogo katika Maisha yake  anakwenda kumtafuta mbaya wake kwa waganga wa kienyeji..sasa akipata kanisa ambalo linatoa huduma kama hizo ndipo anapokita mizizi hapo lakini yeye hana mpango na kumwondoa Adui mkubwa wa dhambi katika Maisha yake.

Sasa kundi lote hili ndio linalojumuisha “Manabii na Makristo wa uongo watakaotokea siku za mwisho”…Wengi wanafikiri Manabii wa uongo ni wale tu wanaosimama pale madhabahuni na kujiita manabii…hapana sio hao tu, hata wachungaji wasio na nia ya Kristo biblia inawaita manabii wa uongo, hata waalimu wanaopotosha biblia inawapa jina moja hilo hilo ambalo ni manabii wa uongo, hata waimbaji walio kinyume na Neno la Mung una wanaopotosha watu wa nyimbo zao na mavazi yao na Maisha yao..jina lao ni hilo hilo “manabii wa uongo au makristo wa uongo”..

Hali kadhalika hata Waumini ambao wanakwenda kanisani kwa nia ambayo sio ya Kristo mioyoni mwao jina lao ni hilo hilo “manabii wa uongo na makristo wa uongo” kwasababu wanawadanganya watu wa nje na waumini wenzao walio waaminifu kwamba wameokoka kumbe ndani hawana nia ya Kristo. Hivyo manabii wa uongo ni jina la ujumla..kuwafunua wale wote ambao wanajifanya wana uhusiano na Imani ya Kikristo na kumbe ndani yao ni maadui wa Msalaba.

Je na wewe upo kwenye kundi gani?..la makristo wa uongo au wa kweli?..Kama unakwenda kanisani kwasababu ya kutafuta majumba, mke au mali…wewe sio nabii wa uongo???…Je uasherati umeuacha?, je matusi umeyaacha, rushwa umeziacha, wizi umeuacha?, usengenyaji umeuacha?, kuishi na mwanamke/mwanamume ambaye humjafunga ndoa bado unaendelea kuishi naye?, ..kama bado hujaacha hayo yote kwanini unajiita mkristo?..huoni kama wewe utakuwa ni mkristo wa uongo?..uliyetabiriwa kutokea siku za mwisho?, ambao mtawadanganya wengi?..

Unatoa fedha nyingi kanisani ili upokee baraka kwenye kazi yako haramu ya uuzaji wa pombe..wewe una tofauti gani na huyu Simoni mchawi ambaye anataka kuwapa fedha wakina Petro ili na yeye awe na uwezo wa kuwawekea watu mikono washukiwe na nguvu za Mungu..Lakini wakina Petro walimwambia..

“20  Lakini Petro akamwambia, Fedha yako na ipotelee mbali pamoja nawe, kwa kuwa umedhania ya kuwa karama ya Mungu yapatikana kwa mali.

21  Huna fungu wala huna sehemu katika jambo hili, kwa kuwa MOYO WAKO SI MNYOFU MBELE ZA MUNGU.”

Lakini pamoja na hayo, pengine ulifanya hayo yote pasipo kujua…ulikuwa unakwenda kanisani nusu uchi kwasababu hukupata kufahamu kuwa unafanya dhambi, ulikuwa unafanya biashara haramu na huku unakwenda kutafa baraka kwa kazi hiyo kanisani kwasababu ulikuwa hujui. Kristo anakupenda na bado unauwezo wa kutengeneza upya na kuwa kipenzi cha Mungu..Unachopaswa kufanya ni kutubu tu!..Toba ni kila mtu anatubu, haijalishi ni mchungaji, mwalimu, au Nabii..wote tunatubu..na Mungu anapendezwa na mtu mwenye kunyenyekea..

Hivyo tubia mambo hayo yote kama ulikuwa unayafanya..na kisha usiyafanye tena..Baada ya kutubu na kudhamiria kuanza Maisha mapya na Kristo, nenda katafute ubatizo sahihi mahali popote ili upate kukamilisha wokovu wako, kumbuka ubatizo ni muhimu, na ni lazima uwe wa Maji tele (Yohana 3:23) na kwa jina la Yesu Kristo (Matendo 2:38).

Na moyo wako utakuwa mnyofu mbele za Bwana na utafanyika kuwa mwanafunzi wa kweli wa Yesu, na Roho Mtakatifu mwenyewe atakuongoza kufanya yaliyosalia.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

YUDA ISKARIOTE! MTUME ALIYECHAGULIWA NA BWANA YESU.

ROHO HUTUOMBEA KWA KUUGUA KUSIKOWEZA KUTAMKWA!

KIJITO CHA UTAKASO.

USHAURI KWA MWANAMKE WA KIKRISTO.

Sanduku la Agano lilikuwa linawakilisha nini katika Agano jipya?

MSHAHARA WA DHAMBI:

WAKINYAMAZA HAWA, MAWE YATAPIGA KELELE.

MAWE YALIYOKWISHA KUCHONGWA MACHIMBONI.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/03/12/je-moyo-wako-ni-mnyofu-mbele-za-mungu/