HATUTAACHA KUJIFUNZA NENO KILA INAPOITWA LEO.

HATUTAACHA KUJIFUNZA NENO KILA INAPOITWA LEO.

Je! Kuna umuhimu wowote wa kujifunza Neno kila siku?

Unajua ni kwasababu gani leo hii tunaomwona Mtume Paulo ni mtu aliyekuwa amejaa mafunuo ya ndani kabisa yamuhusuyo Mungu na YESU KRISTO kiasi cha Mungu kufikia hatua ya kuyafanya mafundisho yake kuwa muhamala mkuu wa kanisa hadi sasa, ni kwasababu mtume Paulo hakuwa mtu wa kuchoka kusoma na kujifunza neno kila iitwapo leo,..Hakuwa mtu wa kulizoelea Neno la Mungu…

Tunaweza kuona mpaka wakati wa kukaribia kufa kwake, wakati anampa Timotheo maagizo ya kuliongoza na kulichunga kanisa, ameshakuwa mzee kabisa amebakisha kipindi kifupi sana cha kuishi, lakini bado anamwagiza Timetheo ampelekee vitabu vya nyaraka za maandiko avisome, kwasababu alijua bado anayo mengi ya kujifunza..

2Timotheo 4:6 “Kwa maana, mimi sasa namiminwa, na wakati wa kufariki kwangu umefika.

7 Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda;

8 baada ya hayo nimewekewa taji ya haki, ambayo Bwana, mhukumu mwenye haki, atanipa siku ile; wala si mimi tu, bali na watu wote pia waliopenda kufunuliwa kwake.

……… 13 Lile joho nililoliacha kwa Karpo huko Troa, ujapo ulilete, na vile vitabu, hasa vile vya Ngozi’

Paulo mtu aliyehubiri Injili tangu ujana wake, Aliyekutana na Yesu uso kwa uso, alifunuliwa siri za ndani kabisa ambazo hata Mitume wengine hawakufunuliwa wakati wakiwa na Bwana Yesu hapa duniani.,..Aliyenyakuliwa mpaka mbingu ya tatu, na kuonyeshwa mambo ambayo hayaelezeki kwa namna ya kibinadamu, lakini bado mtu kama huyo hakuchoka kujifunza neno mpaka siku ya kufa kwake…Bado aliendelea kusoma kwa bidii, akitazamia Mungu kumfunulia mambo mpya ambayo hakuwahi kuyafahamu..Anamwambia Timotheo, Ujapo uvilete vile vitabu vya ngozi..

Hii inatufundisha kuwa kupokea mafunuo ni kitendo endelevu, hatupaswi kuridhika tu na kile tunachokifahamu au tulichopewa kukijua sasa na Mungu bali kila siku tunapaswa tumwombe Mungu azidi kutufumbua macho Zaidi na zaidi katika Neno lake, na kutia bidi katika kusoma Neno lake.

Ndicho alichokifanya Danieli, yeye mwanzoni kabisa ukisoma ile sura ya pili ya kitabu cha Danieli, utaona Mfalme Nebukadneza aliota ndoto ya ile sanamu kubwa yenye kichwa cha dhahabu, kifua cha fedha, kiuno cha shaba na miguu ya chuma..Ambayo Danieli alipewa tafsiri yake inayohusiana na falme 4 zitakazotawala ulimwenguni mpaka mwisho wa dunia..

Lakini utaona Danieli hakuridhika na ufunuo ule peke yake, utaona kwenye sura ya 7 anaonyeshwa mambo ya ndani Zaidi kuhusiana na zile falme 4, ambayo hakufunuliwa katika ile njozi ya kwanza ya Mfalme Nebkadneza, alionyeshwa tabia ya zile falme jinsi zitakavyosimama na kuanguka…Ukiendelea kusoma sura ya 8 utaona tena anaelezwa mambo ya ndani Zaidi jinsi falme zile zitakavyokuwa..Ukizidi kusoma kuanzia ile sura ya 11 hadi ya 12 sasa Ndivyo utakavyooona jinsi Danieli anafunuliwa mambo yote kwa uwazi anaelezwa tukio baada ya tukio kikitoka hichi kinafuata hichi, kuanzia ule ufalme aliokuwepo mpaka ule unaomfuata baada yake…

Ndipo Danieli akaelewa sasa, na ukisoma pale utaona alitamani kuendelea kufahamu Zaidi juu ya matukio ya siku za mwisho, lakini malaika yule alimwambia aache hayo si ya wakati wake bali ayatie muhuri yatafunuliwa siku za mwisho..Ni wazi kuwa kama asingeambiwa vile basi Danieli angetusaidia kujua kila tendo litakalotokea katika siku zetu hizi za mwisho.

