JIOKOE WEWE NA NYUMBA YAKO.

by Admin | 21 August 2020 08:46 pm08

Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe, karibu tujifunze Neno la Mungu ambalo ndio taa ya miguu yetu na mwana uiongozayo njia yetu (Zab.119:105).

Katika safari ya Imani usisahau kamwe kuifanya kazi ya Mungu kwa bidii, kuhakikisha Habari ya ufalme inamfikia kila mtu. Lakini lililo kubwa Zaidi ni kuhakikisha wewe Pamoja na nyumba yako mnaokolewa, wewe Pamoja na Watoto wako, mume wako, mke wako na Watoto wako na wote unaoishi nao wanaokolewa. Utasema hiyo inawezekana hata kama hawataki kabisa kusikia Habari za Mungu?..Jibu ni ndio inawezekana.

Kama umewahi kusoma Habari za Rahabu, utakuwa unaelewa…alipopewa nafasi ya kuokoka yeye peke yake binafsi, hakuona ni vyema kuokoka mwenyewe bali aliiokoa na familia yake yote..

Yoshua 2:12 “Basi sasa, nawasihi, niapieni kwa Bwana, kwa kuwa nimewatendea ihisani, ya kwamba ninyi nanyi mtaitendea ihisani NYUMBA YA BABA YANGU; tena nipeni alama ya uaminifu

13 ya kwamba mtawaponya hai baba yangu na mama yangu, na ndugu zangu wanaume na wanawake, na vitu vyote walivyo navyo, na kutuokoa roho zetu na kufa.

14 Wale wanaume wakamwambia, Uhai wetu badala ya uhai wenu, ikiwa hamwitangazi habari ya shughuli yetu hii; kisha itakuwa, wakati Bwana atakapotupa nchi hii, tutakutendea kwa ihisani na uaminifu”

Kama umewahi kusoma pia Habari za Lutu utakuwa unajua kuwa kabla ya maangamizi kushuka, aliondoka na mke wake na Watoto wake wawili, na baadhi ya ndugu zake pia aliwahubiria.

Na hata wakati wa Gharika..Nuhu hakuona vyema kuokoka yeye peke yake lakini biblia inasema Safina ile aliyoitengeneza ilikuwa pia ni kwaajili ya Watoto wake.

Waebrania 11:6 “Lakini pasipo imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao.

7 Kwa imani Nuhu akiisha kuonywa na Mungu katika habari za mambo yasiyoonekana bado, kwa jinsi alivyomcha Mungu, ALIUNDA SAFINA, APATE KUOKOA NYUMBA YAKE. Na hivyo akauhukumu makosa ulimwengu, akawa mrithi wa haki ipatikanayo kwa Imani”.

Umeona hapo? Anasema aliiunda ili apate kuiokoa familia yake, kwahiyo lengo la Safina halikuwa kumwokoa Nuhu tu, Mungu angeweza kumwokoa Nuhu kwa njia nyingine bila hata hiyo Safina, lakini kwasababu Nuhu alikuwa na familia na pia kulikuwa na Wanyama, Ndipo Mungu akatengeneza njia hiyo ya wokovu kwa kupita Safina.

Na kama umegundua kitu ni kwamba Mungu hakuitengeneza yeye ile Safina bali alimwambia Nuhu aitengeneze, kwasababu aliyekuwa ameonekana mwenye haki mbele za Mungu ni Nuhu peke yake, (Mwanzo 6:8) hao mwengine hawakustahili, hawakumpendeza Mungu kabisa katika njia zao, ndio maana utaona Hamu kipindi kifupi tu baada ya kutoka kwenye Safina aliutazama uchi wa Baba yake kwa makusudi, na wala hata hakusikia kitu kikimhukumu ndani yake kwa alichokifanya. (Sasa unaweza kujiuliza imekuwaje mtu kama huyo hakuangamia kwenye gharika Pamoja na waovu wengine). Jibu ni kwasababu ya Baba yao…hivyo gharama za kuwaokoa watoto wake na mke wake zilikuwa ni za Nuhu..

Hivyo Nuhu ilimbidi afanye kazi kubwa ya kutengeneza Safina ile kwa miaka mingi sana, ili tu familia yake ipone na baadhi ya wanyama.

Kadhalika utasoma pia Musa, alikuwa ni mtu wa namna hiyo hiyo, kwani ulipofika wakati wana wa Israeli jangwani walipomkasirisha Mungu kiasi cha Mungu kutaka kuwaangamiza wote, Musa alisimama kuwatetea mbele za Mungu kwa bidii.

Kutoka 22:7 “Bwana akamwambia Musa, Haya! Shuka; kwa maana watu wako uliowatoa katika nchi ya Misri wamejiharibu nafsi zao,

8 wamepotoka upesi kuiacha ile njia niliyowaamuru, wamejifanyizia ndama ya kuyeyusha wakaiabudu na kuitolea dhabihu, wakasema, Hiyo ndiyo miungu yako, Ee Israeli, iliyokutoa katika nchi ya Misri.

9 Tena Bwana akamwambia Musa, Mimi nimewaona watu hawa, na tazama, ni watu wenye shingo ngumu.

10 basi sasa niache, ili hasira zangu ziwake juu yao, niwaangamize, nami nitakufanya wewe uwe taifa kuu.

11 Musa akamsihi sana Bwana, Mungu wake, na kusema, Bwana, kwa nini hasira zako kuwaka juu ya watu wako uliowaleta kutoka nchi ya Misri kwa uweza mkuu, na kwa mkono wenye nguvu?

12 Kwa nini Wamisri kunena, wakisema, Amewatoa kwa kuwatenda uovu, ili apate kuwaua milimani, na kuwaondoa watoke juu ya uso wa nchi? Geuka katika hasira yako kali, ughairi uovu huu ulio nao juu ya watu wako.

13 Mkumbuke Ibrahimu, na Isaka, na Israeli, watumishi wako, ambao uliwaapia kwa nafsi yako, na kuwaambia, Nitazidisha kizazi chenu mfano wa nyota za mbinguni; tena nchi hii yote niliyoinena nitakipa kizazi chenu nao watairithi milele.

14 Na Bwana akaughairi ule uovu aliosema ya kwamba atawatenda watu wake”

Mifano ipo mingi sana, hatuwezi kuandika yote hapa, lakini kwa hiyo michache unaweza kuelewa kuwa sisi tuliobahatika neema ya wokovu, tunalo jukumu la kusimama kwaajili ya nyumba zetu. Bwana amekupa neema wewe mmoja, ili wengine wote katika nyumba yako waokolewe. Ni jukumu lako na si la Mungu, kupambana kwa bidii ili waingie ndani ya mlango huu wa Neema, kama Musa alivyopambana, kama Nuhu alivyopambana, kama Lutu alivyopamba na kama Rahabu alivyopambana. Na hiyo inakuja kwa kuwaombea kwa bidii na si kuwahukumu, inakuja kwa kuhubiria wanao kwa bidii sana Habari za wokovu, kwa kumhubiria mkeo au mumeo na kumwombea..huku wewe mwenyewe ukionyesha kumpendeza Mungu na kutokuiga wala kufanya matendo kama yao.

Kwa kufanya hivyo ipo neema ya wokovu ambayo itamwagika kwa watu wa nyumbani kwako pia, nao pia mwishoni wataokolewa kama wewe. Hivyo hupaswi/hatupaswi kufurahia wokovu ukiwa kwetu tu!.. tunapaswa tufurahie ukiwa kwa wengine pia.

Mwisho kabisa. Bwana anakaribia kurudi, mambo yote ya ulimwengu yatabatilishwa, na mlango wa neema utafungwa Bwana Yesu alisema wengi watatamani kuingia siku hiyo wasiweze. Hivyo kama hujampokea Yesu na unasoma jumbe hizi kila siku, au jumbe nyingine zinazofanana na hizi, basi siku ile hutasema hukusikia, nakushauri yakabadhi Maisha yako kwa Yesu, yeye ndiye Njia, kweli na Uzima..hakuna namna utaweza kuiona mbingu kama unakataa Habari za uzima sasa.

Bwana atubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

HATUTAACHA KUJIFUNZA NENO KILA INAPOITWA LEO.

Je ni kweli huwezi kuijua karama yako mpaka uwekewe mikono na wazee?

USHAURI KWA MWANAMKE WA KIKRISTO.

Yesu ni Mungu?, Na Kama ni Mungu kwanini alikufa?

HUYU SI YULE SEREMALA, MWANA WA MARIAMU?

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 2

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/08/21/jiokoe-wewe-na-nyumba-yako/