Lakini kama angesema Ah! Huu ufunuo Mungu atakaonipa wa ziada kuhusu ndoto ya Mfalme Nebukadneza. Ule alionipa unatosha hakuna haja ya kujifunza neno na kumwomba Mungu anifunulie Zaidi basi Danieli angebakia kujua tu zipo falme 4 zitakazotawala mpaka mwisho wa dunia basi, lakini habari za chukizo la uharibifu asingezijua, habari za hukumu ya mwisho asingezijua, habari za kuja kwa masihi asingezijua, habari za Kristo kusulibiwa asingezijua, habari za majuma sabini asingejua, habari za dhiki kuu asingezijua…Endapo tu angeridhika na hali ile ile ya ufunuo aliyopewa. Na hata ukizidi kusoma utagundua Danieli alikuwa mtu msomaji sana wa vitabu, mpaka akafikia kugundua miaka Israeli waliyotabiriwa kukaa Babeli.

Danieli 9:2 “katika mwaka wa kwanza wa kumiliki kwake, mimi Danielii, kwa kuvisoma vitabu, nalifahamu hesabu ya miaka, ambayo neno la Bwana lilimjia Yeremia nabii, ya kuutimiza ukiwa wa Yerusalemu, yaani, miaka sabini”

Vivyo hivyo na sisi Mungu atusaidie tujifunze, juu ya mambo haya, tusiridhike katika hali tuliyopo, tukaona kwamba kwasababu tumeisoma biblia nzima basi hakuna jambo jipya tunaweza kujifunza tena, kwasababu tumeshausoma mstari huu au ule, basi huyu muhubiri hawezi kutuambia tena jambo jipya hapo..Neno la Mungu halina ubobeaji..

Mungu anataka sisi tukue kifikra, tukue kiimani, vilevile tukue kiroho, kutoka katika hali ya uchanga hadi hali ya utu uzima kuelewa mambo ya ndani kabisa ya rohoni.. Mafumbo magumu na hiyo yote ni kama tutakuwa tayari kujifunza neno kila siku maneno ya Mungu pasipo kuyazoelewa.

Mungu akubariki sana. Ikiwa bado hujaokoka, nadhani utakuwa unafahamu kuwa hizi ni siku za mwisho, na kwamba moja ya hizi siku parapanda italia, na wafu watafufuliwa, na kuungana na watakatifu waliopo duniani na kwa pamoja kwenda kumlaki Bwana YESU mawingu. Kuelekea katika karamu ile ya mwanakondoo, ambayo Mungu aliindaa tangu enzi na enzi kwa wale waliookolewa..Sasa utajisikiaje ikiwa wewe utakosekana katika karamu hiyo? Mimi sitaki kukosa wewe je?..Utajisikiaje umebaki huku duniani kwenye dhiki ya mpinga kristo halafu baada ya hapo uishie kwenye ziwa la moto?..Angalia jinsi Mungu alivyotupenda, kutupa YESU KRISTO ili atuokoe sisi bure kwa damu yake.

Hivyo anakuita na wewe ayaokoe Maisha yako. Tubu popote pale ulipo, ukabatizwe kisha atakupa amani ambayo utadumu nayo hadi siku ya kuja kwake.

Ubarikiwe sana.jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP

Mada Nyinginezo:

RUDIA, TENA NA TENA KUMWOMBA MUNGU USIKATE TAMAA.

TABIA YA KIPEKEE USIYOIJUA KUHUSU NENO LA MUNGU.

JISHUSHE ILI MUNGU AKUHUDUMIE.

UNATAKA KUBARIKIWA? BASI USIKWEPE GHARAMA ZAKE.

Ni sahihi kumuita Mariamu mama wa Mungu?

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments